Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Mpango wa Tatu wa Maendeleo wa Taifa kwa Kipindi cha Miaka Mitano kuanzia mwaka 2021/2022 – 2025/2026

Hon. Ng'wasi Damas Kamani

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Mpango wa Tatu wa Maendeleo wa Taifa kwa Kipindi cha Miaka Mitano kuanzia mwaka 2021/2022 – 2025/2026

MHE. NG’WASI D. KAMANI: Mheshimiwa Naibu Spika, nami nianze kwa kushukuru kwa nafasi hii ya kuchangia katika Mpango huu jioni ya leo. Nianze pia kwa kutoa pole kwa familia ya Dkt. John Pombe Magufuli, Watanzania wote, viongozi wote kwa msiba huu mzito ambao ulitutikisa kama Taifa, lakini pia nizidi kutoa pongezi nyingi niungane na Wabunge wenzangu kwa Rais wetu Mama Samia Suluhu Hassan, kwa trend nzuri ambayo ameanza nayo ambayo inatoa matumaini makubwa kwa Watanzania wote.

Mheshimiwa Naibu Spika, ningeomba mchango wangu wa leo nianze kwa kutoa mfano wa mfumo wa familia ya Kisukuma. Wote tunaweza kuwa tunafahamu kwamba sisi Wasukuma tunaishi kwenye familia ambazo ni extended, familia yenye watoto wachache sana ni watoto kumi na kuendelea na familia ambayo ina watoto wengi ndio inakuwa familia tajiri Zaidi katika kile kijijini. Hii ni kwa sababu watoto hawa ndio kama source of labour ndio watatumika wakienda kuchunga, watagawa vizuri majike yatachungwa vizuri, madume yatachungwa vizuri, ndama zitachungwa vizuri jioni zikarudi zimeshiba. Pia kama wakienda shambani watoto hawa wakiungana kwa pamoja maana yake heka nyingi zitalimwa, lakini pia hata kama mtoto wa familia ile akitaka kuoa anajengewa pale pale pembeni ili aoe na yeye azae waungane wote pamoja.

Mheshimiwa Naibu Spika, maana ya kutoa mfano huu ni nini? Asilimia zaidi ya sitini ya wananchi wa Taifa hili ni vijana, lakini nasukumwa kuamini kwamba Serikali haitaki au haijaona umuhimu wa kutumia wingi huu wa vijana wenye nguvu na ambao wako tayari kutumikia Taifa hili kama ambavyo familia ya Kisukuma inatumia watoto wake wengi ili kujipatia zaidi na kuwa tajiri. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, changamoto yetu kubwa sisi ni ukosefu wa ajira, lakini kwa nini kwa wingi wetu huu, bado Serikali yetu inaweza ikatumia pesa nyingi sana kuangiza mafuta ya kula kila mwaka, wakati kwa mwaka tunaweza kutumia pesa hizi, tumeshaambiwa na Mheshimiwa Kingu na wengine kwamba wapo tayari kutupa maeneo, Serikali ikaanzisha kambi, ikaweka miundombinu, vijana wakawekwa pale wakalima alizeti, wakalima michikichi na namna nyingine zote tukapata mafuta ya kutosha tuka-save pesa za Taifa letu.

Mheshimiwa Naibu Spika, pia tunaweza tukaamua kutumia vijana hawa hawa katika kazi nyingine nyingi miradi mingi ya kimkakati, vijana ambo wana ari ya kufanya kazi, kulitumikia Taifa hili kuliingizia kipato. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, namna pekee ambayo tunaweza kuweza kufanya hivyo, kwanza kabisa ni kuhakikisha tunakomboa vijana hawa kifikra kwa maana ya kuboresha mfumo wa elimu. Pili, tuwe na national agenda au vipaumbele vya Kitaifa ambavyo tutawaonesha vijana hawa kwamba Taifa letu linaelekea huku na Serikali yetu ikafanya juhudi za makusudi za kuhakikisha kwamba zinawezesha vijana hawa kuendana na vipaumbele vya Kitaifa na mwisho tunakomboa Taifa letu kiuchumi.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwenye suala la elimu, naomba nitoe takwimu chache tu. Mwaka 2014, wanafunzi wapatao 885,000 walimaliza darasa saba, mwaka 2018 walimaliza form four lakini walimaliza wanafunzi 425,000 na mwaka huo walipomaliza form four wanafunzi 121,251 wakachaguliwa kujiunga na kidato cha sita na vyuo vya ufundi. Hata hivyo, mwaka 2020 ni wanafunzi 84,212 tu ndio wamemaliza, maana yake wanafunzi 725,645 wako wapi ambao walimaliza darasa mwaka 2014 na mwaka 2020 hawakumaliza kidato cha sita wala vyuo vya ufundi.

