Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Mpango wa Tatu wa Maendeleo wa Taifa kwa Kipindi cha Miaka Mitano kuanzia mwaka 2021/2022 – 2025/2026

Hon. Zuberi Mohamedi Kuchauka

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Liwale

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Mpango wa Tatu wa Maendeleo wa Taifa kwa Kipindi cha Miaka Mitano kuanzia mwaka 2021/2022 – 2025/2026

MHE. ZUBERI M. KUCHAUKA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi ya kuchangia Mpango huu wa Miaka Mitatu wa Taifa letu. Kwanza, naomba nijielekeze moja kwa moja kwenye upande wa miudnombinu. Ni ukweli usiopingika kwamba nchi yetu imeamua kuingia kwenye nchi ya viwanda. Ili tuweze kulifikia lengo hili la kuwa nchi ya viwanda, matarajio yetu makubwa tunategemea kupata malighafi kutoka mashambani. Vile vile, sera ya nchi yetu sasa hivi tuko kwenye kuunganisha mikoa yetu kwa miundombinu ya barabara za lami. Tumeshamaliza baadhi ya mikoa, lakini bado mikoa mingine haijafikiwa. Ni ukweli vile vile tunahitaji kujenga barabara za kiulinzi, lakini ziko vile vile barabara za kuunganisha za kimkakati.

Mheshimiwa Naibu Spika, tumeshafikiria kwamba ili mazao yetu yaweze kufika kwenye hivyo viwanda tunavyokusudia kuvijenga, ni lazima tuhakikishe kule ambako mazao haya yanazalishwa tumepeleka hizo barabara kuwezesha mazao haya kufika kwenye soko au kwenye viwanda. Kwa mfano, ni ukweli usiopingika zao la korosho kwa Mkoa wa Lindi na Mtwara lina mchango mkubwa sana kwenye pato la Taifa, lakini kwenye Mikoa hiyo hiyo ya Lindi na Mtwara ndiyo mikoa ambayo haifikiki kwa barabara za lami kwenye wilaya zake karibu zote. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kuna mradi mmoja una miaka zaidi ya mitano sasa wa barabara ya kimkakati wa Kanda ya Kusini, barabara inayotoka Mtwara – Newala – Tandahimba – Masasi - Nachingwea mpaka Liwale. Huu wote unaozungumziwa ni ukanda wa korosho, ndiyo maana mwaka huu tumepata shida sana watu wa korosho kwa sababu mpaka imefika masika korosho bado hazijatoka kwa wakulima kwa sababu hakuna barabara ya kuzifikisha maghalani. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, napendekeza kwamba kama kweli Serikali inadhamiria kufufua viwanda au kwenda kwenye uchumi wa viwanda lazima tuhakikishe tunayo miundombinu rafiki ya ufufuaji wa viwanda, lakini kama barabara zetu zitabaki kuwa hivi zilivyo, tukategemea kwamba mazao ya wakulima yatafika kwenye masoko au yatafika kwenye viwanda, hapa tutakuwa tunachezeana kiakili. Naomba sana, ufufuaji wa viwanda lazima uende sambamba na ujenzi wa miundombinu. Kweli Taifa letu liko kwenye hatua ya kuunganisha mikoa lakini bado naomba tuingie sasa kwenye barabara zinazounganisha wilaya zetu, hata basi barabara zinazounganisha wilaya zetu na mikoa yetu ili tuone tija ya wakulima. Wakulima wengi wanateseka hawapati pembejeo kwa wakati, hawapati infrastructure yoyote, lakini hata pale wanapojitahidi kulima, mazao yao yanaharibikia mashambani, wanashindwa kuyafikisha kwenye masoko. Jambo hili ni lazima Mheshimiwa Mwigulu alipeleke pamoja kuungamanisha miundombinu na viwanda.

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo lingine naomba nizungumzie huko huko kwenye miundombinu. Fedha nyingi za Serikali tunazipeleka kwenye halmashauri, tunakwenda kujenga hospitali kwenye wilaya zetu na vituo vya afya, tunajenga madarasa na mabweni shuleni, lakini hizi fedha tunazipeleka kwenye halmashauri ambako hakuna wataalam. Tulipounda TARURA tuliondoa wahandisi wote tukawapeleka TARURA, leo kwenye halmashauri zetu hazina wahandisi, hakuna wakadiriaji majengo. Tunapeleka bilioni 1.5 kwa ajili ya kujenga hospitali ya wilaya, kule unakopeleka yuko Mkurugenzi na watendaji wengine, hakuna mhandisi, nini kinatokea?

