Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Mapendekezo ya Mpango wa Tatu wa Maendeleo wa Taifa kwa Miaka Mitano (2021/2022 – 2025/2026) na Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Mwaka 2021/2022 pamoja na Mapendekezo ya Muongozo wa Maandalizi ya Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka 2021/2022

Hon. Issaay Zacharia Paulo

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mbulu Mjini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Mapendekezo ya Mpango wa Tatu wa Maendeleo wa Taifa kwa Miaka Mitano (2021/2022 – 2025/2026) na Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Mwaka 2021/2022 pamoja na Mapendekezo ya Muongozo wa Maandalizi ya Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka 2021/2022

MHE. ZACHARIA P. ISSAAY: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi hii ya kutoa mchango wangu kwenye Bunge hili. Kwanza nachukua nafasi hii kumshukuru sana Mwenyezi Mungu kwa majaliwa yake kwetu sote na kwa Taifa na sisi Watanzania wote. Pia nachukua nafasi hii kumpongeza sana Mheshimiwa Rais kwa jinsi anavyoongoza Taifa letu toka kipindi kilichopita na sasa. Vile vile nawapongeza wachangiaji wote wa leo kupitia Muswada huu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo sitachangia mpango huu, naomba univumilie, nizungumze kama Mbunge wa Jimbo la Mbulu Mji, lakini pia kama Mbunge wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Mchango wangu ni mdogo sana. Kwanza, ni namna gani ambavyo wananchi wangu wa Jimbo la Mbulu Mji wanapata tabu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tuna kigugumizi cha kuzungumza suala la Corona. Jimbo langu wamepotea nikiwa huku Bungeni kwa mwezi mmoja watu wengi kidogo. Ukanda ule ni wa baridi. Naomba niishauri Serikali, tumekuwa na matumizi ya dawa za asili, tumekunywa kama gongo, yaani tunakunywa tu bila kujua hali halisi ikoje. Ni kwa nini Serikali isichukue jukumu la kuchukua dawa zote za Waganga wa Asili ikapeleka kwa Mkemia Mkuu wa Serikali halafu ikaja na kauli ya kutuambia angalau ni dawa zipi tuweze kutumia?

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa sababu inaonyesha vifo vilivyotokea kwenye Jimbo langu, sehemu kubwa vina viasharia vya mtu kushindwa kupumua, maumivu ya kifua na hali kadhalika. Nimekwenda Jimboni, nikaja kwako mara kadhaa kuomba kibali, wakati mwingine nimetoroka hata bila kuja kwa sababu nakwenda Jimboni, narudi; nafika huku mtu wa karibu amefariki, narudi tena.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, nawapongeza sana Waganga wa Asili waliochemsha miti shamba wakanywesha Watanzania. Waheshimiwa Wabunge tuliokuwa na kigugumizi, asilimia kubwa tumeshakunywa; nami nimeshakunywa. Ni kwa sababu sikubaliani na chanjo ya watu wa Magharibi, lakini nakubaliana na naamini dawa za asili.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali inashindwa nini kutumia wataalam wa ndani na vyombo tulivyonavyo kufanya utafiti ili angalau hizi dawa za asili sehemu fulani tujue ina msaada? Kwa sababu Jimbo langu la Mbulu watu wanapata matatizo. Hata leo niliitwa kwenda kuzika mtoto wa Diwani, nikawaambia jamani, Bunge liko ukingoni, ninyi muendelee tu. Ukiuliza, dalili ni hiyo hiyo; na ukanda wetu una baridi. Hilo la kwanza. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, la pili, majaribio haya ya dawa za asili ambayo tunakunywa kutoka Bunge lililopita na Bunge hili la sasa, mimi nimekunywa, sijui wengine, lakini naona matokeo yake ni chanya katika kutatua tatizo hili. Je, ni kwa nini basi kama hatuna wataalam au vyombo tusiagize hata wataalam wa nchi nyingine na vyombo nchi nyingine tufanye utafiti?

Mheshimiwa Mwenyekiti, nazungumza haya kwa sababu nina machungu. Itafika mahali hata hao wanaotupima hapo getini, Manesi wanaotuhudumia hospitalini; juzi nilienda Benjamin Mkapa kupata vipimo nikaambiwa Mheshimiwa mitungi haitoshi. Mitungi ya oxygen Benjamin Mkapa haitoshi. Pia mashine za oxygen hazitoshi. Najua kuna watu watanielewa vibaya, wacha wanielewe vibaya, mimi nimepewa dhamana ya kuja kuzungumza hapa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hao watumishi wa Afya hatujajiweka vizuri namna ya kuwalinda, namna ya wao kuwa na imani. Dawa hizi za mitishamba tunazokunywa ni ghali sana. Ni kati ya shilingi 30,000/= mpaka 50,000/=. Mwananchi wa kawaida hawezi. Je, haiwezekani Serikali ikachukua jukumu la kufanya utafiti angalau kwa dawa zetu? Siyo lazima sisi tuamini vitu vya watu wa ng’ambo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi naamini kabisa Tanzania tuna hazina kubwa ya dawa za asili. Tatizo letu ni namna ya kuzichambua ili tujue ni dawa gani zina mchango kwa wananchi wetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Jimbo langu la Mbulu Mji lina Hospitali ya Mji ambayo iko katikati. Ina vituo vya afya lakini hawana mashine hiyo ya oxygen, hawana mitungi na watu wanakufa. Wanapokufa kwa ugonjwa huu pengine wa kifua au kushindwa kuhema, mashine hizo zingeweza kuwasaidia. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, wiki iliyopita sikupata kuchangia, nilikuwa naenda Jimboni nazika, narudi; nafika hapa, narudi naenda kuzika; ifike mahali niseme wazi tu kwamba hali halisi ikoje. Kwa Mbulu, ukanda ule ni wa bonde la ufa. Juu ya bonde la ufa kuna baridi sana. Mwezi wa tatu, wa nne, wa tano, wa sita na wa saba, mafua haya yatakuja tu na watu watapata shida.

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MWENYEKITI: Ahsante sana Mheshimiwa Zacharia Issaay.

MHE. ZACHARIA P. ISSAAY: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa kunipa nafasi, lakini naomba mitungi hiyo ipelekwe katika Hospitali ya Mbulu na hospitali nyingine nchini na vituo vya afya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nampongeza sana Mheshimiwa Polepole, alisema, Corona ataishi Tanzania kwa adabu na sasa anaishi kwa adabu, lakini kwa kutegemea dawa zetu tulizonazo na mifumo yetu tuliyonayo na maombi yetu tunayoomba.

Mheshimiwa Mwenyekiti, rai yangu kwa Serikali, hospitali za wilaya, vituo vya afya, wapelekewe hiyo mitungi isaidie.

MWENYEKITI: Ahsante sanaMheshimiwa.

MHE. ZACHARIA P. ISSAAY: Mheshimiwa Mwenyekiti, umenionea, sijamaliza dakika kumi.

MWENYEKITI: Ni dakika tano tano.

MHE. ZACHARIA P. ISSAAY: Ni tano?

MWENYEKITI: Eeh, ni tano.

MHE. ZACHARIA P. ISSAAY: Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono Mpango uliokuwa umejadiliwa na wenzangu. Ila hili ombi langu lifanyiwe kazi kwa nchi nzima. Tunalo tatizo, tusifiche.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hili lipo tu, kwa heshima na taadhima nikwambie. Maana sisi tulioko huku tusifikiri siku moja hatutakuwa wananchi. Tutakuwa wananchi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana. Naunga mkono Mpango wetu ulioletwa kwa asilimia mia moja. (Makofi)