Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Mpango wa Tatu wa Maendeleo wa Taifa kwa Kipindi cha Miaka Mitano kuanzia mwaka 2021/2022 – 2025/2026

Hon. Tabasamu Hamisi Hussein Mwagao

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Sengerema

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Mpango wa Tatu wa Maendeleo wa Taifa kwa Kipindi cha Miaka Mitano kuanzia mwaka 2021/2022 – 2025/2026

MHE. TABASAM H. MWAGAO: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru. Kwa niaba ya wananchi wa Jimbo la Sengerema naomba nichangie Mpango wa Maendeleo uliowasilishwa kwetu leo na Mheshimiwa Mwingulu Nchemba, Waziri wa Fedha.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika Mpango wake aliowasilisha leo sijaona mahali ambapo amezungumzia habari ya zao la pamba. Zao la pamba katika nchi hii linalimwa zaidi ya mikoa 14 na pamba hiyo unayoiona ina uwezo wa kuwa na viwanda vitano. Angalia uchumi mkubwa unaotokana na pamba; pamba ikizalishwa vizuri na ikatafutiwa bei, Serikali ikawekeza katika pamba; na Serikali ilivyojitoa katika kuwekeza katika pamba, wakaachiwa mabepari, zao hili litakuwa limekufa. Kwa nini? Limekufa kwa kupata bei ndogo. Mabepari wameshusha bei. Tusiite wawekezaji, kwa sababu kwenye pamba kule kuna mabepari, zao la pamba likawa limekufa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa tunaiambia Serikali, katika Mpango wake wa miaka mitano, wanafanyaje kulifufua zao la pamba? Serikali ikiwekeza katika zao hili, tutapata viwanda vya pamba, viwanda vya nyuzi, viwanda vya nguo, viwanda vya vyakula vya kuku na mifugo na tutapata mafuta. Haya mafuta ambayo leo mnayaagiza kutoka Malaysia na kwingineko, mnalazimisha mafuta, mafuta, yako kwenye pamba. Huko kote, hizi ni kodi utapata Mheshimiwa Mwigulu Nchemba. Bahati nzuri wewe unatoka kwenye Jimbo ambalo pamba inalimwa. Hebu waonee huruma wananchi wa Iramba, Sengerema wakiwemo na wananchi wengine Tanzania nzima. Njoo na mpango wa pamba. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, katika pamba ninachotaka kueleza, Mheshimiwa Mwigulu Nchemba utapata kodi, leta sheria tu hapa. Badala ya pamba kutozwa ushuru, njooni na Sheria hapa mchukue hata VAT asilimia kumi na pamba muipe bei ya shilingi 2,000/=. Ekari moja ya pamba ina uwezo wa kutoa tani moja ya pamba. Sasa kama kuna mtu anapata shilingi milioni mbili katika pamba na Serikali ikachukua kodi ya asilimia 10, mkachukua shilingi 200,000/= kwa ekari moja, mikoa inayolima 14: Je, utakuwa na shida gani tena ya pesa hapa Mheshimiwa Mwigulu? Hii miradi yako yote itaisha. Treni ya mwendokasi, sijui kuna Bwawa la Nyerere na la wapi, sisi walimaji wa pamba tu tunatosha kutengeneza kodi ya kufanya kazi hii.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika hili, kuna suala la Ziwa Victoria, kule ukianzia juu; Tarime kule, ukaenda moja kwa moja mpaka kule Misheni mwisho kabisa, Kanyigo, kuna wananchi wanaokaa mwambao wa Ziwa, hawajatumikishwa katika kilimo cha irrigation. Sisi tukimwagilia, sasa hivi umeme upo, tukopesheni mashine za kumwagilia, wananchi wetu wana uwezo wa kuzalisha kiwango kikubwa cha mazao. Mnataka uchumi gani kama huu uchumi tunauachia wazi?

