Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Mapendekezo ya Mpango wa Tatu wa Maendeleo wa Taifa kwa Miaka Mitano (2021/2022 – 2025/2026) na Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Mwaka 2021/2022 pamoja na Mapendekezo ya Muongozo wa Maandalizi ya Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka 2021/2022

Hon. Ng'wasi Damas Kamani

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Mapendekezo ya Mpango wa Tatu wa Maendeleo wa Taifa kwa Miaka Mitano (2021/2022 – 2025/2026) na Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Mwaka 2021/2022 pamoja na Mapendekezo ya Muongozo wa Maandalizi ya Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka 2021/2022

MHE. NG’WASI D. KAMANI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa nafasi hii ya kuweza kuchangia hotuba hii ya Mpango wa Maendeleo wa Miaka Mitano na Mwaka Mmoja. Nianze kwa kumpongeza Waziri Dkt. Mpango kwa Mpango huu mzuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hata hivyo, kama mwakilishi wa vijana nina machache tu ya kushauri juu ya namna gani tunaweza tukashughulikia au kutatua tatizo la ajira. Wote ni mashahidi kwamba kila Mbunge anayesimama ni dhahiri anakerwa na tatizo la ukosefu au upungufu wa ajira kwa vijana. Nina ushauri wa namna mbili tu na ndiyo zitakuwa points zangu za msingi kwa jioni ya leo. Kwanza, ni namna gani tunaweza kutumia Mifuko ya Hifadhi za Jamii kutatua changamoto ya ajira; na pili, namna gani vijana tuafikia uchumi wa kweli wa viwanda. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika suala la namna gani tunaweza kutumia Mifuko ya Hifadhi za Jamii kutatua changamoto ya ajira, nianze kwa kuipongeza Ofisi ya Waziri Mkuu, Kazi, Vijana na Ajira kwa kuleta katika Bunge hili Tukufu Sheria ya Mifuko ya Hifadhi za Jamii, mwaka 2018 na Bunge hili Tukufu likapitisha sheria hiyo ambapo mpaka sasa mifuko yetu tunaendelea nayo vizuri. Ni-declare kwamba niko katika Kamati ya Katiba na Sheria ambayo inasimamia mifuko hii. Kwa hiyo, nafahamu namna mifuko hii inafanya kazi na mpaka sasa imefikia wapi. Napenda tu kusema kwamba tusiamini yale tunayosikia kwamba mifuko hii haiko vizuri. Mifuko hii inaendelea vizuri na tunaamini itakwenda kufanya vizuri zaidi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwaka 2018 ilipotungwa Sheria hii ya mabadiliko ya Mifuko ya Hifadhi za Jamii, kifungu cha 91(1) cha Sheria ya NSSF kinaruhusu mfuko huu kupokea michango kutoka kwa watu walioko kwenye informal sectors au ajira zisizo rasmi. Watu hawa wanatoa michango ya shilingi 20,000/= tu kwa mwezi ambayo ni sawa na shilingi 650/= kwa siku. Baada ya kupokea michango hii, mtu akishafikisha miaka miwili, anakuwa na uwezo wa kupokea fao ambalo ni aidha atapata vifaa, mashine au mtaji wa kuanzisha kiwanda kidogo. Hii inafanyika kupitia SIDO na Benki shirikishi za mfuko huu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ushauri wangu ni kama ifuatavyo. Changamoto ya kwanza tunayokutana nayo sisi kama vijana hasa wale ambao tunatoka vyuoni, kwanza anayetaka kuajiriwa katika mfumo ulio rasmi, anapata changamoto ya kukosa uzoefu (experience). Pia yule anayetaka kwenda kujiajiri, hana mtaji na hakopesheki katika benki na taasisi nyingine za fedha kwa sababu hana collateral au dhamana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa kama tukiamua kupeleka utaratibu huu kwenda vyuoni moja kwa moja, tukahamasisha vijana walioko katika vyuo na vyuo vikuu kuweza kupata mchango wa Sh.20,000/= kila mwezi, ambapo kijana huyu atachanga kwa muda wa miaka miwili, mitatu au minne kutegemea na kipindi chake anachokaa chuoni. Akitoka hapo, kijana huyu kupitia benki hizi shirikishi chini ya Mfuko wa NSSF na SIDO anakuwa anaweza kukopesheka aidha mashine, kifaa cha kazi au anaweza kukopesheka kwa mtaji kwa ajili ya kuanzisha viwanda vidogo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naamini Wizara husika ikikaa na kuangalia mpango huu, itakuwa tumepata mwarobaini wa tatizo la ajira kwa vijana wanaotoka katika vyuo na vyuo vikuu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, siyo hivyo tu, napenda kusema kwamba tutakuwa ndiyo tumeondoa tatizo la ajira kwa upande wao, lakini tutakuwa tumeiongezea nguvu mifuko hii ambayo kwa namna moja au nyingine naweza nikasema ni National Security. Kwa sababu fedha hizi ndizo zinazotumiwa na Serikali yetu kuwekeza katika miundombinu na katika huduma mbalimbali za jamii. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, siyo hivyo tu, vijana hawa wakienda kujiajiri wenyewe…

T A A R I F A

WAZIRI WA NCHI, OFISI YA WAZIRI MKUU (SERA, BUNGE, VIJANA, KAZI, AJIRA NA WATU WENYE ULEMAVU): Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa.

