Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Mpango wa Tatu wa Maendeleo wa Taifa kwa Kipindi cha Miaka Mitano kuanzia mwaka 2021/2022 – 2025/2026

Hon. Oran Manase Njeza

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mbeya Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Mpango wa Tatu wa Maendeleo wa Taifa kwa Kipindi cha Miaka Mitano kuanzia mwaka 2021/2022 – 2025/2026

MHE. ORAN M. NJEZA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa fursa hii na mimi ya kuchangia Mpango wetu wa Tatu wa Taifa.

Mheshimiwa Spika, naomba kwanza nianze kwa kuipongeza Serikali. Kama ulivyosema mwenyewe, huu mpango unatupa fursa ya tathmini lakini vile vile inakuangalia tunaenda vipi mbele ya safari yetu.

Mheshimiwa Spika, ukiangalia tathmini ya tulikotoka tumefanya vizuri kiuchumi, kutoka uchumi wa chini kwenda uchumi wa chini kati nafikiri ni hatua nzuri sana. Lakini ukiangalia vile vile kwenye miundombinu tumefanya vizuri na maeneo mengi tumefanya vizuri sana. Kwa hiyo napenda sana kumshukuru na kumpongeza Mheshimwa Rais, Serikali yake nzima, Mheshimiwa Waziri wa Mipango kwa kutuletea hii taarifa nzuri sana ambayo kwakweli ukiangalia inatupa matumaini makubwa sisi kama Taifa, na ukiangalia dhima nzima ya huu mpango ni kujenga uchumi shindani, lakini vile vile inaenda pamoja na viwanda na maendeleo ya watu.

Mheshimiwa Spika, kwakweli uzito wa hiyo dhima ni mkubwa mno. Lakini nilikuwa najaribu kuangalia, sisi kama Taifa pamoja na hii dhima, je, tunasimama wapi?

Mheshimiwa Spika, hii dhima nguzo kubwa ziko kwenye uimara wa uchumi; uchumi wetu je, ni imara au si imara? Kama tathmini tuliyoifanya tumetoka uchumi wa chini sasa hivi tupo kwenye uchumi wa kati ina maana uchumi wetu ni imara. Vile vile nguzo yake ingine ni miundombinu, je, tuna misingi mizuri ya miundombinu? Ndiyo, tumeanza vizuri tumejijenga vizuri katika miundombinu na tunakwenda vizuri, nakadharika, nakadhalika.

Mheshimiwa Spika, ukianza na hii hatua ya kwanza tu ya uchumi. Nina imani ya kwamba kuna maboresho machache sana ambayo tunaweza kuyafanya katika nchi yetu. Tunategemea sana kilimo, kilimo ndiyo nguzo ndicho kinachoajiri asilimia kubwa ya Watanzania. Watu wengi tunafikiri masoko hayapo, masoko yapo, na masoko ya Tanzania ya mazao yetu naweza kusema kwa kiasi fulani ni ya upendeleo.

Mheshimiwa Spika, ukiangalia zao la kahawa, hasa arabica, kwenye Soko la Dunia la New York bei yetu ya kahawa inaongezewa senti thelathini mpaka hamsini kutegemea na bei shindani ya New York hiyo ina maana kuwa wakulima wetu wangepata bei nzuri sana ya Kahawa kutokana na upendeleo tulionao kwenye Soko la Dunia.hata hivyo hali siyo hivyo, kuna matatizo tuliyonayo ambayo usimamizi wa masoko haya ambayo yapo inaelekea kuna mahali hatufanyi vizuri.

Mheshimiwa Spika, tunapozungumzia huu mpango wa tatu tungeangalia hizi fursa zilizopo, tufanye namna gani haya masoko yaliyopo yaende vizuri. Kama tumeongezewa bei ya arabica kwa senti thelathini mpaka arobaini kwa kila lb, lb 2.2 ndio sawa na kilo moja, kama tumeongezewa hizo kwanini hatufanyi vizuri?

Mheshmiwa Spika, kwenye mahindi Mwenyezi Mungu ametupa ardhi nzuri, lakini nayo uzalishaji wetu si wa ushindani kwasababu uzalishaji wa Tanzania kwa mahindi ukilinganisha na majirani zetu kwakweli hatufanyi vizuri.

Mheshimiwa Spika, soko la nje la majirani zetu, ukiangalia nchi zinazotuzunguka, hasa Zambia wanaweza kuuza kwa faida mahindi yao kwa kilo kwa shilingi 300, lakini kwa sisi tunaozalisha Tanzania ukiuza kwa shilingi 500 kwa kilo ni hasara; ni kwanini? Kwasababu bei ya mbolea kwa hapa kwetu si Rafiki, na hiyo inasababisha kwa kiasi kikubwa na utendaji ambao sio mzuri katika miundombinu.