Mheshimiwa Naibu Spika, leo kwa mfano, kwenye Jimbo langu tu la Sengerema pale, kuna mradi wa maji wa shilingi bilioni 23, unadaiwa deni la umeme la shilingi milioni 300. Umeme unakatwa, mradi wa shilingi bilioni 23 unateswa na shilingi milioni 300. Sasa tunashangaa, hawa ndio wawekezaji? Ndio Watanzania wanaotaka uchumi wa bluu? Unaandaa mradi wa shilingi bilioni 23 na una deni la shilingi milioni 300, halafu ule mradi unakaa haufanyi kazi, unadaiwa shilingi milioni 300! Ni maajabu makubwa sana katika nchi hii. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Waziri wa Fedha aliangalie sana hili suala katika miradi kama hii. Huu ni mradi mmoja tu wa Sengerema, sijui miradi mingine inayoteswa na vijipesa vidogo kama hivi kwa uwekezaji mkubwa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kuna suala la uvuvi. Kule katika uvuvi tuna matatizo makubwa. Sheria za Uvuvi zilizoko kule katika Ziwa Victoria na hatujui Maziwa mengine huko; leo kuna samaki ambao ni wadogo hawakui. Kuna furu, kuna vimote na samaki wa aina nyingi; barara, hizi ni lugha za kienyeji kule. Wao wanajua hawa samaki hawakui, lakini wanakamatwa nao wale Samaki, nyavu zinachomwa moto. Mlikuwa na Kiwanda cha Nyavu, fufueni kiwanda hicho halafu mtengeneze nyavu zinazotakiwa na Serikali, lakini mkiwaacha waagizaji wakaleta nyavu, matokeo yake mnakwenda kuzichoma moto, mnatengeneza umasikini katika Ziwa Victoria. Liangalieni sana hili jambo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, hivi tunavyozungumza tunakwenda kufunga mradi. Mgodi wa Buzwagi unafungwa. Sengerema kuna wawekezaji katika Mgodi wa Nyanzaga wameomba kufungua Mgodi wa Nyanzaga; leo ni mwaka wa nne toka mwaka 2017, mnataka wawekezaji gani? Huu mradi unakuja kuzalisha pesa. Uwekezaji wake tu wa kuandaa ule mgodi una shilingi trilioni moja, leo mnataka wawekezaji gani? Kwa sababu tu ule mradi unatakiwa kukua Sengerema watu hawautaki, halafu wanataka kuita wawekezaji. Waje wawekezaji gani wakati wengine mnawakataa? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Waziri wa Fedha aangalie katika Mpango wake wa miaka mitano, tunahitaji Mgodi wa Nyanzaga Sengerema ufunguliwe. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lingine kuna suala kubwa sana hapa tunalozungumzia la utengenezaji wa barabara. Hizi barabara unazoziona zinakwenda kwa wananchi, ambazo zinatengenezwa na TARURA, nilifikiria sana kwa nini TARURA isirudi ujenzi? Hata hivyo, naangalia kazi waliyonayo watu wa ujenzi; ukiangalia miradi aliyonayo TANROAD na bado ukamwongezee tena mradi mwingine wa TARURA, sishauri TARURA ihame. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nakuomba sana Mheshimiwa TARURA ibakie mahali pake, lakini kuna pesa ziko hapa. Nilizungumza hapa siku moja nikawaambieni, jamani kuna pesa za TARURA, kuna pesa ziko kwenye ukokotoaji wa mafuta, wanakokotoa watu wa EWURA. Shilingi 90/= kila siku ya Mungu wanakusanya katika huu ukokotoaji, hizi fedha zinakwenda kutumika vibaya. Shilingi 1,080,000,000/=. Ukichukua pesa hizi Mheshimiwa Mwigulu, kwa mwezi ni shilingi 32,400,000,000/=; kwa mwaka kunakuwa na fedha hapa zaidi ya shilingi bilioni karibu 400 ambazo zinakwenda kwenye hizi tozo ndogo ndogo.

