Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Azimio la Bunge la Kutambua na Kuenzi Mchango wa Rais wa Tano wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. John Pombe Joseph Magufuli, kwa Utumishi wake Uliotukuka Pamoja na Azimio la Bunge la Kumpongeza Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan kuwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania

Hon. Asia Abdulkarim Halamga

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Azimio la Bunge la Kutambua na Kuenzi Mchango wa Rais wa Tano wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. John Pombe Joseph Magufuli, kwa Utumishi wake Uliotukuka Pamoja na Azimio la Bunge la Kumpongeza Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan kuwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania

MHE. ASIA A. HALAMGA: Mheshimiwa Naibu Spika, asante sana. Kwanza nianze na kuunga mkono azimio hili, maazimio yote mawili.

Mheshimiwa Naibu Spika, nianze kwa kuenzi na kutambua mchango wa Rais wa Awamu ya Tano, Hayati Dokta John Pombe Magufuli. Kweli ni wingu la simanzi lililotawala anga ya nchi yetu kwa kupoteza jemadari wetu wa mapambano, baba yetu, mzalendo wa zama zetu, rafiki yetu na Rais wa Awamu ya Tano, Hayati Dkt. John Pombe Joseph Magufuli. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nianze kukupa pole wewe na Watanzania wenzangu wote kwa msiba mzito uliolikuta Taifa letu kwa kumpoteza Rais wetu mpendwa Hayati Dkt. John Pombe Joseph Magufuli. Sisi vijana wa nchi hii tutamkumbuka Mheshimiwa Magufuli kwa kutuonesha njia sahihi ya kuipenda nchi yetu, kuilinda nchi yetu na kuwa majasiri katika kuitetea nchi yetu kwa gharama yoyote ile. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sisi vijana tutamuenzi Hayati Rais Magufuli kwenye vitu vikuu vitatu, miongoni mwa vitu vingi alivyoacha alama katika mioyo ya Watanzania, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, moja uzalendo. Hakuna kati yetu atakayepingana na ukweli kwamba, Hayati Rais Magufuli alikuwa mstari wa mbele pasipo kupepesa macho au pasipo kuwa na simile ya aina yoyote katika kuilinda na kuitetea nchi yetu dhidi ya adui yoyote wa nchi hii. Uhodari wake katika kulinda rasilimali za nchi hii, leo tuna ukuta wa Mererani, leo tuna Twiga Cooperation Limited na mengineyo mengi ikiwemo umahiri na uhodari wa utoaji huduma serikalini na zaidi kutetea dhana na kuaminisha kuwa nchi yetu ni nchi tajiri sana kupitia rasilimali zetu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mbili, uongozi wenye maono (Visionary Leader). Hayati Rais Magufuli ametufunza kuwa viongozi kwa kuangalia kesho na kukubali kufanya kazi ya kutesema ili kesho ya nchi yetu iwe nzuri zaidi.

Mheshimiwa Naibu Spika, tutazame miradi mikakati aliyoiona na kuisisitiza na kutimiza kama Bwawa la Umeme la Mwalimu Nyerere, ili kuzalisha umeme kwetu wa kutosha na hatimaye tunavyokwenda kujenga uchumi wa viwanda basi suala la umeme lisiwe lenye kutatiza tena. Mradi wa reli ya umeme ambayo licha ya kuunganisha mikoa ya kati na bandari yetu tunaenda kuunganisha nchi jirani kwa kuleta tija kwenye kufungua fursa za biashara na kufanya bandari yetu kukua. Vilevile Tunalinda miundombinu ya barabara na zaidi kupunguza muda wa usafirishaji wa mizigo, gharama za usafirishaji na pia kwani usafiri wa reli ni wa gharama nafuu kuliko wowote duniani. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tatu, mtaani kuna usemi tulikuwa tunataniwa sana na majirani zetu wa Afrika Mashariki kwa sera nzuri…

Mheshimiwa Naibu Spika, bado tuko katika siku 21 za maombolezo na ndiyo maana binafsi nimeamua kuandika kwa ajili ya kuendelea kuomboleza kifo cha Mheshimiwa Rais, lakini pia kwa ajili ya kumpongeza Mheshimiwa Rais Mama Samia Suluhu Hassan. Kwa hiyo, msinishangae kwa kusoma, kusoma nayo ni sehemu ya utaratibu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, hakika hakuna kitabu kitakachotosha kuongelea umahiri na uhodari wa uongozi wa Rais Magufuli zaidi ya kwamba Hayati Dkt. Magufuli ameacha uongozi wenye alama wa vit una alama ndani ya mioyo ya Watanzania. Nilihakikishie Bunge hili na Watanzania wote kuna kina Magufuli wengi ambao wamezalishwa katika kipindi chake. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nifupishe kwa kusema, Raha ya Milele Umme Ee Bwana, na Mwamba wa Milele Umuangazie. Apumzike kwa amani, amina.

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kutoa na kuunga mkono azimio la kwanza, sasa niende azimio la pili… (Kicheko)

(Hapa baadhi ya Wabunge walizungumza bila kufuata utaratibu)

MHE. ASIA A. HALAMGA:…la kumpongeza Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania...

…kuchekwa pia ni sehemu ya kuendelea mimi kuwa imara. Tuendelee kumpongeza Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, hakika sisi kama vijana tunajivunia. Kwanza hatuna hfunaye kwa kuwa tunachokipigania sasahivi kwa Watanzania ni maendeleo na maendeleo hayo hayatoki sehemu nyingine tofauti na kwenye Ilani ya Chama cha Mapinduzi, ambayo mwaka 2020 Mheshimiwa Mama Samia alipita kuinadi, na hapa Bungeni ndicho tunachoendelea kukitimiza. Tuendelee kumpongeza mama yetu na tumhakikishie kama vijana humu ndani tutahakikisha yale yote yatakayoletwa na Wizara na Mawaziri na Serikali juu ya maendeleo ya Watanzania na hasa kwa kuzingatia ilani yetu tutaunga mkono kwa asilimia 100. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nichukue nafasi hii kumpongeza Makamu wa Rais Mteule kwa kukalia kiti chake. Hivi karibuni tunaamini anakwenda kuapishwa. Sisi kama vijana hatuna hofu naye, tuna imaninaye kubwa kwa sababu, amehudumu katika Serikali ndani ya nchi na nje ya nchi. Hatuna hofu wala shaka na Dokta Mpango. Hakika tumepata Makamu wa Rais na sisi kama vijana tutahakikisha tunaunga mkono Serikali yetu na viongozi wetu ili kuendeleza amani, umoja na mshikamano wa Watanzania kwa maslahi mapana ya vijana sisi na vijana wajao.

Mheshimiwa Naibu Spika, nilitangulia kwa kusema kwamba, bado nipo kwenye simanzi japo tuna furaha ya kuwapata viongozi thabiti na madhubuti katika taifa letu. Naomba kwa siku ya leo niwe nimeishia hapo, asante sana. (Makofi)