Mheshimiwa Naibu Spika, kinachotokea ni kwamba, mahali ambapo mkadiriaji wa majengo akikadiria jengo ili kuezeka bati hamsini anaandika bati 200, zinaenda kununuliwa bati 200 zinakuwa pale jengo limeisha, bati zimebaki, fedha zimeisha. Au jengo lingine ambalo lilitakiwa kuezekwa kwa bati 50 ananunua bati 25, fedha zimeisha, jengo halijaezekwa. Huwezi kumchukulia hatua, hana taaluma hiyo, yuko pale, anafanyaje? Mkurugenzi yuko pale, Mhasibu yuko pale lakini hakuna Mkadiriaji Majengo. Unamchukulia hatua gani huyu mtu ambaye hujamuajiri kwa kwa kazi hiyo? Pangekuwa na Mhandisi pale angeweza kuwajibika, lakini hatuna Wahandisi.

Mheshimiwa Naibu Spika, nikiondoka hapo, tunayo kada ya wakandarasi. Kwa sababu tumeshaamini kwamba ujenzi kwa force account ni rahisi zaidi kuliko wakandarasi, sasa tumeua hii kada ya ufundi. Naomba jambo hili basi liende sambamba na mitaala yetu ya elimu, wanaendelea kuzalisha wataalam kule wa ujenzi, wakati huku hawawahitaji kuna faida gani? Wakandarasi peke yao ambao wanabaki kidogo ambao tunasema tunataka kulea wakandarasi wazawa, waliobaki ni walioko kwenye barabara tu na ni wachache sana, tena hawana hata mitaji na wala hawafikirii kupata mitaji, lakini wale wakandarasi wa majengo hawana kazi tena nchi hii. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba Wizara ya Elimu waondoe hiyo taaluma kwenye vyuo vyetu, hawana kazi! Sisi tumeshaamua kwamba Mwalimu Mkuu ndiyo atasimamia jengo letu, tumeshaamini Mkurugenzi ndiyo atasimamia jengo, tunaamini kwamba DMO ndiyo atasimamia jengo letu, hawa wengine hatuwahitaji! Ndiyo maana tangu tumeunda taaluma mpaka leo hii kwenye halmashauri nyingi hatuna Wahandisi, uongo au ukweli? Naomba sana tulifikirie hilo kwamba tunapeleka fedha nyingi halmashauri, lakini hazina wasimamizi na tutawahukumu kweli lakini tunawahukumu isivyo halali. (Kicheko)

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba pia nizungumzie suala la uwekezaji. Namshukuru sana Mheshimiwa Rais, amelizungumza suala hili la uwekezaji vizuri sana, lakini naomba nitoe tahadhari kwa nyie mliopata mamlaka. Hiki kitu cha uwekezaji kiko very delicate. Nimemsikia Mheshimiwa Rais amesema tusiwabughudhi wawekezaji na naunga mkono, tupunguze urasimu kwa wawekezaji lakini tuwe makini. Haiwezekani kazi ambazo Watanzania wanahangaika nazo kila siku wakizitafuta waende wakagawie wawekezaji eti tu kwa sababu tukimkatalia kuajiri ataondoka. Tuwe makini sana hapo. Tusipoangalia ni mwanya mwingine wa kupoteza ajira nchini.

Mheshimiwa Naibu Spika, bahati nzuri mimi nimedumu kwenye Sekta Binafsi zaidi ya miaka 30, najua kinachoendelea kule. Wapo watu wana vyeti vya expert, wana vibali vya ma- expert lakini ni wasimamizi tu wa kupakia mizigo kwenye malori. Wapo watu wana kada ya expert kazi yao ni madereva tu wa kuendesha viberenge mle ndani, kupaki paki mizigo kwenye godown, lakini ukiangalia cheti chake, huyo ni expert. Muda wa miaka miwili ukiisha, anaombewa tena kibali. Tuwe makini kwenye nafasi hiyo, tunahitaji wawekezaji, tunawahitaji sana na wafungue milango na wawe rafiki wa wawekezaji, lakini kwa umakini mkubwa sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, hayo ndiyo niliomba niyachangie kwa leo. Naomba kabla hujanipigia kengele, hayo hayo mawili, matatu yatoshe kwa leo. (Kicheko/Makofi)