Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Azimio la Bunge la Kutambua na Kuenzi Mchango wa Rais wa Tano wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. John Pombe Joseph Magufuli, kwa Utumishi wake Uliotukuka Pamoja na Azimio la Bunge la Kumpongeza Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan kuwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania

Hon. Neema Kichiki Lugangira

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Azimio la Bunge la Kutambua na Kuenzi Mchango wa Rais wa Tano wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. John Pombe Joseph Magufuli, kwa Utumishi wake Uliotukuka Pamoja na Azimio la Bunge la Kumpongeza Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan kuwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania

MHE. NEEMA K. LUGANGIRA: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru kwa fursa hii. Naomba nianze kwa kusema naunga mkono Maazimio yote mawili.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Sekta ya Asasi za Kiraia ambazo mimi ni mwakilishi wao hapa Bungeni kupitia nafasi ya Viti Maalum Chama cha Mapinduzi, napenda kuwasilisha pole za dhati kwa Mheshimiwa Rais Samia Suluhu Hassan kufuatia kifo cha Hayati Rais Magufuli. Vilevile napenda kuwasilisha salamu za pongezi kwa Rais wetu mpendwa Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan.

Mheshimiwa Naibu Spika, wiki hii zaidi ya asasi za kiraia 200 kutoka Bara na Zanzibar zimewasilisha tamko la pamoja la pongezi na pole kwa Mheshimiwa Rais Samia Suluhu Hassan. Vivyo hivyo, Jukwaa la Wanawake Wakurugenzi wa Asasi za Kiraia kwa maana ya CSO’s and NGO’s na wao pia wametoa tamko la pongezi kwa Mheshimiwa Rais Samia Suluhu Hassan.

Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kumfahamisha Mheshimiwa Rais Samia Suluhu Hassan kupitia Bunge lako Tukufu kuwa Sekta ya Asasi za Kiraia zina imani kubwa sana na yeye kwa sababu ana uzoefu mkubwa sana wa uongozi. Nitumie fursa hii kutaja maeneo machache. La kwanza, Mheshimiwa Rais Samia Suluhu Hassan alianza ajira yake kwenye mwamvuli wa mashirika yasiyo ya Kiserikali linaloitwa ANGOZA (Association For Non- Governmental Organizations in Zanzibar) na kwa mantiki hiyo Mheshimiwa Rais ni mwana Azaki mwenzetu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, la pili, Mheshimiwa Rais Samia Suluhu Hassan ana uzoefu mkubwa katika masuala ya uwezeshaji kiuchumi. Kupitia uzoefu huu mwaka 2016 Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa, Bani Ki Moon alimteua Mheshimiwa Rais Samia Suluhu Hassan akiwa Makamu wa Rais kuwa Mjumbe wa Jopo la Dunia kama mwakilishi wa Afrika lililopewa jukumu la kumshauri kwenye masuala ya uwezeshaji wanawake kiuchumi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, la tatu, miaka 25 iliyopita Mheshimiwa Rais Samia Suluhu Hassan akiwa anatokea Sekta ya NGO’s alishiriki katika Mkutano wa Beijing uliokuwa unalenga kuleta ukombozi wa usawa wa kijinsia ikiwemo wanawake kwenye nafasi za uongozi na maamuzi. Hivyo kupitia yeye kuwa Rais wetu wa kwanza mwanamke, Mheshimiwa Rais Samia Suluhu Hassan ameiwezesha Tanzania kuweka historia ya kuwa sehemu ya utekelezaji wa Maazimio ya Beijing. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kumalizia, nikiwa kama mdau wa lishe, sisi wadau wa lishe tunatambua juhudi kubwa ambazo Mheshimiwa Makamu wa Rais mteule ameweka katika kuhakikisha nchi yetu inaboresha hali ya lishe. Vivyo hivyo, tunatambua pia jitihada kubwa ambazo Makamu wa Rais mteule, Mheshimiwa Dkt. Phillip Mpango ambazo pia ameweka katika eneo hilo la kuboresha hali ya lishe kwa kuhakikisha kwamba Halmashauri zote nchini zinatenga bajeti ya lishe kwa kulingana na idadi ya watoto wenye chini ya umri wa miaka mitano. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kumhakikishia Mheshimiwa Rais Samia Suluhu Hassan kuwa Sekta ya Asasi za Kiraia itampa ushirikiano mkubwa katika kutekeleza dira yake ya maendeleo ya Taifa letu la Tanzania. Naomba nitumie fursa hii kipekee kuomba kuwasilisha ombi rasmi la kukutana naye kama Sekta ya Asasi za Kiraia ili nasi pia tuwe sehemu ya mafanikio yake.

Mheshimiwa Naibu Spika, tunamuomba Mwenyezi Mungu aendelee kumbariki na kumlinda Rais wetu, Mheshimiwa Rais Samia Suluhu Hassan. Mungu ibariki Tanzania, Mungu ibariki Afrika, ahsante. (Makofi)