Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Mapendekezo ya Mpango wa Tatu wa Maendeleo wa Taifa kwa Miaka Mitano (2021/2022 – 2025/2026) na Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Mwaka 2021/2022 pamoja na Mapendekezo ya Muongozo wa Maandalizi ya Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka 2021/2022

Hon. Alexander Pastory Mnyeti

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Misungwi

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Mapendekezo ya Mpango wa Tatu wa Maendeleo wa Taifa kwa Miaka Mitano (2021/2022 – 2025/2026) na Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Mwaka 2021/2022 pamoja na Mapendekezo ya Muongozo wa Maandalizi ya Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka 2021/2022

MHE. ALEXANDER P. MNYETI: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nikushukuru sana kwa kunipa nafasi hii. Pia nitumie nafasi hii kuwashukuru Wanamisungwi kwa kunipitisha bila kupingwa na Madiwani wangu wote 27 na hatimaye sasa tupo humu kwa ajili ya kuwatumikia Wanamisungwi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mengi yamesemwa, mchango wangu nitajikita kwenye mambo matatu, jambo la kwanza ni kweli kwamba Taifa letu msingi wake mkubwa ni kilimo na kwa sababu hiyo tuna kila sababu ya kuelekeza nguvu kubwa kwenye kilimo tuwasaidie wakulima wetu hawa ili waweze kuleta tija kwenye Taifa letu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, yapo mashamba makubwa ambayo Serikali iliwapa wawekezaji ili wayaendeleze, lakini kwa masikitiko makubwa mashamba hayo mengi yametelekezwa na hao wawekezaji na hakuna kinachoendelea. Sasa niombe Wizara ya Ardhi, kama kuna namna yoyote ya kufanya mashamba hayo ama yarudi kwa wawekezaji wengine ama yarudi kwa wananchi ili wananchi waweze kuzalisha. Mashamba hayo wawekezaji unakuta mwekezaji mmoja anamiliki mashamba ekari 20,000, wengine ekari 50,000, wengine hivi, lakini ukiangalia uendelezaji wa mashamba hayo ni asilimia nne hadi 10, eneo lingine lililobaki lote liko wazi halilimwi na wananchi wanashangaa Serikali inashangaa na mwekezaji anashangaa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa kama kweli lengo letu ni kuzuia kuagiza vitu nje ya nchi, hebu basi tutengeneze mazingira ya kuzalisha hayo mashamba yafanye kazi ili basi tuongeze pato la Taifa kwa namna hiyo, vinginevyo tutaendelea kuagiza choroko, ngono, nyanya, vitunguu, kila kitu tunaagiza kutoka nje lakini mashamba tunayo hayafanyiwi kazi. Ukienda kule Bassutu kuna mashamba ngano, tunasema tunaagiza ngano, wakati mashamba tunayo lakini hakuna anayeyalima. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama kweli tuko serious na hii mipango, otherwise mipango ya kwenye karatasi kama kweli tunataka tutoke hapa tulipo, yako mambo makubwa ambayo tunatakiwa tuchukue hatua ili basi tuweze kutoka hapa tulipokwama. Mashamba yametekelezwa, nenda Lotiana mashamba makubwa yametekelezwa. Leo Tanzania bado tunaagiza nyama kutoka nje ya nchi. Hii mipango, ni kweli ni mipango mizuri lakini utekelezaji wake mbona tunakwama, mashamba yametekelezwa, hatuendi kwenye kugota kwenye pointi ya kwamba tunatokaje kwenye hili tatizo lililokwamisha, haya makaratasi ni mazuri kwa sababu yameandikwa na Professors, ma-PhD holder lakini utekelezaji wake. Nazungumza utekelezaji wa namna gani tunakwama hapo tulipokwamia. Kwa hiyo, naomba hili niishauri sana Serikali kama kweli tuko serious hebu mtoke hapa tulipokwama. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la pili, tumeanzisha viwanda vingi sana kwenye Taifa letu kwa muda mfupi, hongera sana Serikali kwa kazi hii nzuri. Hata hivyo, nasikitika kukujulisha kwamba viwanda hivi baada ya muda vitakufa vyote, kwa sababu hatuna malighafi yakuendesha hivyo viwanda, tunazalisha wapi? Unaniambia tunaanzisha viwanda ni kweli kule Iringa viwanda vya kuchakata mbao, lakini viwanda hivi miti iko wapi? Miti iko wapi, viwanda vinaanzishwa kule Misungwi, vinaanzishwa Kahama, vinaanzishwa wapi vya kuchakata pamba, pamba iko wapi? Tuwahamasishe wakulima wetu walime, tuwawezeshe pembejeo za kilimo walime. Hii Habari ya kumfurahisha mkuu wa nchi kwamba tunaanzisha viwanda, halafu baada ya miaka sita vimekufa, hii nataka niseme tutashindwa na tunashindwa very soon kwa sababu hatuwahamasishi wananchi kulima, hatuwatengenezei mazingira mazuri wananchi wetu waweze kulima, waweze kupatiwa pembejeo za kilimo, matrekta na kila kitu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tuna kiwanda chetu cha mbolea; leo mbolea tunanunua 60,000 mpaka 55,000 kwa mfuko wa kilo 25 mpaka 50. Sasa tuna Kiwanda chetu kule Minjingu, kiwanda peke kwenye Taifa letu, lakini Serikali ni kama wamekipuuza, bado wanaagiza mbolea nje ya nchi, inafika mbolea hapa kwa 50,000 mpaka 60,000, lakini kile kiwanda kipo, Serikali ikikiwezesha kidogo tunaweza tukanunua mbolea 20,000 mpaka 15,000 kwa sababu tuna uwezo wa kutengeneza mbolea yetu wenyewe kwenye Taifa letu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwisho nataka niwaambie….

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MWENYEKITI: Mheshimiwa kengele imeshagonga.

MHE. ALEXANDER P. MNYETI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. (Makofi)