Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Mapendekezo ya Mpango wa Tatu wa Maendeleo wa Taifa kwa Miaka Mitano (2021/2022 – 2025/2026) na Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Mwaka 2021/2022 pamoja na Mapendekezo ya Muongozo wa Maandalizi ya Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka 2021/2022

Hon. Nicodemas Henry Maganga

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mbogwe

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Mapendekezo ya Mpango wa Tatu wa Maendeleo wa Taifa kwa Miaka Mitano (2021/2022 – 2025/2026) na Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Mwaka 2021/2022 pamoja na Mapendekezo ya Muongozo wa Maandalizi ya Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka 2021/2022

MHE. NICODEMUS H. MAGANGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru. Awali ya yote, naomba nimshukuru Mwenyezi Mungu kwa mara ya pili nimesimama mbele ya Bunge hili Tukufu kutumia nafasi hii kuishauri Serikali.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kwanza nitumie neno ku-declare interest, mambo yote toka tumeanza kujadili Mpango binafsi nimeuelewa vizuri sana. Niwaombe tu Wabunge wenzangu wote ni vyema tumtangulize Mungu tunapokuwa tunaishauri Serikali tusiishie tu kulalamika sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, muda ni mdogo sana, naomba niende moja kwa moja kwenye hoja, mimi ni mkulima, mfanyabiashara pia ni mwanasiasa, naomba kwenye upande wa kilimo niishauri Serikali, ni vyema sasa wakulima tupatiwe vifaa vya kilimo kama matrekta, mimi natokea Wilaya ya wakulima pale Mbogwe.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini vilevile kwenye upande wa biashara, wafanyabiashara tumekuwa na kilio kikubwa kwenye hili taifa la Tanzania. Mimi nilikuwa miongoni mwa wafanyabiashara East Africa Community lakini Watanzania tumefeli kufanya biashara na mataifa mengine. Kwa maana hiyo hii ajenda ni vyema Serikali iichukue kwa mapana na marefu sana, tumeshindwa yaani kila kona tumefeli, masoko yote sisi tunaonekana tuko chini. Chanzo kikubwa kabisa ni haya mabenki yetu ya ndani. Benki za hapa Tanzania riba zake ziko juu sana, ni tofauti na mabenki mengine.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunapoongelea suala la uchumi lina mapana na marefu sana. Mimi somo langu lilikuwa ni moja tu shuleni, ni uchumi peke yake. Kwa hiyo, tunapokuwa tunaongelea neno uchumi, kwanza uchumi umelenga sana sana kwenye mafuta, mimi nauza mafuta ya petrol na diesel, tukiangalia vizuri Serikali kwenye upande wa mafuta na tukiangalia mataifa mengine yanayotuzunguka bei ya mafuta ni ya chini sana. Kwa maana hiyo Serikali ikitibu kwenye tozo hizo za mafuta zikiwemo faini za EWURA milioni 20 kila kosa moja, tutasonga mbele sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sisi Geita ni wachimbaji, kwa kuwa Serikali inatuhakikishia kwamba imekusanya vya kutosha watupe vifaa vya kuchimbia. Sisi tuna elimu kubwa ya uchimbaji ila hatuna capital. Serikali ikituwezesha ikatupa vifaa vya kuchimba wenyewe na sisi tutaishi kwa raha na amani kwenye nchi yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, upande mwingine ni elimu, kuna dada yangu pale alizungumza point sana, naomba nimuunge mkono, elimu yetu ya Kitanzania inamuandaa mtu kuwa maskini, tunaandaliwa kuwa waajiriwa. Leo Wabunge wote humu tukiangaliana mfukoni tumetumwa na watu wetu kuja kuwatafutia ajira. Kwa maoni yangu ninavyoona kabisa ajira karibia zote zimejaa, kwa hiyo, ni vema walimu wawe wakweli kuanzia kule shuleni. Nimpongeze Waziri wa Elimu kuna siku moja alitangaza kwamba atapima uelewa maana suala la vyeti walikagua watumishi wote ila kwenye uelewa hapo na mimi bado nafikiria sijui atatumia taaluma ipi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine kubwa kabisa linalotufanya kurudi nyuma kwenye hili Taifa letu la Tanzania ni kule kutokujituma katika kazi. Niwaombe Waheshimiwa Wabunge wenzangu pamoja na ndugu zangu wote mnaonisikia, tunao ugonjwa Tanzania hapa wa kutokufanya kazi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Rais wetu amekuwa ni jemedari mkuu akituhamasisha tufanye kazi. Tatizo kubwa sisi ni wepesi wa kuridhika, tukipata tu hizi posho kidogo na mishahara hii ya Kibunge tunaziacha kazi za msingi za kuweza kutuingizia maarifa na kutuzalishia mali nyingi. Kwa hiyo, niwaombe Wabunge wenzangu sisi ni vyema tukawe kielelezo kwenye jamii tukafanye kazi hata hivi viwanda tunavyovisema na kilimo tukaanze sisi Wabunge kulima ili Taifa letu liweze kupata manufaa. Hata maandiko yanasema sisi viongozi ni barua tunasomwa na watu wote. Kwa maana hiyo tukifanya vizuri kanzia sisi Wabunge na wale tunaowaongoza watatufuata.

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MWENYEKITI: Ahsante sana Mheshimiwa, kengele imegonga.

MHE. NICODEMUS H. MAGANGA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana, ila muda haujatosha, nitaleta mchango wangu kwa maandishi, ahsante sana. (Makofi)