MWENYEKITI: Mheshimiwa Waziri wa Nchi. Mheshimiwa Ng’wasi ukae chini halafu uzime microphone. Ahsante.

WAZIRI WA NCHI, OFISI YA WAZIRI MKUU (SERA, BUNGE, VIJANA, KAZI, AJIRA NA WATU WENYE ULEMAVU): Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kweli nampongeza sanasana Mbunge huyu kijana kwa mchango wake na umahiri mkubwa wa kiushauri anaoutoa sasa hivi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kumpa taarifa kwamba kwa hesabu na taarifa niliyonayo kama Waziri wa Sekta kwa sasa, Mfuko wa NSSF ambao unashughulika na private sector, asilimia 100 ya makusanyo, ni asilimia 40 tu ndiyo inayotosha kulipa aina zote za mafao na kubakiwa na asilimia 60 ya makusanyo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa asilimia ile 60 ya makusanyo, mimi kama Waziri wa Sekta, kwa kushirikiana na vijana wazalendo kama huyu anayechangia hapa, tukatengeneza kwa pamoja programu nzuri, nadhani ushauri huu unaweza kuwa ni muafaka kabisa wa kutafuta mwarobaini kwa ajili ya kuwahudumia vijana wetu na kutatua tatizo la ajira. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nami kwa taarifa hii kwa kweli ningefurahi kumpa Ubalozi au Champion wa kuwasaidia vijana. (Makofi)

MWENYEKITI: Mheshimiwa Ng’wasi Kamani, unapokea taarifa hiyo?

MHE. NG’WASI D. KAMANI: Mheshimiwa Mwenyekiti, naipokea na nitafurahi sana kuwa Balozi. (Kicheko/Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sambamba na hayo, tumesikia hapa kwamba kuna changamoto kubwa sana katika mikopo ya elimu ya juu. Mpango huu kama ukifanikiwa, utasaidia vijana hawa wanaotoka vyuoni moja kwa moja kuingia katika mpango wa kujiajiri na kuajiri wengine kuweza kuanza mara moja kurejesha mikopo yao ya elimu ya juu na kuepuka suala zima la riba. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, siyo hivyo tu, llani yetu ya Chama cha Mapinduzi ya mwaka 2020 – 2025 inaahidi kwamba kuna ajira milioni nane ndani ya miaka hii mitano zinatakiwa kuzalishwa. Kwa mpango huu, kama ukifanikiwa, maana yake suala hili la ajira milioni nane linakwenda kuwa rahisi na linakwenda kufanikiwa moja kwa moja. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, point yangu ya pili inakwenda sambamba na hii, ni namna gani vijana tutafikia uchumi wa kweli wa viwanda? Tunapozungumzia uchumi wa viwanda hasa kwetu sisi vijana ambao ndiyo kwanza tunaanza maisha, hatuzungumzia viwanda vya billions of money au millions of money, a hundred of millions, hapana; tunazungumzia viwanda vidogo vidogo ambavyo kila mtu atakuwa na uwezo wa kukianzisha kwenye chumba chake au kwenye nyumba yake. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, viwanda hivi vitawezekana tu kwetu sisi vijana kama tukitoa bajeti ya kutosha kwenda kwenye SIDO na TIRDO. Taasisi hizi ndizo pekee ambazo zina uwezo wa kutusaidia sisi kupata mashine zenye efficiency sawa lakini kwa gharama ya chini. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninao mfano wa mfanyabiashara aliyetaka mtambo wa kutengeneza ethanol kwa kutumia zao la mihogo. Mtambo huu huu Brazil na China ulikuwa ni shilingi milioni 850, lakini mtambo huu huu, model ile ile baada ya kuwa studied na TIRDO wametoa mapendekezo ya kuweza kuutengeneza kwa shilingi milioni 150. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, maana yake ni nini? Mitambo ambayo tunaweza kuipata katika nchi jirani kwa gharama kubwa, tunaweza tukaitengeneza sisi wenyewe katika nchi yetu kwa gharama ya chini ambayo itatusaidia vijana kuweza kushiriki moja kwa moja katika uchumi wa viwanda na kukuza pato la Taifa. Naomba katika Mpango huu mawazo haya tuyaangalie namna tunavyoyaweka ili sisi kama vijana tupate kunufaika. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hata hivyo, bado deni la msingi linabaki kwa Wizara ya Elimu. Vijana tukitoka vyuoni, hata tukitengenezewa mazingira mazuri kiasi gani, kama elimu tuliyopata katika shule tulizosoma haitusaidii au haitu- equip kuweza kuwa na uelewa wa kutosha wa kijamii, maana yake mambo haya yote ni bure. Mama yangu Mheshimiwa Ndalichako nakuamini, naomba sana mpango mfumo wa elimu uangaliwe kwa kushirikisha wadau wakiwemo vijana, nini hasa kinaweza kubadilishwa katika mfumo wetu wa elimu ili vijana watoke shuleni wakiwa na uwezo wa kuishi katika jamii zetu (real societies). (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kusema hayo, naunga mkono hoja, nashukuru sana. (Makofi)