Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Mapendekezo ya Mpango wa Tatu wa Maendeleo wa Taifa kwa Miaka Mitano (2021/2022 – 2025/2026) na Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Mwaka 2021/2022 pamoja na Mapendekezo ya Muongozo wa Maandalizi ya Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka 2021/2022

Hon. Maimuna Salum Mtanda

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Newala Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

2

Ministries

nil

Mapendekezo ya Mpango wa Tatu wa Maendeleo wa Taifa kwa Miaka Mitano (2021/2022 – 2025/2026) na Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Mwaka 2021/2022 pamoja na Mapendekezo ya Muongozo wa Maandalizi ya Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka 2021/2022

MHE. MAIMUNA S. MTANDA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipatia nafasi hii. Awali ya yote, namshukuru Mwenyezi Mungu, lakini pia naishukuru Wizara ya Fedha kwa uwasilishaji mzuri wa Mpango wa Miaka Mitano inayokuja kwa Taifa letu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunapozungumzia Mpango huu, tuna maana kwamba ni mwelekezo wa Serikali kwa miaka mitano ijayo. Sasa ili kuutendea haki Mpango huu na yale matarajio tunayoyatarajia yaweze kupatikana vizuri, kuna mambo lazima yaboreshwe ikiwemo rasilimali watu, lazima iwepo, miundombinu iboreke na vitu kama hivyo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze kwa kuwapongeza wenzetu wa Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia kwa sababu wametuwezesha na kutuelewa sisi Wananewala kwa kuwaendeleza na kuchukua majengo ambayo yalikuwa ya NDF ili kuwa VETA. Sisi Wananewala tuna kiu kubwa ya kupata ajira kwa vijana wetu, kwa hiyo, tukawakabidhi wenzetu wa Wizara ya Elimu majengo ili yatumike kama VETA na vijana wetu wakapate ujuzi, waweze kujiajiri wenyewe na kisha maendeleo ya watu yaweze kupatikana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni jambo jema, lakini majengo yale yatatumiwa na Wilaya zaidi ya moja kwa maana ya Tandahimba, hakuna VETA, ni majirani zetu, watatumia pale; Masasi kwa maana ya Lulindi, hawana VETA, watatumia pale na Wananewala. Kwa hiyo, naiomba Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia ituongezee au itujengee mabweni ili wanafunzi watakaoenda kusoma pale wapate elimu na ujuzi unaotosheleza bila kuhangaika, mwisho wa siku wakapate wao wenyewe kujiajiri na maendeleo ya nchi yaweze kupatikana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ili maendeleo yaweze kupatikana, lazima miundombinu iboreshwe hasa barabara. Wananewala Vijijini wana barabara yao ambayo inaunganisha Mkoa wa Lindi na Mtwara kwa maana ya Wilaya ya Lindi Vijijini na Newala; barabara ya kutoka Mkwiti – Kitangali hadi Amkeni. Barabara ile ni ya vumbi, lakini ikiboreshwa kwa kiwango cha lami, tuna uhakika kabisa kwamba mawasiliano yatakuwa rahisi, watu watafanya biashara, watakuwa wanasafiri kutoka eneo moja na kwenda eneo lingine na kujipatia fedha ambazo wataenda kuendeleza maisha yao na kuachana na hali ambayo wanayo kwa sasa. Kwa hiyo, naiomba Wizara ambayo inasimamia ujenzi, kwa sababu tunataka kuboresha au kuleta maendeleo ya watu, basi itujengee barabara ile kwa kiwango cha lami ili nasi maendeleo yetu yaweze kupatikana kwa urahisi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna mchangiaji ambaye amezungumzia suala la utafiti kwa vyuo vyetu vya kilimo, ni muhimu sana. Utafiti wa mazao ni muhimu sana. Kwa hiyo, naiomba Serikali iongeze fedha kwenye vyuo vya utafiti ili waweze kufanya utafiti wa mara kwa mara ambapo watakuwa up to date na hali ya mabadiliko ya mazao yetu kwa kadri inavyojitokeza. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sisi Wanamtwara tunalima korosho ambazo zina magonjwa mbalimbali; ni kama binadamu, magonjwa yanabadilika kila leo. Kwa hiyo, tusipowekeza kwenye utafiti wakulima wetu wakapata kujua aina ya magonjwa ambayo yanajitokeza kwa wakati huo kupitia watafiti wale wa TARI Naliendele, nadhani tutakuwa hatufanyi chochote na uzalishaji wa zao la korosho utakuwa unapungua kadri ya siku zinavyokwenda. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia niunganishe na Maafisa Ugani. Tunaomba Maafisa hawa wawepo kwenye vijiji vyetu, kwa sababu sasa hivi tunavuna lakini kiholela…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MWENYEKITI: Ahsante sana.

MHE. MAIMUNA S. MTANDA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Naunga mkono hoja, lakini tunaomba tupatiwe Maafisa Ugani ili wakawasimamie wakulima wetu ipasavyo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana. Kwa mara nyingine naunga mkono hoja. (Makofi)