Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Azimio la Bunge la Kutambua na Kuenzi Mchango wa Rais wa Tano wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. John Pombe Joseph Magufuli, kwa Utumishi wake Uliotukuka Pamoja na Azimio la Bunge la Kumpongeza Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan kuwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania

Hon. Saashisha Elinikyo Mafuwe

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Hai

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Azimio la Bunge la Kutambua na Kuenzi Mchango wa Rais wa Tano wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. John Pombe Joseph Magufuli, kwa Utumishi wake Uliotukuka Pamoja na Azimio la Bunge la Kumpongeza Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan kuwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania

MHE. SAASHISA E. MAFUWE: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nakushukuru sana kwa kunipa nafasi hii. Pia kabla ya kusema chochote, nitoe pole sana kwako wewe, kwa Mama Samia Suluhu kwa kuondokewa na Hayati Dkt. John Pombe Magufuli, familia ya Hayati Dkt. John Pombe Magufuli na Watanzania wote.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nianze kwa kumshukuru Mwenyezi Mungu ambaye ndiye aliyetuletea mwenyewe Mheshimiwa Hayati Dkt. John Pombe Magufuli. Hii kwangu naitafsiri kama ni zawadi kutoka kwa Mwenyezi Mungu kuja kwa Watanzania. Leo nasimama hapa kushukuru na kurudisha sifa na utukufu kwa Mwenyezi Mungu kwa zawadi hii ambayo alitupa ya Mheshimiwa Hayati Dkt. John Pombe Magufuli. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mtoa hoja ameeleza mambo makubwa ambayo yamefanywa na Hayati Dkt. John Pombe Magufuli, lakini Watanzania kwa hakika wanajua mambo haya makubwa yaliyofanywa na Mheshimiwa Hayati Dkt. John Pombe Magufuli. Ukiangalia kipindi cha maombolezo, ukianzia safari ya kuaga pale Dar es Salaam, hii ni dhahiri kwamba Watanzania wanajua haya mambo makubwa ambayo Hayati Dkt. Magufuli aliyafanya.

Mheshimiwa Naibu Spika, wananchi hawakujali ukubwa wa uzito wa uzio ulipo pale Uwanja wa Ndege. Wakatafsiri, ndege ni zetu wenyewe, Rais ni wetu wenyewe na sasa tunaingia wenyewe kwenye uwanja wetu. Waliingia kuonyesha mapenzi yao kwa Rais wao mpendwa wanayempenda. Vile vile kila mahali msafara ulipopita, wananchi walijitokeza kwa wingi. Hii ni ishara kubwa kwamba wananchi walimwelewa, walimpenda na hili ni zao la Watanzania kwa hakika. Naomba nishauri, haya mambo makubwa yaliyofanya tuyaweke kwenye kumbukumbu, niishauri Serikali ikiona inafaa itenge siku maalum iitwe Magufuli Day kwa ajili ya kumuenzi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, siyo hivyo tu, Serikali ione namna ya kufanya hapa Dodoma, jiji ambalo mwenzangu aliyepita ameshaeleza namna ambavyo alipambana kuhakikisha linakuwa Makao Makuu ya Nchi; kijengwe kituo maalum kwa ajili ya kutunza kumbukumbu zake. Hii itakuwa ni sehemu kubwa ya kuendelea kuenzi hayo mambo mazuri aliyoyafanya. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kuwa tayari alikuwa ameshaelekeza namna Wizara ya Elimu itakavyotengeneza mtaala wa kutengeneza historia yetu, basi kwenye mtaala wetu tuweke pamoja na viongozi wengine historia yake ili Watanzania waweze kuisoma vizuri.

Mheshimiwa Naibu Spika, nataka niseme, tunalo jambo la kujivunia kwa haya mambo makubwa ambayo wenzangu wameeleza. Leo tunazungumza uwepo wa reli, treni ya umeme; haya ni mapinduzi makubwa ya kihistoria ambayo yamefanyika wakiwa pamoja na Mheshimiwa Mama Samia Suluhu.

Mheshimiwa Naibu Spika, naenda moja kwa moja kwenye Azimio la pili. Haya mambo tunayoyataja leo, haya mambo tunayoyaona leo na kuyafurahia, barabara za chini na za juu zimejengwa, Vituo vya Afya vimejengwa, Mahakama wamejengewa ofisi nzuri. Kama wamejengewa Ofisi nzuri, watoto wanasoma kupitia Mfumo wa Elimu Bure, yamefanyika sambamba kwa kushirikiana na aliyekuwa Makamu wa Rais wakati huo ambaye leo ni Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Mama Samia Suluhu Hassan.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, sina mashaka hata kidogo kwamba miradi ile yote ambayo ilikuwa imepangwa itaendelea vizuri kabisa bila wasiwasi wowote. Tumeona katika kipindi cha muda mfupi, ndani ya siku tano, cha uongozi baada ya yeye kuapishwa kama Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, amefanya mambo makubwa ndani ya siku hizo tano. Kule Bandarini tumeona kilichotokea, hii ni ishara kwamba kiatu kilipotoka kimeingia kiatu kingine chenye size ile ile kwa speed nyingine kubwa. Kwa hiyo, tunayo matazamio makubwa sana. Hili lililotokea leo, nadhani wale ambao wanafuatilia kwenye mitandao, hapa kuna watu wamepigwa chenga ya mwili. (Kicheko/ Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, walichokuwa wanadhani kwamba sasa tunafika mahali tunaenda kuyumba kama nchi, wamepigwa chenga ya mwili mzima. Leo tumeletewa tena Mtumishi mwingine wa Mungu, mtu ambaye ni mzalendo, amechukua nafasi ya Makamu wa Rais. Nasi hapa bila tashwishi tumempitisha kwa asilimia mia. Nawapongeza sana ndugu zangu upande ule kule kwa namna ambavyo tumeungana kwenye jambo hili. Huu ndiyo msingi wa kuanzia leo, tuendelee kuungana kwenye mambo ambayo ni ya Kitaifa ili hata wale wengine walioko huko, ambao wamebaki na kazi ya kujifungia ndani, kazi yao ni WhatsApp, Twitter, kukashifu, kutukana nchi yetu, wajifunze kuanzia leo kwamba sisi ni Watanzania, tunaenda kusimama kuhakikisha Rais wetu anaenda kutekeleza yale yaliyopo kwenye Ilani ya Chama cha Mapinduzi na vile vile yale yote ambayo waliandika katika hotuba.

Mheshimiwa Naibu Spika, tutakumbuka hapa, Mheshimiwa Hayati Dkt. Magufuli alituletea hotuba hapa Bungeni inayoonyesha mwelekeo wa Serikali. Hotuba ile kwa hakika waliandaa pamoja na Mheshimiwa Rais, Mama Samia Suluhu. Kwa hiyo, haya yote yanaenda kutekelezwa kwa speed ile ile. Kwa hiyo, niwatumie salamu pia wale waliodhani kwamba tunaenda kukwama, Mungu ameshusha tena baraka nyingine na leo tumeshuhudia hapa namna ambavyo tunaenda kukimbia kwa speed. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naunga mkono na nawaomba sana Watanzania, tumwombee sana Mheshimiwa Rais wetu ili ayafanye yale ambayo ni matarajio yetu. Nasi kama Wabunge tusimame imara kuisaidia Serikali na kumshauri ili yale matarajio ya Watanzania yapate kutokea.

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema hayo, nakushukuru sana na naunga mkono hoja zote. (Makofi)