Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Mpango wa Tatu wa Maendeleo wa Taifa kwa Kipindi cha Miaka Mitano kuanzia mwaka 2021/2022 – 2025/2026

Hon. Kasalali Emmanuel Mageni

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Sumve

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Mpango wa Tatu wa Maendeleo wa Taifa kwa Kipindi cha Miaka Mitano kuanzia mwaka 2021/2022 – 2025/2026

MHE. KASALALI E. MAGENI: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa nafasi naomba nimshukuru Mwenyezi Mungu kwa uhai na uzima lakini pia nitumie fursa hii kutoa pole kwa Watanzania na mimi mwenyewe kufuatia kifo cha Rais wetu wa Awamu ya Tano Rais wetu aliyekuwa amejikita kwenye kuhakikisha anatuletea maendeleo ya kweli Watanzania Hayati Dkt John Pombe Magufuli tunamuombea huko aliko apate pumziko jema na sisi tulioko huku tuendelee kuchapa kazi ili kutimiza malengo waliyonayo Watanzania na matumaini waliyonayo na Serikali yetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, pia nimpongeze Rais wetu mama Samia Suluhu Hassan na Makamu wake na Serikali yote na niwakaribishe katika kuchapa kazi sisi tupo tutaungana nao na tutawaunga mkono kuhakikisha kazi ina kwenda ipasavyo.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba sasa nijielekeze katika mpango wa bajeti ambao umewasilishwa leo Bungeni hapa. Ukiangalia Mpango huu unaona yapo matumaini ndiyo maana naanza kwa kuunga mkono lakini yapo mambo ya kuzingatia ambayo nilitaka tuyazungumze kidogo kwenye Bunge lako.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nizungumzie kuhusu mambo ya vijijini kwasababu ni moja ya Wabunge wenye Majimbo ya vijijini, huko vijijini asilimia kubwa ya watu ni wakulima na sekta ya kilimo imekuwa ni uti wa mgongo wa Taifa letu lakini sisi kule kijijini ndiyo Maisha yetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kupitia Bunge lako niiombe Serikali katika sekta ya kilimo mnatakiwa sasa ifike tuanze kuwekeza katika kuboresha sekta hii kuanzia kwenye uzalishaji. Kumekuwa na utaratibu ambao umekuwa ukinishtua nadhani kwenye kikao kilichopita nilisema wakulima wakati tunazalisha mazao yetu Serikali imekuwa ikikaa kimya ikituangalia inapofika wakati wa kuvuna mazao yetu unaanza kuona vitu vinaitwa AMCOS unaanza kuona vitu vinaitwa Stakabadhi Ghalani, unaanza kuona usimamizi ambao si rafiki kwa wakulima. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwenye Jimbo la Sumve tunalima mazao ya jamii ya kunde hizi choroko na dengu ni mazao ambayo sisi wakulima tunayalima kwa nguvu zetu wenyewe hatujawahi kuona mbegu kutoka Serikalini, hatujawahi kuona dawa kutoka Serikalini, hatujawahi kuona Afisa Ugani kutoka Serikalini lakini inapofika wakati wa kuyauza unaanza kuona kuna watu wanaitwa AMCOS, kuna watu wanaitwa Ushirika wanakuja kusimamia mazao ambayo tumeyalima sisi wenyewe kwa nguvu zetu wenyewe. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini zaidi wanaleta utaratibu wa hovyo utaratibu ambao hautusaidii bei zimeshuka sasa hivi ukienda kwenye maeneo ambayo yanalima hizi choroko na dengu tunakaribia kuanza kuuza choroko soko lake limeporomoka kwa wakulima. Wakulima wameshindwa kabisa kufaidika kwa hiyo, naomba Serikali muwekeze zaidi kwenye uzalishaji kabla hamjaamua kuwekeza kwenye kutupangia namna ya kuuza mazao yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, hili ni lazima mliangalie kwa undani hamuwezi kuweka mazao yote kwenye kapu moja zao kama choroko na dengu huwezi kulifananisha na korosho. Dengu sisi na choroko Wasukuma ni zao la chakula na biashara kuna mtu anahitaji kwenda kununua dengu sokoni akapike atumie lakini wewe umemwambia ili aziuze lazima apeleke AMCOS.

