Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Mapendekezo ya Mpango wa Tatu wa Maendeleo wa Taifa kwa Miaka Mitano (2021/2022 – 2025/2026) na Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Mwaka 2021/2022 pamoja na Mapendekezo ya Muongozo wa Maandalizi ya Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka 2021/2022

Hon. Edwin Enosy Swalle

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Lupembe

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

2

Ministries

nil

Mapendekezo ya Mpango wa Tatu wa Maendeleo wa Taifa kwa Miaka Mitano (2021/2022 – 2025/2026) na Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Mwaka 2021/2022 pamoja na Mapendekezo ya Muongozo wa Maandalizi ya Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka 2021/2022

MHE. EDWIN E. SWALLE: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi ili niweze kuchangia kwenye Mpango huu wa Miaka Mitano wa Serikali. Niende moja kwa moja kwenye Mpango ambao umewasilishwa na Serikali. Kwanza nipongeze sana Mheshimiwa Dkt. Mwigulu Nchemba kwa kuwasilisha Mpango huu kwa niaba ya Waziri wa Fedha, ameuwasilisha vizuri sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimesoma Mpango huu mzima Mpango wetu ni mzuri sana na umeweka vipaumbele vyote vizuri. Na ukisoma kwenye ukurasa wa 88 wa mapendekezo ya Mpango huu wa Miaka Mitano, Serikali imetamka wazi kwamba sekta ya kilimo itaendelea kuwa kitovu cha ukuzaji wa viwanda na maisha ya watu. Huu ni ukweli ambao Wabunge wote humu ndani tunaujua.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nina mchango ufuatao kuhusu sekta ya kilimo; wakati fulani ukitazama takwimu za Mpango wa Pili wa Maendeleo wa Nchi yetu, utakuta kwamba kwenye kilimo zilipelekwa fedha bilioni 188 tu. Sasa kama kilimo ndio kitovu cha kukuza viwanda, unaweza kuona ule msemo ambao alikuwa anasema Rais wetu wa Nne, kwamba zilongwa mbali, zitendwa mbali. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa nini nasema hivi? Ukitazama kwenye sekta ya kilimo, iko mipango mizuri imewekwa hapa kwamba Serikali itaboresha suala la utafiti mbegu bora, Maafisa Ugani na kadhalika. Naishauri Serikali kwa sababu maeneo mengi ya kilimo ambapo mazao ya kimkakati kama kahawa, chai, korosho, pamba na mazao mengine, haya maeneo hatuwezi kuweka kipaumbele cha kupeleka mbegu bora na wataalam na utafiti wakati miundombinu yake haiwezeshi kilimo kile kuwa na tija.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, naishauri Serikali kwenye maeneo ambayo kuna mazao ya kimkakati, Mpango huu ubainishe kwamba yatapewa kipaumbele cha miundombinu kama ya barabara, miundombinu ya umeme, miundombinu ya afya, ili kusudi kama unasema Jimbo la Lupembe kwa mfano lina zao la mkakati ambalo ni chai na eneo hili linalo viwanda, lakini wakati huo huo kwenye eneo hilo barabara hazipitiki, umeme hakuna, maji hakuna, Mpango huu hauwezi kufanikiwa. Ushauri wangu ulikuwa ni huo kwamba Mpango huu uendane na maeneo ya vipaumbele ili kusudi uakisi uhalisia wa mpango wenye.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sehemu ya pili ambayo napenda kuchangia kwa ufupi, lipo jambo limesemwa na Wabunge wengi humu ndani, Wabunge wengi tumetoa maoni kwamba Serikali haina fedha na Wabunge wamependekeza njia mbalimbali za kupata fedha. Nataka niseme eneo lingine ambalo wengi hatujalisema shida yetu kwenye utekelezaji wa hii Mipango ya Serikali kwa maoni yangu siyo fedha tu, lipo tatizo lingine la kutofanya maamuzi kwa wakati kwa watu wenye mamlaka ya kufanya maamuzi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni wazi kwa mfano, yuko Mbunge mwenzangu wa Njombe Mjini amezungumza hapa, kwa mfano yupo mwekezaji wa zao la chai ambaye yeye anashindwa kuendesha kiwanda kwa sababu tu watu wa Hazina wanashindwa kufanya maamuzi wa jinsi yeye aweze kusamehewa kodi na kuendesha biashara yake ya viwanda.

Mheshimiwa Mwenyekiti, yapo maeneo pia mengine, mfano eneo kama la Kilolo, kuna mashamba ya chai yametelekezwa ni mapori, kwa sababu tu maamuzi hayajafanyika ni nani akawekeze maeneo haya. Kwa hiyo, naomba sana watu wa Serikali wafanye maamuzi, decision making ni kipaumbele muhimu sana kwa utekelezaji wa Mpango huu wa Serikali.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. (Makofi)