Mheshimiwa Naibu Spika, pia VETA zetu zote nchi nzima at high capacity zina uwezo wa ku-accommodate watu 150,000 hadi 170,000 tu, wale wengine waliobaki wanakwenda wapi. Pia wote tunakubaliana katika michango yetu Waheshimiwa Wabunge wote tangu mwanzo wa Bunge hili mpaka sasa wame-hint kwamba mfumo wetu wa elimu haumwandai kijana kuweza kubaki kwenye jamii na kuitumikia jamii yake kwa kujiajiri mwenyewe, vijana hao wanaobaki wanakwenda wapi? Ndio huku huku tunazidi kuzalisha magenge ya wezi na majambazi, lakini sisi ndio tumezalisha watu hawa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nasema haya ili niseme nini, ushauri wangu; kuna mifumo mingi ambayo imeanzishwa na Wizara zetu na Serikali yetu ya kuhakikisha kwamba tuna- remedy suala hili ikiwa ni pamoja na kuanzisha program za internship na apprenticeship, kuwapa watu elimu ya vitendo ili wawe tayari kuingia kwenye soko la ajira. Hata hivyo, Serikali yetu kila mwaka imekuwa inatenga pesa nyingi sana kwa ajili ya mifumo hii. Pesa hii hii ambayo ingeweza kutumika kurudi kwenye mifumo yetu ya elimu, tukaboresha mifumo yetu, tukaanza kuwafundisha watu vitu ambavyo ni relevant kwa mazingira ya Kitanzania na tuka-save pesa nyingi za Serikali zizazotumika kuweka mifumo ya internship na apprenticeship. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kuna mambo mengi ambayo tumekuwa shuleni tumefundishwa, lakini mpaka leo applicability yake hatujaona kwenye maisha ya kawaida. Hii ni kwa sababu mfumo wetu wa elimu umekuwa static, kitu ambacho walijifunza watu miaka 20 iliyopita, wanajifunza hawa hawa wa miaka ya leo, lakini dunia inabadilika. Ushauri wangu kwa Serikali na Wizara ya Elimu, suala la elimu liwe suala la kubadilika, liwe revolving issue, watu wafundishe vitu ambavyo vinakwenda na muda, kitu alichojifunza jana kilikuwa relevant leo sio relevant tena tuache, tuanze kufundisha watu vitu vinavyokwenda na wakati, ikiwa ni pamoja na elimu ya vitendo ambayo itamsaidia kijana, hata akiamua kwamba siendelei mbele naishia darasa la saba, naishia form four, naishia form six au labda naenda mpaka chou, ana uwezo wa kurudi kwenye jamii, kuitumikia jamii yake akazalisha kujikomboa yeye, familia yake na kujenga uchumi wa nchi kwa ujumla. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, suala la pili, nimezungumzia suala la kutengeneza vipaumbele vya Taifa au National Agendas. Nitoe tu mfano leo kaka yangu Kingu amezungumzia suala la Misri na namna gani wamebadilisha kutoka jangwa na kuwa wazalishaji wakubwa sana wa vyakula vingine vingi, land reclamation Egypty ilikuwa ni National Agenda ambayo ilibebwa iwe, isiwe lazima wai- achieve. Nchi zetu za Afrika hasa sisi labda Watanzania National agenda zinakwenda na uongozi unaoingia, hatuja- define agenda zetu sisi kama Taifa labda kwa miaka 20 au 30 kwamba iwe isiwe, inyeshe mvua, liwake jua, sisi tutakwenda na mkondo huu tu mpaka tuhakikishe kwamba tumeufanyia kazi na ume-bear fruits.