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali yetu amezungumza hapa Mheshimiwa Tabasamu kuhusu zao la pamba, ni Mbunge ninayetoka kwenye jimbo la wakulima wa pamba. Wilaya ya Kwimba ni moja ya wilaya ambazo zinazalisha pamba kwa wingi kuliko zote kwenye Mkoa wa Mwanza zao la pamba niwaambie kabisa Serikali mmeshiriki kuliua na mnaendelea kushiriki kupitia namna ambavyo mnasimamia masoko yake. Wakulima wengi wa Tanzania tunalima hatujui hata kama tunapata faida au hasara huwa tunalima tu lakini ukifanya hesabu asilimia kubwa tunapata hasara. Lakini bado Serikali kwenye kusimamia bei za mazao bado haijaonekana kwamba tuko serious kwasababu tunapeleka watu kwenda kusimamia vitu wasivyovijua.

Mheshimiwa Naibu Spika, zao la pamba asilimia kubwa linasimamiwa na watu wasiolijua na limeingiliwa amesema Mheshimiwa Tabasamu hapa hawa siyo wawekezaji ni mabeberu ni watu ambao wanakwenda kumdidimiza mkulima. Kwa hiyo, ni lazima Serikali muangalie Mheshimiwa Waziri wa Fedha muone namna ambavyo mtalifufua zao la pamba kwasababu tunataka viwanda, viwanda vinatoka wapi kama mazao tunayaua.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini huko vijijini kwetu ambako ndiko tunakozalisha mazao haya ya chakula ambayo watu wa mjini wanatumia lakini ndiko nguvu kazi nyingi iko kule, bado tunazo changamoto za miundombinu. Katika mpango wa bajeti nimeona tunazungumza kuhusu miundombinu mikubwa mikubwa kama reli ya kati tunazungumza madaraja lakini pia sisi kule site vijijini kuna miundombinu ya kwetu ya kawaida kabisa mabarabara ya vijijini kupitia TARURA bado hali vijijini si nzuri barabara za Dar es Salaam zisipopitika utaona watu wamepiga picha zimeonekana kwenye mitandao Serikali imeenda kurekebisha. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini barabara za Sumve asilimia kubwa hazipitiki vijijini kuna kata zingine kama Kata ya Mwabomba ikinyesha mvua ikakukuta uko kule kama una pikipiki unaacha unatembea kwa mguu. Kwa hiyo, bado kabisa tunatakiwa tuwekeze pesa kwenye miundombinu ya vijijini ili wakulima wetu waweze kusafiri waweze kusafirisha mazao lakini pia ipo miundombinu ya kimkakati ambayo inawezekana hatujaiona sana.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuna barabara ambayo imekuwa ikiongelewa sana tangu mimi nimekuwa chaguzi zote za Chama cha Mapinduzi za vyama vingi imekuwa ikitajwa barabara yenye urefu wa kilometa 71 inayotokea Hungumarwa kupita Ngudu kwenda mpaka Magu. Barabara hii ni barabara ya kimkakati ambayo imesahaulika. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwenye mpango huu pia nimeiona imezungumzwa lakini imezungumzwa katika ile stori ya kutenga pesa na mipango ya baadaye. Lakini imeanza kuzungumzwa niko darasa la tatu. Sasa barabara hizi za kimkakati kwasababu barabara hii ikijengwa kwa kiwango cha lami inapunguza umbali wa mtu anayesafiri kutokea Shinyanga kwenda nchi Jirani ya Kenya au Mkoa wa Mara au Wilaya ya Magu kwa kilometa zaidi ya 83. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, barabara hii ukiijenga unakuwa umeokoa uchumi tunaposema kukuza uchumi barabara za kimkakati ndiyo hizi. Hii ni barabara ambayo inaweza ikafungua mbali na kufungua wilaya ya Kwimba kuongeza mapato kuongeza mzunguko kwasababu Wilaya ya Kwimba ni wilaya pekee ambayo kwenye Mkoa wa Mwanza haijui maana ya lami kwenye Makao Makuu yake kwa hiyo, barabara hii ikipita itafungua uchumi wa Wilaya ya Kwimba. Lakini siyo tu uchumi wa Wilaya ya Kwimba itafungua uchumi wa kanda ya Ziwa na uchumi wa Taifa kwasababu tunahitaji mizigo inayopelekwa nchi jirani ya Kenya iende kwa urahisi zaidi, tunapunguza uhai lakini tunafungua uchumi wa wilaya husika.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, katika mpango huu wa kiuchumi; Mpango Mkakati wa Maendeleo ambao tumeletewa leo, ni lazima tuangalie pia maeneo ya vijijini. Sisi tunaotoka vijijini, bado tumesahaulika. Hii miundombinu yote tunayoisema inazungumza mambo mengi ya mjini, lakini sisi ambao wakati mwingine hata mawasiliano ya simu siyo mazuri, hatuzungumzwi humu.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, naomba kupitia Bunge lako, Wizara na Serikali katika Mpango wao huu wahakikishe wanazingatia maeneo ya vijijini.

Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana. Ahsante sana. (Makofi)