Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Mpango wa Tatu wa Maendeleo wa Taifa kwa Kipindi cha Miaka Mitano kuanzia mwaka 2021/2022 – 2025/2026

Hon. Kunti Yusuph Majala

Sex

Female

Party

CHADEMA

Constituent

Special Seats

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Mpango wa Tatu wa Maendeleo wa Taifa kwa Kipindi cha Miaka Mitano kuanzia mwaka 2021/2022 – 2025/2026

MHE. KUNTI Y. MAJALA: Mheshimiwa Naibu Spika, nikushukuru kwa nafasi kwa dakika hizo tano naomba niseme ya kwangu machache ambayo nitaweza kuyasema. Zaidi ya watanzania 75% wamejiajiri kwenye sekta ya kilimo. Lakini sekta hii ya kilimo ambayo ndiyo imeajiri watanzania walio wengi lakini ndiyo inayochangia uchumi wa pato la Taifa hili, lakini ndilo linalosababisha sisi watanzania tuendelee kuishi, Serikali imekuwa haitoi kipaumbele kwenye sekta ya kilimo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, wamesema wenzangu waliotangulia kwenye suala zima la masoko naomba nizungumzie suala zima la upatikanaji wa pembejeo na suala zima la wagani kwenye sekta hii ya kilimo. Mheshimiwa Waziri wa Fedha sasa alikuwa Waziri wa Kilimo kwenye Serikali ya Awamu ya Tano na alivyokuja akiwa Waziri wa Kilimo aliwatangazia watanzania kuhusiana na suala zima la upatikanaji wa pembejeo na hususan kwenye suala la mbolea akasema mbolea itakuwa kama Coca Cola. Sasa Mheshimiwa Waziri Dkt. Mwigulu umerudi huko huko jikoni nikuombe sana suala lile la pembejeo kwenye suala zima la mbolea ile Coca Cola ile tunaitaka safari hii kwenye bajeti hii tuone mbolea inapatikana kwa wakati na yenye tija kwa wakulima wetu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini kwenye suala la pembejeo matrekta power tiller na vitu mbalimbali ambavyo vinakwenda kumsaidia mkulima huyu wa chini vimekuwa vikipatikana kwa shida sana. Hata hiyo mikopo ya matrekta imekuwa ni changamoto pia watu wanazungushwa kwelikweli lakini ili uweze kupata hata hilo trekta unatakiwa kuwa na hati. Wizara ya Ardhi nayo imekuwa ni changamoto hata kuwapatia tu zile ardhi za kimila wakulima wetu ili waweze kupata hati hizo waweze kwenda kukopa hayo matrekta.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini cha kujiuliza Serikali ni moja hivi wanashindwaje kuwaamini hawa watanzania kwamba mtu huyu anajulikana anaishi Kijiji fulani ana ekari kadhaa mwenyekiti wa Kijiji yuko pale anamtambua ni kwanini Serikali imekuwa na kigugumizi kuhusiana na suala zima la utoaji wa mikopo ya pembejeo kwa wakulima wetu wadogo huko vijijini na badala yake tumeendelea kuwaacha wanateseka tuna Benki ya Kilimo ambayo inatakiwa kuwasaidia wakulima wa nchi hii haifanyi chochote hakuna mkulima mdogo hata mmoja anaekopeshwa na Benki ya Kilimo tunaambiwa ni Benki ya Kilimo kwenye makaratasi na majina. Ili tuweze kuleta tija kwenye benki hii niombe benki ya kilimo tuirudishe Wizara ya Kilimo ili iweze kuwahudumia wakulima wetu kule chini na hatimae waweze kunufaika na kodi zao. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nisemee suala na wagani, bado watanzania tunalima kilimo cha kujisukuma tu cha jana cha leo tunakwenda nacho hivyo hivyo. Wagani ndani ya nchi yetu pia kwenye sekta ya kilimo ni changamoto Wizara inayohusika na kuajiri Wizara ya Utumishi tunaombeni mtuambie shida ni nini inayosababisha kushindwa kuajiri wagani wakutosha kwenye sekta ya kilimo.

Mheshimiwa Naibu Spika, suala la wagani ni muhimu sana, tunaona hata watu wamoja moja ambao wanajitutumia wenyewe kwa jitihada zao kuweza kulima kilimo cha kuondokana na umasikini, kilimo cha kutoka kwenye mvua ya Mwenyezi Mungu kwenda kwenye kilimo cha kisasa cha umwagiliaji bado wamekuwa wakikosa huduma hii ya ugani kwasababu tu ya Serikali kushindwa kuajiri wagani kwenye maeneo yetu mbalimbali. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, niliombe pia kama kweli tunahitaji tija kwenye sekta ya kilimo na tuweze kujenga na kuimarisha uchumi wa Taifa letu tuhakikishe kwenye bajeti hii inayokuja kwenye sekta ya kilimo twendeni tukaajiri wagani wa kilimo ili wakulima wetu waweze kupata hiyo huduma muhimu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pia kwenye suala la wagani suala la wagani wako TAMISEMI kwenye kilimo huku hawapo kwa hiyo, pale wanapokwenda kupata changamoto wagani hawa wanashindwa namna ya kuzifikisha mahali husika. Lakini mgani huyu unakuta mgani huyo ni mtendaji wa kata, mgani huyo ni Afisa Mifugo, mgani huyo huyo ndiyo hata yeye anashughulika na masuala ya kilimo kwa hiyo, unamkuta mtu mmoja ana majukumu kadhaa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ningeomba pia kwenye suala zima la wagani wanaohusiana na kilimo tuwarudishe Wizara ya Kilimo ili waende wakasimamiwe na Wizara yao na waweze kufuatiliwa na tuweze kupata tija kwenye suala hilo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nigusie kidogo kwa dakika chache zilizobaki miundombinu tunafahamu vizuri nimalizie tu kidogo dakika moja tunafahamu tuna barabara za kimkakati…

NAIBU SPIKA: Nina orodha ndefu hapa Mheshimiwa.

MHE. KUNTI Y. MAJALA: Mheshimiwa Naibu Spika, dakika moja tu my dear kidogo tu dakika moja ningekuwa nimeshamaliza tuna barabara za kimkakati tangu Bunge la 10 tuliahidiwa barabara ya kutoka Kilindi kupita Chemba tunaenda kuungana na Singida barabara ile mpaka leo bado hatujaweza kuona nini mkakati wake. Niombe Wizara mtakapokuja kuja kuhitimisha tunaombeni tuione barabara ya kutoka Kilindi inayokwenda kupita Jimboni kwangu Chemba…

NAIBU SPIKA: Haya ahsante Mheshimiwa hiyo barabara umeshaitaja, kwa hiyo imeshasikika.

MHE. KUNTI Y. MAJALA: …nakwenda kuunganisha na Mkoa wa Singida nakushukuru sana kwa nafasi. (Makofi)