Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Mpango wa Tatu wa Maendeleo wa Taifa kwa Kipindi cha Miaka Mitano kuanzia mwaka 2021/2022 – 2025/2026

Hon. Issa Ally Mchungahela

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Lulindi

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Mpango wa Tatu wa Maendeleo wa Taifa kwa Kipindi cha Miaka Mitano kuanzia mwaka 2021/2022 – 2025/2026

MHE. ISSA A. MCHUNGAHELA: Mheshimiwa Naibu Spika, nikushukuru wewe kwa kunipa nafasi hii. Pia nitangulize pongezi zangu kwa watu wote waliopa bahati ya kuchaguliwa kuwa Mawaziri na Manaibu Mawaziri kwenye nafasi zote.

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema hayo nampongeza pia Mheshimiwa Rais, mama yetu kwa kuonyesha njia ya jinsi tutakavyoelekea Tanzania kwa kipindi hiki japo tulikuwa tunashaka kidogo tukifikiria kwamba itakuwaje baada ya kupata msiba mkubwa tulioupata angalau sasa hivi tunaona kidogo kuna hali tunaweza kuelekea sehemu. Nashukuru kwa hilo na tumshukuru Mwenyezi Mungu kwamba ametuona. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema hivyo, kwanza pia niwapongeze wananchi wangu wa Jimbo la Lulindi kwa kunichagua nawahakikishia kwamba sitawaangusha hata mara moja. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nimejaribu kuangalia jinsi mwenendo mzima wa huu Mpango ulivyokwenda ni mpango mzuri sana ambao kwa muda mrefu sana tulikuwa tukiusubiri mpango wa namna hii. Kwa kweli hakuna shaka juu ya mpango huu, lakini nafikiri kwa namna moja au nyingine najielekeza katika kuchangia baadhi ya mambo katika mpango huu, hususani katika fursa ambazo kwa namna moja au nyingine tunaweza tukazitumia sisi kama Watanzania.

Mheshimiwa Naibu Spika, upande wa kusini kwa mfano, tuna fursa kubwa sana eneo lote la Mkoa wa Mtwara ni eneo la fursa ambalo tunaweza tukalitumia vizuri sana kujielekeza na kujikita kwenye biashara na nchi takribani tatu au nne. Hiyo ni advantage kubwa sana na mfano, ukiangalia kusini kule Mtwara tuna ukaribu kabisa moja kwa moja na Nchi ya South Afrika na Nchi ya Mozambique lakini pia tuna ukaribu na nchi ya Comoro, hali kadhalika tuna ukaribu na nchi ya Madagascar. Hizi nchi kwa namna moja au nyingine kama tutajikita kufanya nazo biashara, kwa sababu kwanza zenyewe zina mapungufu mengi sana ambayo wanayategema sana yanaweza yakasaidiwa na sisi uimara wetu katika kuwekeza. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa mfano, tunayo bandari kubwa ambayo haina shida, mpaka sasa imetengenezwa kwa kiasi kikubwa kabisa lakini pale ni lango pia ambalo la kuweza kutokea nchi nyingi kwenye bandari hiyo. Kwa sababu kama unavyoangalia ile Bahari ya Hindi imeunganika moja kwa moja katika hizi nchi, lakini sisi tunazalisha vitu vingi hususani mazao ya kilimo ambayo kwa namna moja au nyingine wenzetu kule hawawezi kuzalisha kwa mfano Nchi ya Comoro. Pia tunazalisha mifugo ambayo Nchi ya Comoro hawawezi kuzalisha, sisi tunaweza kuitumia nafasi hii kwa kuwauzia kwa kiwango kikubwa kabisa tukapata pesa za kutosha. (Makofi.)

Mheshimiwa Naibu Spika, kama tulivyosema Bandari ya Mtwara, moja kwa moja kwa makusudio yetu yale ya kuunganisha reli ya standard gauge kwenda Mbamba Bay lakini kupitia Mchuchuma na Liganga moja kwa moja, hapo tunaona kwa jinsi gani hizi products zinazozalishwa kwenye Liganga na Mchuchuma kwa mfano chuma na makaa ya mawe, tuna uwezo wa kuwauzia moja kwa moja nchi hizi ambazo nimeziataja hapa kirahisi kabisa. Kwa namna moja au nyingine pia bandari hii inaweza ikawa ni kiunganishi cha nchi nyingi sana hasa hasa zilizounganikaunganika kwa upande kwa kusini.

