Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Mapendekezo ya Mpango wa Tatu wa Maendeleo wa Taifa kwa Miaka Mitano (2021/2022 – 2025/2026) na Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Mwaka 2021/2022 pamoja na Mapendekezo ya Muongozo wa Maandalizi ya Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka 2021/2022

Hon. Janeth Elias Mahawanga

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Mapendekezo ya Mpango wa Tatu wa Maendeleo wa Taifa kwa Miaka Mitano (2021/2022 – 2025/2026) na Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Mwaka 2021/2022 pamoja na Mapendekezo ya Muongozo wa Maandalizi ya Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka 2021/2022

MHE. JANETH E. MAHAWANGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Nichukue nafasi hii kumshukuru Mwenyezi Mungu, Chama changu ha Mapinduzi, kina mama wa Mkoa wa Dar es Salaam na familia yangu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa nichangie Mapendekezo ya Mpango wa Tatu wa Miaka Mitano na Mwaka Mmoja. Katika kuongeza kipato cha Serikali na kuwawezesha wananchi kiuchumi kupitia ile Mifuko 18 ambayo iko chini ya Ofisi ya Waziri Mkuu, napendekeza ishirikiane kwa karibu na Wizara ya TAMISEMI pamoja na Halmashauri zetu. Pia iongeze wigo kwa kuhusisha Madiwani nao kwenye Mpango huu ili itengeneze mfumo mzuri wa ukusanyaji wa hizi pesa pindi wajasiriamali hawa wanapopata hiyo fursa kwani fedha nyingi zinatoka kwenye vikundi lakini pia hazirudi. Kwa hiyo, tatizo kubwa hapa ni mfumo wa ukusanyaji wa hizi hela. Watakapohusishwa pia Madiwani katika utaratibu huu itasaidia kwani vikundi vingi kwenye kata zetu Madiwani ndiyo watu sahihi na wanavijua zaidi vikundi itasaidia ufuatiliaji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile katika kutoa fursa hizi, Serikali iangalie zaidi kwenye kutoa elimu kwa wajasiriamali hawa kwa sababu fursa zipo, mikopo inatoka lakini wananchi wengi wanakwama kutokana na ukosefu wa elimu. Elimu hizi zikajikite katika kukuza ujuzi wa kuongeza thamani za bidhaa zao, upatikanaji wa mitaji, utafiti wa masoko na kuzitambua fursa zinazowazunguka. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na haya naomba niongelee usajili wa vikundi. Sheria ya Fedha imetoa mamlaka kwa Benki Kuu ya Tanzania (BoT) kukasimu shughuli zote za usajili, usimamizi na ufuatiliaji wa vikundi vya kifedha. Makundi haya ya kifedha yamegawanywa katika sehemu nne, kuna mabenki na microfinance ambazo zinapata miongozo moja kwa moja kutoka BoT, kuna SACCOS ambazo zinapata miongozo katika Vyama Ushirika na kuna vikundi vya kina mama ambavyo ni VICOBA wao wanapata miongozo kutoka TAMISEMI. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Benki Kuu ilitoa muda wa mwaka mmoja vikundi yyote viwe vimesajiliwa kupitia sheria mpya. Ule muda uliisha, akina mama walikuwa wako tayari kusajili lakini miongozo kutoka TAMISEMI ilikuwa haijashuka huku chini. Iliongezwa muda wa miezi sita ambao unaisha mwezi Aprili mwaka huu, lakini mpaka sasa bado akina mama wakienda kwenye Halmashauri wanakuta bado hakuna utaratibu wowote ambao umetoka TAMISEMI unaowataka wao wasajili.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hii imeleta hofu kubwa kwenye vikundi vya kina mama kwani kuna vikundi ambavyo vimesimama kufanya shughuli zake za ujasiriamali na kuna vingine vinafanya kwa uwoga vikiwa vinasubiri kuangalia miongozo hii ya usajili mpya inataka nini na inasemaje. Kwa hiyo, niiombe Wizara ya TAMISEMI, ijitahidi kutoa miongozo hii basi ili kina mama wafanye huo usajili kwa kutumia hii Sheria mpya ya Fedha. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile Serikali iangalie baadhi ya kero kuzifanya kama vyanzo vya mapato yaani fursa. Kwa mfano, Mkoa wa Dar es Salaam kuna kero kubwa sana ya takataka, Wizara ya Viwanda na Uwekezaji ni wakati sasa wa kuangalia ni jinsi gani kiwanda cha kuchakata taka kinaweza kupatikana kwani zaidi ya kuongeza kipato kwenye nchi yetu itaongeza ajira pamoja na kumaliza hili tatizo la taka, tutapata mbolea na gesi na Serikali itapata pato lake. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niende kwenye ushauri, nashauri Serikali irejeshe mifumo ya kuzisaidia na kuchochea benki nchini yaani credit guarantee schemes ambazo zitasaidia wawekezaji kulipa kodi na Serikali itapata pato pia. Vilevile yafanyike marekebisho ya kodi inayohusu ufutaji wa madeni ambayo hayalipiki yaani bad debts write-off iendane na sera, kanuni na Sheria ya Benki Kuu ili kuweka mazingira ya biashara yanayotabirika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia Serikali iwe inatoa muda wa kutosha inapofanya marekebisho ya sera zake mbalimbali ili kutoa muda wa wadau kujipanga kutokana na mabadiliko ya sera zinapokuwa zinafanyiwa marekebisho. Pia Serikali iweke mazingira mazuri ya kufanya mabenki binafsi kuachana na sera ya kuanzisha benki ambazo zinakuja kuwa mzigo na hazina tija kwenye Taifa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwisho niombe mamlaka ya kukusanya kodi irekebishe Tax Administration Regulation kwa kuondoa utaratibu wa sasa wa kutumia Urgent Notice kutoka kwenye mabenki moja kwa moja badala yake iweke utaratibu wa kukubaliana na walipa kodi kulipa kodi kwa muda rafiki. Hii itasaidia sana kwani wafanyabiashara wengi wataweza kuweka hela benki, watakuwa na imani na kuondoa ile hofu kwamba benki siyo sehemu salama sasa hivi ya kuweka hela.

Mheshimiwa Mwenyekiti, wakiweka taratibu hizi wafanyabiashara, wajasiriamali wengi watakuwa na imani, itaongeza hamasa, watu wataweka fedha benki, ukizingatia hata Mheshimiwa Rais wakati anahutubia Bunge la Kumi na Mbili alisisitiza kuwa watu wahimizwe kuweka hela benki ili kusaidia benki zetu zifanye biashara na mzunguko uwe imara.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante, naunga mkono hoja. (Makofi)