Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Azimio la Bunge la Kutambua na Kuenzi Mchango wa Rais wa Tano wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. John Pombe Joseph Magufuli, kwa Utumishi wake Uliotukuka Pamoja na Azimio la Bunge la Kumpongeza Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan kuwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania

Hon. Nicodemas Henry Maganga

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mbogwe

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Azimio la Bunge la Kutambua na Kuenzi Mchango wa Rais wa Tano wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. John Pombe Joseph Magufuli, kwa Utumishi wake Uliotukuka Pamoja na Azimio la Bunge la Kumpongeza Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan kuwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania

MHE. NICODEMAS H. MAGANGA: Mheshimiwa Naibu Spika, asante sana. Awali ya yote naomba nimshukuru Mwenyezi Mungu kuweza tena kupata nafasi hii ya kuweza kuongea yale aliyokuwa akiyafanya marehemu, baba yetu John Pombe Joseph Magufuli.

Mheshimiwa Naibu Spika, ninamshukuru Mungu, ninamshukuru Mwenyekiti wangu wa Chama Cha Mapinduzi, Mungu amuweke mahali pema peponi. Kweli haikuwa rahisi kwanza mimi binafsi kuweza kufika kwenye Bunge hili tukufu maana ilikuwa kazi ngumu sana, lakini kwa uwezo wa Mungu na uwezo wake kwa juhudi zake Mheshimiwa nikaweza kufika hapa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba niwakumbushe tu Waheshimiwa Wabunge; tarehe 27 mwezi wa pili wakati akitoka Chato Mheshimiwa Rais alipita Jimboni kwangu Mbogwe, aliacha ahadi sitazisahau daima kwenye maisha yangu.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba niwakumbushe tu Waheshimiwa Wabunge tarehe 27 mwezi wa Pili wakati akitoka Chato Mheshimiwa Rais alipita Jimboni kwangu Mbogwe, aliacha ahadi sitazisahau daima kwenye maisha yangu. Jimbo la Mbogwe ni Jimbo moja katika majimbo ya Kanda ya Ziwa lilikuwa limesahaulika sana katika awamu zilizopita zote zile nne, hatukuwa na lami, hatukuwa na taa barabarani, lakini Mheshimiwa alipita akatoa ahadi mbele za wananchi na mimi nilipata fursa ya kuongea na wananchi zaidi ya elfu tatu nikimwambia ukweli jinsi ulivyo katika Jimbo na matatizo ya Jimbo.

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya wiki moja tukamwona mama yetu anatangaza kifo cha Rais wetu, kweli tulipokea kwa masikitiko makubwa. Kwa kawaida sisi asili yetu Wasukuma huwa sio wepesi wa kuamini jambo, hatukuamini yale matangazo ya kwanza na kwa kuwa kama mnavyofahamu Waheshimiwa Wabunge tuko tofauti tofauti katika Imani, wale wenzetu ambao hawajamwamini Mungu walikataa kabisa, Wasukuma wale wa Kanda ya Ziwa kwamba haiwezekani huyu bwana afe, maana ilikuwa haijawahi kutokea siku moja ameonekana akiwa na malaria au akionekana akitibiwa popote pale.

Mheshimiwa Naibu Spika, kama mlivyokuwa mnaona Waheshimiwa Wabunge mitandao ilivyokuwa iki-tweet, kuna mtu anaitwa Kigogo, walikuwa wakisoma sana wananchi wangu hasa wa Kanda ya Ziwa wakihakikisha kwamba huyu jamaa wanamsingizia, ila kwa leo naomba niwape tu neno moja Yohana 14:1 ambalo inatutia moyo sote Watanzania bila kujali itikadi zetu na niwaombe tu baba zangu na mababu zangu wale ambao bado hawajamwamini Mungu tukubaliane tu kwamba hii hali imeshatupata na imeshatokea hakuna haja ya kufikiria wala kudhania kwamba labda tutazama. Tanzania naifananisha kama safari ya wana Israel wakati Musa akiwa anawatoa kwenye nchi ile ya shida, aliinuliwa mtu mmoja Yoshua na niseme tu kwa sasa hivi dhahiri kabisa, mimi Mama Samia kiukweli nilikuwa sijamfahamu kivile maana nilikuwa ni mfanyabiashara kazi yangu ilikuwa nikukaa ofisini nilikuwa sifuatilii sana mambo ya siasa.