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo lingine ambalo naliona kwa sababu Mkoa wa Mtwara unazalisha zao kubwa la korosho ambalo kwa namna moja au nyingine siku zinavyokwenda limekuwa zao linalopendwa kwa matumizi na watu wengi sana inakuwa ni rahisi kwa namna moja au nyingine kuziuza korosho zetu katika nchi hizo ambazo nimezitaja. Kwa hiyo tunaweza kuona jinsi gani Mkoa wa Mtwara unaweza ukawa umetumika kwa namna moja au nyingine ikawa kama mkoa mkakati wakusambaza uchumi wetu, lakini na kuhakikisha kwamba uchumi wetu unakua kiasi kikubwa.

Mheshimiwa Spika, naona kwamba, bado hatujachelewa, lakini kuna gesi ambayo Mtwara imekuwa ni kitovu kikubwa sana cha gesi ambayo mpaka sasa hivi haijatumika vya kutosha. Naomba Serikali ifanye jitihada ya kutosha kabisa kuhakikisha gesi Mtwara inatumika. Sijajua tatizo ni nini mpaka sasa hivi ambalo linatukwamisha. Ningeomba Wizara husika ifanye mkakati wa kutosha kabisa kuhakikisha kuona gesi hii inatumika kama vile tumetegemea itumike.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuna eneo la uzalishaji katika masuala ya kilimo, Mkoa wa Mtwara hauko nyuma pia katika uzalishaji wa mazao mengine ukiachia korosho ambao ni zao maarufu. Mkoa wa Mtwara ni maarufu pia katika kuzalisha ufuta ambao ni kigezo kikubwa kabisa cha kupunguza hili gap ya matatizo ya mafuta ya kupikia kama tutaweka nguvu za kutosha kidogo kwenye ufuta, lakini korosho na mazao mengine bila shaka Mtwara itakuwa ni sehemu mojawapo inatusaidia sana kupunguza shida hasa hasa katika suala zima la kupunguza matatizo ya mafuta yanayohitajika katika nchi yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pia niweze kuzungumzia suala la miche ya korosho ambayo ilikuwa imelimwa na wajasiriamali wadogo wadogo kwa minajili ya kwamba ilikuwa ikatumike kwenda kuwekezwa katika maeneo mengine ambayo hayalimi hiyo miche. Wawekezaji wale mpaka sasa hivi wamekuwa wakilalamika kwamba hawajalipwa stahiki zao baada ya kuwa wametumia nguvu nyingi sana, lakini pia na kutumia pesa zao katika kuwekeza hiyo miche ambayo namna moja au nyingine ilizalishwa ikaiuzia Serikali kupitia Mamlaka ya Korosho lakini mpaka sasa hivi wananchi wale wanalalamika hawajalipwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, naiomba Serikali kwa jicho la huruma kabisa iwasaidie hawa wawekezaji wadogowadogo kwa sababu wao ni sehemu kubwa kabisa ya maendeleo ya nchi hii kama vile ilivyokuwa wawekezaji wa maeneo mengine, hususani ukizingatia kwamba hawa ni wakulima ambao hutegemea kidogo sana wanachokuwa nacho waweze kukiwekeza sehemu nyingine wajipatie mkate wa siku zote.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa namna moja ama nyingine hapo ni kama nimchomekea tu maana yake nilijua sitapata nafasi ya kulizungumza hili, nimejaribu kulizungumza kwa mara mbili, mara ya tatu, sijalipatia jibu, naomba japo sio mahali pake hapa, lakini kwa taadhima Waziri husika atuonee huruma watu wa Mtwara, aweze kuwapa wale watu waliowekeza katika ile miche ya korosho wanachostahili angalau waweze kusukuma mbele kidogo maisha yao, japo najua sio mahali pake hapa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya hapo, najaribu kujielekeza pia katika suala zima la gesi kwa ujumla. Gesi kwa namna moja au nyingine imekuwa ni tegemeo kubwa katika eneo la Mtwara, lakini hata kwa Tanzania kwa ujumla, nafikiri itakuwa sehemu ya mojawapo itakayotusaidia kutatua baadhi ya changamoto ndogondogo ambazo kwa namna moja au nyingine tungeweza kushindwa kuzitatua.

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya hapo, naomba nishukuru kwa kupata nafasi hii ya kuchangia. Ahsante. (Makofi)