Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Mapendekezo ya Mpango wa Tatu wa Maendeleo wa Taifa kwa Miaka Mitano (2021/2022 – 2025/2026) na Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Mwaka 2021/2022 pamoja na Mapendekezo ya Muongozo wa Maandalizi ya Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka 2021/2022

Hon. Saashisha Elinikyo Mafuwe

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Hai

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Mapendekezo ya Mpango wa Tatu wa Maendeleo wa Taifa kwa Miaka Mitano (2021/2022 – 2025/2026) na Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Mwaka 2021/2022 pamoja na Mapendekezo ya Muongozo wa Maandalizi ya Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka 2021/2022

MHE. SAASHISHA E. MAFUWE: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Kwanza nianze kumshukuru sana Mwenyezi Mungu ambaye ametupa uzima na zawadi ya kuwa na Mheshimiwa Rais Dkt. John Pombe Magufuli, Rais ambaye amefanya mengi na ambaye tunategemea ataendelea kuyafanya mengi kwa kipindi cha miaka mitano iliyobaki. Pia nishukuru sana viongozi wenzake Makamu wa Rais, Waziri Mkuu, Mawaziri na Naibu Mawaziri kwa kazi nzuri wanayoifanya kwa Taifa letu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, shukrani za pekee ziende kwa watumishi wa umma Tanzania nzima. Hawa ndiyo wanaotekeleza mipango ambayo sisi tunaipanga hapa na kama ambavyo wamemsikia Mheshimiwa Waziri Mkuu kwamba wasiwe na wasiwasi Serikali yao inawapenda na kama alivyosema Mheshimiwa Rais yeye haongezi vibaba vibaba ataongeza mzigo wa kutosha, kwa hiyo, waendelee kushirikiana nasi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo, lipo jambo nimeliona hapa. Wakati najiandaa kuchangia hapa, nimesoma kwanza Mpango uliopita yale mapendekezo yaliyoletwa humu Bungeni, nikasoma Hansard za Wabunge walivyochangia na nikapitia kwenye changamoto ambazo zimesababisha Mpango ule usitekelezwe kwa asilimia 100, nikajifunza kitu ambacho naomba sasa wakati Waziri anakuja kuhitimisha atuambie hapa ni kwa asilimia ngapi hii michango ya Wabunge hapa inaenda kufanya mabadiliko kwenye rasimu hii tunayoijadili na kuleta Mpango ulio kamili? Tusipopata asilimia ya namna ambavyo michango yetu inaingizwa kwenye Mpango huu na mabadiliko yakatokea tutakuwa tunazungumza hapa halafu hayafanyiwi kazi. Kwa hiyo, niombe sana wakati anakuja kuhitimisha atuambie michango yetu imeingizwa kwenye Mpango huu kwa asilimia ngapi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niseme jambo lingine, wote hapa tunasema, hata dada zangu kule wanakiri kwamba Mheshimiwa Rais anafanya kazi nzuri mno ya kutukuka lakini swali langu, hii kazi nzuri inayofanywa na Mheshimiwa Rais itakuwa sustainable, itaendelea kuishi? Hii miradi mikubwa inayoanzishwa na Serikali itaendelea hata kama yeye hayupo? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nachokishauri sasa tuweke mifumo ambayo itasaidia hizi shughuli nzuri zinazofanywa ziendelee kuishi. Hapa kuna wanasheria na Mwanasheria wa Serikali atusaidie, huko kwenye nchi zilizoendelea wana vitu vyao kama interest za Taifa lao, hivi hapa Tanzania hatuwezi kuwa na mambo yetu ambayo ni interest ya Tanzania na yakae kwenye Mpango wa muda mrefu hata kama ni miaka 50 kwa kuanzia baadaye twende miaka 100 ili tuwe na Mipango ya muda mfupi ya mwaka mmoja kama tunavyojadili sasa hivi lakini tuwe na Mipango ya miaka mitano?