Mheshimiwa Naibu Spika, hata hivyo, kwa Hotuba yake ile ya kwanza tu ya kusema kwamba maumbile yangu ni ya kike imenipa moyo sana na kuzidi kuipenda siasa. Naamini sasa kumbe hata huyu aliyeingia ni mashine ile ile, ni kutwanga na kukoboa. Kwa maana hiyo niwaombe Waheshimiwa Wabunge huu sio wakati wa kampeni, ni wakati wa kufanya kazi kama jinsi Rais alivyokuwa anatunadi kwenye majukwaa kwamba, kuisimamia Ilani yenye page 303, kuna kazi ambazo zimeainishwa mle, tusiwasahau wananchi wetu waliotufanya kufika huku. Nimeona niwakumbushe tu hilo maana tunaweza tukawa tunasema Katiba labda tukiibadilisha tunaweza tena kushindwa kufika mjengoni, matendo yako ndiyo yatakayokufanya kuja huku au usije kabisa huku.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa maana hiyo niseme, wewe ni mwanamama vilevile na Rais wetu sasa hivi ni mwanamke, nami nina watani wengi sana hapa Wagogo niwatanie tu kidogo kwa kusema, mtutendee haki sisi wanaume hasa Kanda ya Ziwa, tulishazoea kuoa wanawake wengi sana na nimeangalia mfumo wa Katiba huu kumtambulisha mwanamke ni mmoja tu hapa Bungeni na sisi Wasukuma tunaoa zaidi ya wanawake 10, kwa hiyo kuna kila sababu ya kuifanyia marekebisho hiyo Ibara ili kusudi mwenye wake 11, watano au watatu waweze kutambulishwa kwenye Bunge lako hili Tukufu ili wapate haki zao za msingi na wao ni binadamu. Pia kama mnavyoisoma sayansi wanawake ni wengi wanaume tuko wachache, japokuwa unaweza ukawa wewe una mume mmoja ukawa unaumia sana lakini naongea kwa niaba ya Watanzania ili tusijifiche fiche sana; na kwakuwa akinamama sasa hivi wanasema sasa tayari tumeshawapa rungu wasilitumie rungu lao vibaya ili tukashindwa kuwarudisha tena madarakani miaka ijayo, miaka 2025 na miaka mingine. (Kicheko)

Mheshimiwa Naibu Spika, nitumie nafasi hii kumpongeza Makamu kwa Hotuba yake ya mchana aliyoiongea hapa, yeye kwanza amejitambulisha ni mtoto wa maskini na hasa maskini wanakuwaga na akili nyingi sana kuliko watoto wa matajiri. Kwa maana hiyo atumie hekima na busara sasa kuhakikisha kwanza Chama chetu cha Mapinduzi anatupa heshima ili tuweze kurudi tena humu Bungeni kiurahisi. Wabunge wengi wakipata madaraka pamoja na Waheshimiwa Madiwani na viongozi mbalimbali kupitia vyama huwa wanakisahau Chama. Kwa maana hiyo maneno yake yale aliyoyaongea mchana akiyaishi na sisi tukatembelea mlemle, hata kama utokee upinzani wa namna gani tutashinda tena kwa wingi na Watanzania wana imani na sisi sana hasa Chama cha Mapinduzi na mimi kweli imani imezidi kabisa kuongezeka kwamba hiki Chama kweli kiko imara.

Mheshimiwa Naibu Spika, nikimwangalia Waziri wa Mambo ya Nje yuko imara, Waziri wa Mambo ya Ndani yuko imara, kwa maana hiyo tusonge mbele kuhakikisha tunalinda rasilimali yetu na heshima ya Taifa letu, asitokee mtu akaja tena kututapeli kwa maneno ama kwa njia moja ama nyingine maana watu wa shetani wamejaliwa kuwa na maneno matamu sana, kama alivyosema Mheshimiwa pale kwamba sasa hivi tuachieni vyama, kweli watu wale wakiachiliwa wana maneno matamu na shetani alikuwa na maneno matamu vilevile hata Edeni pale alipomsogeza Eva akamdanganya Eva kula tena tunda ambalo halina matunda mazuri tukaingia kwenye dhambi.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa maana hiyo Watanzania tusiingie kwenye maneno ya kushawishiwa kama vile Eva alivyoshawishiwa Eden tukahukumiwa mwishowe tukaambiwa kufa tulikuwa hatufi lakini mpaka leo tunakufa. Kwa kukiamini Chama hiki cha Mapinduzi, lakini vilevile na sisi Wabunge tuko imara tuna uwezo kabisa wa kufanya chochote kile.

Mheshimiwa Naibu Spika, nikutoe wasiwasi tu sisi Wabunge wa awamu hii kiukweli kama ni timu ilikuwa imekuwa sorted, tuko tayari kwa lolote lile na ukitaka kujua Uchaguzi mdogo ule uliotangazwa mchana mimi naomba mnitume Buhigwe huko nikapambane na watu wa upinzani wenye maneno mabaya. Kwa maana mimi walinifundisha nazijua siasa za aina yeyote ile, siasa za matusi, siasa za kistaarabu, siasa za maombi, siasa za aina yeyote ile tutaenda kulipigania Jimbo la Mheshimiwa Philipo Mpango kuhakikisha kwamba linarudi kwenye Chama hiki pamoja na marehemu yule wa Kigoma sijui Jimbo gani, hivi alitokea jimbo gani? Nalo tutahakikisha linarudi kwenye Chama cha Mapinduzi. (Kicheko)

Mheshimiwa Naibu Spika, niwaombe tu Chama changu cha Mapinduzi uteuzi uliofanywa na Mama yangu Rais, umefanywa kila mtu kweli ameunga mkono hakuna mtu aliyepinga, maana amechagua chombo ambacho kinakubalika mbele ya Mungu na mbele za wanadamu ndiyo maana hakuna kura iliyoharibika. Wakiendelea kufanya hivyo hata kwenye kura za maoni kuchagua mtu anayetakiwa na Mungu maana uchaguzi wa Mungu mwanadamu hawezi akaushinda lakiniā€¦.

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

NAIBU SPIKA: Ahsante sana Mheshimiwa, kengele ya pili imegonga.

MHE. NICODEMUS H. MAGANGA: Nakushukuru sana, naiunga mkono hoja ila naomba Serikali iendelee kutusaidia zile ahadi za page 303, zitekelezeke ili turudi kwa urahisi huku. (Makofi)