Mheshimwa Naibu Spika, kwa hiyo kila atakayeingia maana yake ataingia na vipaumbele vyake na vipaumbele hivi ni vyema, lakini labda muda ule ambao tunakuwa tunawapa viongozi wetu ni mfupi. Akiingia mwingine akaingia na lingine maana yake bidii yote, resources zote zilizokwishatumika zinaishia pale, tunaanza na vitu vingine, kitu ambacho tunapoteza rasilimali nyingi. Hata hivyo, wananchi wetu watashindwa kuelewa majukumu yao Kitaifa ni yapi, Taifa letu linatoka wapi linaenda wapi, tujikite wapi na tukiwa na vipaumbele hivi itasaidia sasa Serikali nayo kuhakikisha kwamba inachukua steps za msingi. Let say tumesema sasa hivi ni Serikali ya viwanda na mkondo wetu Kitaifa ni viwanda maana yake ni nini?

Mheshimiwa Naibu Spika, maana yake ni kwamba, Serikali itahakikisha kwenye suala la viwanda inaondoa urasimu wote, inarekebisha au kufuta baadhi ya kodi ili wavutike na kuingia kule kwenye viwanda. Tukikaa na mkondo huu kwa miaka 20 maana yake viwanda nchi kwetu, by the time tunabadilisha kwenda kwenye kipaumbele kingine viwanda vimesimima na nchi yetu kwenye suala hilo imekwishakaa vizuri. Kwa hiyo, naomba Serikali ikae chini, iangalie kwamba vipaumbele vyetu ni vipi na wananchi waambiwe na waambiwe majukumu yao na Serikali iji- dedicate kwenye vipaumbele hivyo kuhakikisha inavirahisha kiasi ambacho mwananchi yeyote yule ana uwezo wa kuingia na kufanya kazi katika vipaumbele hivyo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwetu sisi vijana imekuwa changamoto sana kuingia kwenye hizi biashara kwa sababu bado hakuna urafiki wa kukaribisha mtu anayeanza biashara au anayeanza uwekezaji kwenye nchi yetu. Mtu akiingia mtaji wenyewe ame-struggle, amekopa halmashauri, kakopa benki, dhamana inasumbua, lakini akiingia nusu robo tatu yote inatakiwa iende ikalipie leseni, ikalipie kodi na vitu vingine, kwa hiyo tunawakatisha tamaa. Tuki-define vipaumbele vyetu, maana yake mtu anajua sasa hivi kuna urahisi wa kwenda huku, wananchi wote wanajua tunaelekea wapi na nini tunafanya. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nitoe mfano kutoka kwenye Nchi ya Thailand; ukifika kwenye nchi ile, ukishuka tu Airport unaulizwa hii ni mara yako ya kwanza kufika au wewe ni mwenyeji hapa. Ukisema ni mara yako ya kwanza unaanza kupewa vipaumbele; nchi yetu ina hiki, hiki na hiki , kabla hujaondoka tafadhali tembelea hapa na hapa, maana yake ni uzalendo ambao wananchi wa kawaida wamekwishajiwekea kwa kutambua vipaumbele vya nchi yao wapi inakwenda na wanaitangaza kidunia. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kusema hayo machache, la mwisho kabisa nimalizie kwa kumshukuru sana Mheshimwa Rais kwa msimamo mzuri alioutoa katika hotuba yake ya mwisho juu zima ya suala ya bando au mitandao. Vijana wengi pamoja na kuwa ajira ni changamoto, wengi tunatumia sana sana mitandao hii kujiajiri. Tunafanya biashara za mitandaoni, lakini hata pia kwenye kusoma, tunasoma kupitia mitandao, lakini hata kwenye sanaa na michezo, wasanii wetu wanategemea kupitia you tube na namna nyingine zingine zote ndio sisi tukaona kazi zao na kuzinunua. Kwa hiyo kidogo changamoto hii ilikuwa inatupeleka kwenye shida kubwa sana na nimshukuru sana Mheshimiwa Rais na niombe Wizara hii husika basi iliangalie suala hili ili lisije likajirudia tena. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru sana. (Makofi)