Mheshimiwa Mwenyekiti, nayasema haya kwa sababu tunafahamu namna siasa zetu zinavyoenda. Mara nyingi unakuta viongozi wanacheza beat kulingana na mpigaji anavyopiga ngoma. Sasa tunataka tutengeneze ngoma ya Watanzania ambayo tunaweza kuipiga kwa kipindi cha miaka 50 tuone hayo mambo ambayo yamewekwa yawe ni msingi na yaendelee. Namna ya kuyafanya yawe endelevu ni sisi Wabunge kuweka sheria za kubana lakini pia kuwa na taasisi ambazo ni strong zinazoweza kufanya maamuzi na kuyasimamia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tukifanya hivyo tutakuwa tumemfaidi Mheshimiwa Rais tuliyenaye sisi wa kizazi hiki na kizazi kijacho. Tukiacha haya, iko hatari kwamba akiondoka Mheshimiwa Rais na haya yataondoka, atakuja mwingine tutacheza ngoma nyingine.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niombe pia hebu tutazame mfumo wa elimu ya Tanzania, je, unatupa output nzuri kwa watu wetu? Wapo Wabunge wamechangia hapa na utaona kuna kitu ambacho tunakifanya. Sisi tuna-base kwenye kuangalia mazingira zaidi lakini ubora wa elimu bado hatujauweka vizuri. Je, mtaala tulionao una-reflect National objectives maana yake ni kwamba hii Mipango ya Taifa tunayoipanga tukienda kwenye mitaala yetu tunaikuta? Tunataka Serikali ya viwanda, je, mifumo ya elimu inatupeleka huko kuandaa watu waje wafanye kazi kwenye viwanda hivi?

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, niombe pia wakati tunapanga Mipango hii tutazame pia suala la mitaala yetu. Kwa sababu moja ya changamoto iliyosababisha Mpango ule usitekelezwe kwa asilimia 100 ni kwamba nchi hii hatuna wataalam wa kuandika maandiko. Hii siyo sawa, watoto wanamaliza vyuo kila siku tunawezaje kuweka challenge kama hii, kwa hiyo, kuna shida.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini lingine hapa tunaangalia michango yetu na hili siyo zuri sana ninavyolitazama mimi. Nitoe mfano mtoto wangu aliniuliza swali juzi hapa, akaniuliza baba hebu niambie, mle Bungeni kuna Mbunge anaitwa Musukuma na Mbunge mwingine wa Kahama, wanachangia vizuri kweli lakini wao wanasema darasa la saba. Zaidi ya hivyo, tunaambiwa wamefanikiwa kwenye maisha, hivi kuna sababu ya kusoma?

Mheshimiwa Mwenyekiti, hili swali ingekuwa ni wewe, ungemjibuje mtoto akikuuliza kitu cha namna hiyo? Iko sababu ya kupita kwenye mfumo wa elimu ili tuweze kuwa na wataalam ambao wana output nzuri. Hata hii tunayosema kuwa sisi tuna sera nzuri, sera nzuri ni ile ambayo ina strong tools of implementation ambazo zinaleta output nzuri. Kwa hiyo na hili pia tunapoangalia tulitazame. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo lingine ambalo nimetaka kuchangia ni kwenye kilimo.

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MWENYEKITI: Muda hauko upande wako Mheshimiwa.

MHE. SAASHISHA E. MAFUWE: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye kilimo…

MWENYEKITI: Dakika tano tayari zimeisha.

MHE. SAASHISHA E. MAFUWE: Mheshimiwa Mwenyekiti, ndiyo nilikuwa naanza? (Kicheko)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba niseme kwa dakika moja tu tafadhali sana, kwa kuwa Jimbo la Hai lilifanya kazi kubwa sana, naomba niongezee.

MWENYEKITI: Haya, dakika moja.

MHE. SAASHISHA E. MAFUWE: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba niseme kwenye eneo la kilimo. Pale Hai tukiamua kuna vyanzo vya maji vya kutosha, kuna ardhi nzuri tuko tayari kufanya kazi. Tukipewa vyanzo hivi vya maji tutalima na tutachangia kwenye Pato la Taifa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini kwenye Vyama vya Ushirika, kaka yangu Mheshimiwa Nape tumezungumza sana, iko shida. Kule Hai hatuna ardhi ya kutosha lakini tuko tayari kufanya kazi lakini Vyama vya Ushirika vimekumbatia mashamba yetu, wanachokifanya mle ndani hatujui, ukiwaambia ni wataalam wa kufanya lobbying za kutosha. Tafadhali sana ile team niliyoomba iende kule Hai, Mheshimiwa Waziri Mkuu uko hapa, iko shida, uko utajiri mkubwa kule Hai kama tukiamua kufanya kazi. Ahsante sana. (Makofi)