Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Azimio la Bunge la Kutambua na Kuenzi Mchango wa Rais wa Tano wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. John Pombe Joseph Magufuli, kwa Utumishi wake Uliotukuka Pamoja na Azimio la Bunge la Kumpongeza Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan kuwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania

Hon. Dr. Mwigulu Lameck Nchemba Madelu

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Iramba Magharibi

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Azimio la Bunge la Kutambua na Kuenzi Mchango wa Rais wa Tano wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. John Pombe Joseph Magufuli, kwa Utumishi wake Uliotukuka Pamoja na Azimio la Bunge la Kumpongeza Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan kuwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania

WAZIRI WA KATIBA NA SHERIA: Mheshimiwa Naibu Spika, nikushukuru kwa kunipa fursa hii na mimi kuweza kuchangia mjadala huu. La kwanza, nitoe pole kwa Watanzania wote kwa msiba huu uliotupata; na nikiri kwamba naunga mkono hoja iliyotolewa na watoa hoja, na kwa kweli wamefafanua kwa kirefu na kwa kina na wameutendea haki mjadala wenyewe huu tunaoujadili, ambao utakaa kwenye kumbukumbu zetu rasmi za Bunge. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nikianzia hapo hapo; katika jambo hili lililotokea nitumie fursa hii kuwashukuru Watanzania. Watanzania wametendea haki uhuru wa nchi yetu, wameipa heshima nchi yetu kwa namna walivyomsindikiza kiongozi wetu, kwa namna walivyomuaga kiongozi wetu. Ni kiongozi aliyesimamia waziwazi uhuru wa nchi yetu, ni kiongozi aliyesimamia waziwazi maslahi ya Watanzania, ni kiongozi aliyesimamia waziwazi na aliyeyatoa maisha yake kwa ajili ya Watanzania. Heshima aliyopewa wakati wanamuaga katika maeneo alikopelekwa; mimi niliendelea kupata hata message maeneo mengine wakisema tunatamani na majiji mengine apite, tunatamani na huku apite; ni basi tu kwa ratiba ilivyokuwa tukafanya kwa uwakilishi. Ile ilikuwa heshima inayolinda na inayotambulisha uhuru wa Taifa letu.

Mheshimiwa Naibu Spika, na wakati anachaguliwa Mheshimiwa Rais wetu pamoja na Makamu wake, watanzania walipiga kura kwa siri. Zile zilikuwa kura za siri na asilimia ilizopatikana ile ilipatikana kwa kura za siri. Lakini namna walivomsindikiza wameitangazia dunia kwamba kwa kura ya wazi walikuwa wanamaanisha nini wakati wanapiga kura wakati wa Uchaguzi Mkuu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nitoe tu neno la faraja kwa Watanzania, kwamba hili limeshatokea. Niwape neno la Faraja; wakati tunaingia kwenye uchaguzi mwaka 2015, Ilani ya Uchaguzi ambayo imetupa matokeo makubwa haya, ambayo ndiyo ilikuwa ahadi kwa Watanzania wabeba maono, kwenye Ilani alikuwa Dkt. Magufuli na Mama Samia Suluhu. Kwahiyo hakuna namna mafanikio yale tuliyoyapata kutoka 2015 - 2020 ukayaongelea bila kumtaja Mama Samia Suluhu. Ameshiriki kikamilifu na yeye ni sehemu ya mafanikio yale. Na katika mafanikio yale wakiwa wao wabeba maono msimamizi wa maono yale, msimamizi wa kazi alikuwa Waziri Mkuu ambaye yupo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwahiyo mmoja wa mbeba maono yupo, msimamizi wa mbeba maono yupo lakini wakati mbeba maono na msimamizi wa wapo, pia mbeba kikapu yule aliyekuwa anawezesha yale maono yatekelezwe Dkt. Mpango naye yupo. Kwa maana hiyo hatuna haja ya kuwa na hofu kwa sababu seti hiyo bado imekamilika, ambayo imetupa mafanikio makubwa haya ambayo tumeweza kuyasimulia leo hii. Tunachotakiwa ni kuendelea kwa wale ambao ni mihimili, Bunge na Mahakama kutoa ushirikiano. Kwetu sisi ambao ni wasaidizi wa Serikalini tumepokea maelekeo na tunasimama kuendelea kupokea maelekezo kama ambavyo tumekuwa tukifanya na kuyasimamia ili tuweze kufanikiwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, na hata katika utekelezaji, kinachomfanya kiongozi aweze kusimama na kutekeleza wala si jinsia yake, kinachomfanya kiongozi akemee rushwa wala si jinsia yake, ni uadilifu wake; hata mwanaume akiwa mla rushwa hawezi kukemea rushwa; ni uadilifu wake. Sasa fuatilieni historia ya Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan Rais wetu wa sasa hivi, hana record yoyote ya kukosa uadilifu, ni muadilifu ambaye anaweza kwa namna yoyote bila uoga kukemea rushwa mahali popote pale.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini pia ukiangalia ni mchapa kazi ambaye hapendi kazi ilale. Sisi ambao tumekuwa tukipokea maelekezo tangu muda wote ule tuna uhakika na haya tunayowaelezea. Hata juzi aliposema pale kwetu sisi tayari tumeshapokea yale ni maelekezo. Amesema atasimama imara kwenye mapato na matumizi na masuala ya rushwa. Sisi wasaidizi wake tayari tumeshapigia mstari, na mimi nilishawaelekeza wasaidizi wangu kuendelea kutafasiri yale waendelee kuyafatilia ili yale ambayo yataenda kinyume na maelekezo yake yaweze kuchukuliwa hatua. Maana yake hapo tayari ni zero tolerance of corruption no nonsense on public offices and public funds pamoja na kusimamia haki za watu.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini pia kwa mwanamke katika jamii yoyote, mwanamke ni baraka, mwanamke ni kibali. Tanzania inaenda kupata kibali. Na hata ukienda tu kwenye mifano hata ya kawaida, kwasababu nimeshaona kengele imegongwa, hata kwenye mifano ya Maisha ya kawaida tu, yaani hata simba tu tangia wapate CO mwanamke mambo yao yamewanyookea kweli kweli siku hizi hawang’oi hata viti. Maana yake wanabaraka katika nafasi yao na wanafanya vizuri. (Makofi/Kicheko)

Mheshimiwa Naibu Spika, niliona niweke na hili kwa sababu tunaomboleza, watu wasitoke bado wananyong’onyea nyong’onyea ili tuendelee kuwatia moyo wananchi wetu na Taifa letu liweze kusonga mbele. Naunga mkono hoja na watoa hoja wameielezea vizuri sana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana.