Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Mapendekezo ya Mpango wa Tatu wa Maendeleo wa Taifa kwa Miaka Mitano (2021/2022 – 2025/2026) na Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Mwaka 2021/2022 pamoja na Mapendekezo ya Muongozo wa Maandalizi ya Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka 2021/2022

Hon. Dr. Stephen Lemomo Kiruswa Mamasita

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Longido

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Mapendekezo ya Mpango wa Tatu wa Maendeleo wa Taifa kwa Miaka Mitano (2021/2022 – 2025/2026) na Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Mwaka 2021/2022 pamoja na Mapendekezo ya Muongozo wa Maandalizi ya Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka 2021/2022

MHE. DKT. STEVEN L. KIRUSWA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa fursa ili niweze kuchangia kwenye huu Mpango wetu wa Tatu wa Maendeleo wa Taifa wa Miaka Mitano pamoja na Mpango wa mwaka wa fedha unaokuja.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nilijipanga kuchangia katika maeneo yaliyotamkwa na kuelezewa kwa kina kwenye Mpango katika sekta za kilimo, mifugo, maji na madini, lakini kwa kutambua ufinyu wa muda nitaomba nichangie maeneo mengine kwa maandishi ila nijikite katika hoja inayohusu sekta ya mifugo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na kwamba Mpango umeweka bayana mikakati sahihi na safi kabisa ya kuijenga sekta ya mifugo kwa kuhakikisha kwamba maeneo ya malisho yanaongezwa, upatikanaji wa maji, upatikanaji wa madawa ya tiba na chanjo na maendeleo mengine ya miundombinu ya mifugo, lakini kuna changamoto nyingine moja kubwa ambayo bado tunakabiliwa nayo kama Taifa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, changamoto kubwa ni kwenye upande wa masoko; hali halisi ilivyo sasa hivi kwa wafanyabiashara wa mifugo katika nchi yetu ni kwamba hakuna masoko yenye tija ya ndani wala nje. Naomba nichukue mfano na naipongeza sana Serikali yetu kwa kutengeneza mazingira safi ya wawekezaji kwenye sekta ya bidhaa za mifugo kuja kuwekeza nchini na azma kubwa iliyojitokeza ya ujenzi wa viwanda mbalimbali vya mazao ya mifugo nichukue mfano wa kiwanda kikubwa kilichojengwa katika Wilaya yangu ya Longido Kiwanda cha Elia Foods Oversees Limited. Kiwanda kile kimejengwa kwa gharama kubwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kiwanda kile kimejengwa kwa gharama kubwa, kina uwezo wa kuchinja mpaka ng’ombe 500 kwa siku na mbuzi pamoja na kondoo 4,000 kwa siku. Baada ya mwekezaji kumaliza kujenga kiwanda kile na akaanza uzalishaji mwezi wa 11 akakutana na changamoto kubwa ambayo hata sisi kama wafugaji na wafanyabiashara wa mifugo tumeona kwamba itakuwa ni kikwazo kikubwa kwa ufanisi wa viwanda vinavyojengwa katika sekta ya mifugo katika nchi hii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna utitiri wa kodi ambazo bahati nzuri Mheshimiwa Kingu alishatolea ufafanuzi juzi akatoa ulinganifu mzuri kabisa wa jinsi Tanzania tunavyofanya vibaya kwa kuwekeza tozo mbalimbali katika viwanda vyetu kiasi cha kufanya vile viwanda ili viweze kuwa endelevu. Kuna zaidi ya tozo 11 lakini ukiangalia madhara anayopata mwekezaji ya kutoona namna nyingine ya kutengeneza faida, anayahamishia kwa muuzaji ambaye sasa ni mfanyabiashara wa mifugo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mfano, katika hiki kiwanda cha mfano tu ambacho nimekitaja cha Longido, mwekezaji huyu amepanga bei ya kununua mbuzi Sh.6,500 kwa kilo na wafugaji ambao wamekuwa wakitegemea soko la nchi ya jirani hawaoni tija kwa sababu hata kama wakilipia ushuru wa Serikali wakifisha mbuzi zao Kenya wanauza kilo kwa Sh.8,500. Kwa hiyo, kwa ajili ya kodi zilizoko maana nilishafanya kikao kati ya wafanyabiashara wa mifugo wa wilaya yangu na Tanzania kwa ujumla wanaotumia soko la Namanga na mwekezaji tukatafuta chimbuko la shida iko wapi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwekezaji akatupa changamoto zake akasema kuna hizi regulatory fees ndiyo zinafanya yeye asiweze ku-compete na masoko ya nchi jirani na asiweze kutoa bei yenye tija. Yeye kila akichinja na kuweka consignment moja akifisha bandarini asilimia moja ya thamani ya ile consignment inachukuliwa na Meat Board. Mwekezaji huyu anapopeleka bidhaa yake sasa kuuza sokoni, Wizara inachukua Sh.50 kwa kila mbuzi na kondoo kwa kilo na Sh.100 kwa ng’ombe. Mfanyabishara huyuhuyu mwenye kiwanda anachajiwa na BAKWATA kwa ajili ya kukagua nyama shilingi milioni 2 kwa mwaka ambayo sasa hivi wanabishania nao wawe wanalipwa kwa kila kilo ya nyama wanayosafirisha kwenda kuuza kwenye masoko.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, akajikuta kwamba hakuna namna anaweza akaongeza bei kwenye bidhaa na yeye akaweza kukiendesha kiwanda kile. Kwa sababu hiyo basi tukajikuta ile adhima iliyotamkwa kwenye Mpango ya kuendesha uchumi wa viwanda na shindani hatuko anywhere karibu na kufanikiwa kwa kuwa washindani katika biashara ya bidhaa mbalimbali zinazotengenezwa na viwanda vya hapa nchini kwetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, napenda kuishauri Serikali ili tutoke na wafugaji wetu wasiwe na sababu ya kupeleka mifugo Kenya tukapoteza bidhaa mbalimbali inayotokana na mifugo, ni vizuri sasa kodi hizi ama zifutwe au zifanyiwe marekebisho ili ziweze kutoa tija kwa wafugaji wetu na mwekezaji naye aone kwamba kiwanda chake kinamuletea faida na aweze kukiendeleza.

Pia kama kuna uwezekano kuwe na tax holiday ya mpaka mwaka mmoja maana huyu mwekezaji alisema kwamba mkinipunguzia kodi nitatoa bei shindanishi na ya Kenya ili ateke soko wale wafugaji wote wanaopeleka mifugo Kenya walete bidhaa pale pale Longido wauze kwenye kiwanda chetu na ajira ziongeze na faida zingine tunazopata kwa sababu kiwanda kile kinatumia kila kitu mfano kwato, pembe, mifupa na mbolea zinatoka finished product ambazo zinaendelea kuingia sokoni. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwekezaji huyu akasema kwamba kama Serikali ikimuondolea kodi yuko tayari kushindana. Kwa hiyo, naomba Serikali iangalie suala la kupunguza kodi katika bidhaa mbalimbali zinazozalishwa na viwanda vyetu vya ndani ili tuweze kujenga huo uchumi na biashara shindani.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa yale mengine ambayo nilitamani kuchangia, nitawasilisha kwa maandishi na naunga mkono hoja kwa asilimia mia moja. (Makofi)