Mheshimiwa Naibu Spika, hawa walioweka tozo, wote wako kwenye bajeti. Mnakwendaje kuweka kwenye tozo la mafuta? Kule kuna import duty, kuna import levy pale, kuna petrol levy pale; mnakwenda kuweka hivi vitu vingine vya nini? Hii fedha ileteni TARURA tutengeneze barabara zetu. Tunazo Halmashauri za Miji. Halmashauri za Miji tunazo 21, Halmashauri za Wilaya tunazo 137, tunazo Manispaa 20 na Majiji sita, kwa nini TARURA haongezewi fedha hapa za kufanyia kazi? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, hata kwa Mheshimiwa Mwigulu juzi nimepita barabara ya Ndago, nimepita Shelui kuzungukia Ndago, hata yeye hana barabara. Nitashangaa sana kama Mheshimiwa Mwigulu hata wewe hutakubali TARURA iongezewe fedha. Hutarudi 2025. Haya maneno nakwambia kabisa, usidhani hatutarudi sisi tu, hata ninyi Mawaziri mtakomea ndani huko huko. Tengenezeni pale TARURA, ipeni pesa za kutosha tutengeneze barabara zetu. (Kicheko/Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, hata wewe hapo hutarudi kama barabara hizi hazitatengenezwa. Msidhani kwamba hili ni suala ni la Tabasam pekee.

Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. Nafikiri message imekwenda. (Makofi/Kicheko)

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Tabasam huu utabiri wako huu! (Kicheko/Makofi)

MHE. TABASAM H. MWAGAO: Ndiyo. Hili ni hatari! (Makofi/Kicheko)

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Tabasam.

MHE. TABASAM H. MWAGAO: Mheshimiwa Naibu Spika, angalia dakika zangu lakini.

NAIBU SPIKA: Subiri kwanza Mheshimiwa Tabasam, subiri kidogo.

MHE. TABASAM H. MWAGAO: Ndiyo.

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Mwigulu humu ndani ni Senator na mimi nataka kwanza kumkaribia kidogo, lakini sasa wewe ni mgeni kabisa, ukitutabiria sisi kutokurudi humu ndani, nahisi hali yako wewe ni mbaya zaidi kuliko ya kwetu. (Kicheko/Makofi)

Endelea Mheshimiwa, karibu.

MHE. TABASAM H. MWAGAO: Mheshimiwa Naibu Spika, ninachotaka kukwambia, TARURA ni janga la Kitaifa. TARURA, yaani kama ingekuwa nchi nyingine tungekuwa tuna mjadala wa Kitaifa tufanyeje kuhusu TARURA?

Mheshimiwa Naibu Spika, ninachotaka kuwaambieni jamani, Waheshimiwa Wabunge humu ndani, nimewaelezeni kwamba fedha ziko kwenye mafuta. Nikawaambia kwamba, nilimwambia hapa Mheshimiwa Spika, tukae tujadili hili jambo, kuna fedha kule sisi tuwaonyeshe. Hii Habari ya kuwa tu bei za mafuta zinapanda kila mwezi, bado hatuna manufaa nazo hizi fedha, kodi yetu iko pale pale, hili ni jambo ambalo kwenda kwenye uwekezaji, kama Serikali haiwezi kuagiza mafuta yake, ninachotaka kukuambia Mheshimiwa Mwigulu, utatwanga maji kwenye kinu. Haitawezekana nchi yoyote inayotaka uchumi wake isipoweka fedha kwenye kuagiza mafuta yake. Tegemeeni wafanyabiashara waje wawatengenezee nchi, hili jambo halipo hata siku moja. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tunazo nchi marafiki nyingi, hili suala la mafuta; tunalo eneo letu la TIPER pale. Lile eneo amepewa mwekezaji ambapo hakuna hata faida yoyote. Tungeenda kutengeneza matenki tukawa na reserve kubwa pale ya lita hata bilioni mbili. Leo mafuta yanakuja kupanda bei katika Soko la Dunia, sisi tunaweza tuka-stabilize pale tukabakia salama. Endeleeni kuudharau huu ushauri ninaowapeni, kwa sababu unatolewa na mtu wa Darasa la Saba katika nchi hii.

Mheshimiwa Naibu Spika, ahsanteni sana. Mimi nimewasilisha. (Makofi/Kicheko)