Mheshimiwa Spika, usafirishaji unachukua kiasi kikubwa sana cha bei ya pembejeo. Kwa hiyo tukiweze kuboresha miundombinu, tukaboresha vile vile na wenzetu wa Barandari ambao walikuwa wanaendelea na maboresho nafikiri kwa kiasi kwa kiasi kikubwa tunaweza kuwa na ushindani. Huwezi wenzetu wa Zambia wakauza Mahindi yao kwa faida kwa shilingi 300 na sisi tukauza bila faida kwa shilingi 500, hiyo haileti ile dhama nzima ya Uchumi wa ushindani. Ina maana sisi hatutakuwa washindani kwa hiyo hata ukitafuta soko, soko ambalo utauza kwa bei ambayo ni ya hasara hilo soko litakuwa baya. Kwa hiyo tuanze kwanza na kuboresha kilimo cha tija.(Makofi)

Mheshimiwa Spika, kuhusu suala la Miundombinu, mwenzangu amezungumzia kuhusu TAZARA. sasa ni kwanini ukiangalia TAZARA kwenye mpango haizungumziwi kama mradi ambao ni quick win? Reli ya TARAZA ipo pale na ni Standard Gauge lakini bidhaa nyingi zinazokwenda nje ya nchi asilimia zaidi ya 70 zinatumia barabara yetu ya TANZAM na hawatumii TAZARA. Mimi mwenyewe nimejaribu kuulizia usafirishaji kwa kupitia TAZARA ni takriban mara mbili ya usafirishaji kwa gari. Sasa unashangaa, tungetegemea reli iwe rahisi kuliko barabara; hasa ni kwa nini usafirishaji kwa reli hapa kwetu umekuwa ni tatizo na bei ya juu? Ina maana hapa tunatatizo kubwa.

Mheshimiwa Spika, tunaomba, ninaomba sana tuangalie tunapoboresha SGR tuangalie ni namna gani tunaweze kuiunganisha SGR na mtandao wa Reli za kwetu za Afrika Mashariki pamoja na nchi za SADC, ikowemo kuunganisha TAZARA pamoja na SGR. Kama alivyosema mtangulizi wangu, kuna kumuhimu wa kuunganisha Reli ya TAZARA na Port ya Kasanga kutokea Tunduma, lakini vile vile kuanzia Mbeya kwenda Ziwa Nyasa, ili uwe na muunganiko mzuri sasa na wa Reli ya Mtwara mpaka Mbamba Bay, na hapo sasa kutakuwa na mzunguko mzuri wa reli yetu.

Mheshimiwa Spika, kuhusu suala la uzalishaji wa viwanda na fursa za pesa za kigeni. Tuna Madini mengi hapa nchini wawekezaji wapo, lakini ukiritimba tulionao wakati mwingine unasababisha wawekezaji wanakosa imani na kuwekeza hapa kwetu. Nimezungumzia mara nyingi kuhusu madini ya Niobium. Madini ya niobium ni madini ambayo ni adimu. Kiwanda ambacho kinategemewa kuwekeze hapa nchini kwetu kitakuwa ni cha nne duniani, na hiki kiwanda kitatumia rasilimali zetu na madini yaliyoko Tanzania na kitatuletea mapato kwa kila mwaka zaidi ya Dola 200 na Serikali itapata Dola zaidi ya milioni 20 kwa kila mwaka.

Mheshimiwa Spika, Ukiangalia direct investment ni zaidi ya Dola milioni 200 vile vile. Sasa, ni ka nini tusichukue fursa kama hizo kama hao watu wapo tayari nao kwenda pamoja na sheria tulizonazo nchini kwetu?

Mheshimiwa Spika, nafikiri tukiweza kuyaboresha haya na yakawepo kwenye mpango wetu, tukawa na mazingira ambayo ni rafiki tukapunguza gharama, hayo tutakwenda vizuri sana. Lakini kwenye miundombinu, hata ukiangalia TARURA sasa hivi barabara ziko hoi. Kwenye Wilaya ya Mbeya Jimbo la Mbeya Vijijini barabara zetu takriban kilometa 1000 zote zina hali mbaya. Lakini unaangalia, wakati mwingine ni utendaji wa watendaji wetu. Kwenye Bajeti ya mwaka huu tu bado miezi miwili ametumia asilimia 20, wananchi hawaweze kusafirisha mazao yao.

Mheshimiwa Spika, sasa tusipoboresha hata kilichopo nina imani kuwa hatuweze kufanya vizuri. Hivyo ninaiomba Serikali kupitia TARURA iboreshe Miundombinu ya barabara zetu, lakini barabara zetu ambazo zina fursa za kwenda mipakani kama kutuunganisha sisi na Zambia, sisi na Malawi nazo zipewe kipaumbele.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo ningeomba Barabara kama hii ya Mbalizi kwenda Shigamba ambayo inakwenda mpaka Isongole karibu na mpaka na Malawi iwe kwenye kipaumbele cha mpango wetu.

Mheshimiwa Spika, nashukuru sana niendelee tena kumpongeza Mheshimiwa Waziri, na ninaunga mkono hoja, ahsante sana. (Makofi)