Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Mapendekezo ya Mpango wa Tatu wa Maendeleo wa Taifa kwa Miaka Mitano (2021/2022 – 2025/2026) na Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Mwaka 2021/2022 pamoja na Mapendekezo ya Muongozo wa Maandalizi ya Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka 2021/2022

Hon. Prof. Patrick Alois Ndakidemi

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Moshi Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

2

Ministries

nil

Mapendekezo ya Mpango wa Tatu wa Maendeleo wa Taifa kwa Miaka Mitano (2021/2022 – 2025/2026) na Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Mwaka 2021/2022 pamoja na Mapendekezo ya Muongozo wa Maandalizi ya Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka 2021/2022

MHE. PROF. PATRICK A. NDAKIDEMI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana kwa fursa ya kuchangia Mpango wa Tatu wa Maendeleo wa Miaka Mitano na ule wa Mwaka Mmoja wa 2021/2022. Kutokana na uhaba wa muda, nitachangia kwenye eneo la kilimo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kilimo ni sekta muhimu sana. Karibu kila Mbunge aliyesimama hapa na hata Mabunge yaliyopita; nimekuwa nafuatilia kwenye runinga, hii ni mara yangu ya kwanza, Wabunge wengi walikuwa wanaonyesha hisia zao kwamba kilimo ni muhimu. Pamoja na huo umuhimu, bado kilimo kina changamoto kubwa kwamba hatujawekeza kikamilifu kwenye miradi ya kilimo. Bado hatujawa serious sana kwenye kilimo kama ambavyo Wabunge wengi wameonyesha hisia zao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika wasilisho alilotoa Waziri wa Fedha na Mipango, miaka mitano iliyopita tuliwekeza vizuri sana kwenye miradi mikubwa ya maendeleo na nitaitaja hapa. Tuliwekeza vizuri sana trillions of money kwenye SGR, tulitoa 3.79 trillion, tukawekeza kwenye barabara 8.6 trillion, tukawekeza kwenye elimu 3.15 trillion, tukawekeza kwenye ndege 1.24 trillion, kwenye maji 2.03 trillion, kwenye umeme na nishati 2.83 trillion. Ni kitu kizuri na hii miradi imetupa heshima kubwa sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye kilimo sasa, miaka mitano iliyopita fedha iliyokwenda Wizara ya Kilimo ilikuwa ni shilingi bilioni 189.9 tu. Niseme tu, kwa mawazo yangu, nafikiria kiasi hiki kilikuwa ni kidogo sana kwa miaka mitano. Hebu tujiulize, sote tunakiri kwamba kilimo ndiyo uti wa mgongo wa Taifa hili, ni nini kinatukwaza tusiwekeze fedha za kutosha kwenye sekta ya kilimo? Nina hakika tukijitoa kikamilifu tukawekeza kwenye kilimo, tutamkwamua mkulima, tutalikwamua Taifa hili na sote tutaingia kwenye uchumi wa kati tukiwa pamoja na wakulima wetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nashauri kwamba sasa ni wakati wa kufanya maamuzi magumu tuwekeze trillions kwenye kilimo na siyo billions kama ilivyokuwa kwenye miaka mitano iliyopita. Tuwekeze trillions kwenye kilimo ili tuweze kusaidia nchi yetu kwa Pamoja kwa sababu kilimo ndiyo kinachoajiri watu wengi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tukiwekeza fedha za kutosha kwenye kilimo, zitatusaidia mambo mengi sana. Sitaki kuyarudia lakini machache ambayo wenzangu wameshayasema, tutasaidia vituo vya utafiti na huduma za ugani. Namshukuru sana Waziri wa Kilimo, amesimamisha Maonyesho ya Nane Nane, ameshaona kuna shida kwenye ugani, amesema fedha zielekezwe kwenye Ugani. Kwa hiyo, tutasaidia huduma za Ugani na uzalishaji mbegu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tukiachana na hilo, tukiwekeza fedha nyingi kwenye kilimo, hizo trilioni ambazo nashauri, zitasaidia sana kutekeleza ujenzi wa miundombinu ya umwagiliaji, tutachimba mabwawa ya kutosha, tutachimba visima mahali popote palipo na maji kwenye nchi hii, tutarekebisha ile miundombinu ya mifereji ya asili ambayo ipo nchi nzima na tumeiacha haijafanyiwa kazi sana. Tukisharekebisha hii mifereji tutakuwa na maji ya kutosha.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni nini kitatokea tukishakuwa na maji ya kutosha? Maji yatasambaa nchi nzima kwa ajili ya kilimo kama tulivyosambaza umeme na barabara. Tukishafikia hapo, maji yakishapatikana, tutalima kwa uhakika na kuvuna zaidi ya mara mbili kwa mwaka. Kile kitu ambacho Mheshimiwa Bashe na Wizara ya Kilimo walikuwa wanasema block farming, kitafanyika kwa uhakika, kwa sababu tutakuwa na maji ya kupeleka kwenye hizi blocks ili tuweze ku-irrigate na watu wazalishe mazao ya kutosha.

Mheshimiwa Mwenyekiti, maji yakishapatikana, wakulima wetu hawatasita kwenda kuchukua mikopo benki. Watakuwa na uhakika wa kuzalisha na kupata kitu. Watakwenda kukopa TIB na Benki ya Kilimo na maisha yataanzia hapo, watu watafanya vizuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, najua muda umeisha lakini niseme tu, ni vyema pia tuwezeshe hizi benki; TIB na Benki ya Kilimo, wapewe mitaji ya kutosha na waelekezwe kuwa na window maalum ya kuwasaidia wakulima wadogo wadogo, siyo wakulima wakubwa tu. Kwa hiyo, tukifanya hivyo, tutakuwa tumewasaidia wakulima na watazalisha vya kutosha. Wakishazalisha vya kutosha, tutaanzisha viwanda na tutafanya mambo mengi ambayo yataleta maendeleo kwa Taifa letu, tutamkwamua mkulima kutoka kwenye umasikini na tutakuwa tunakwenda mbele.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nisemeā€¦

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MWENYEKITI: Ahsante sana Profesa. Nakushukuru sana.

MHE. PROF. PATRICK A. NDAKIDEMI: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kuunga mkono hoja. (Makofi)