Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Mapendekezo ya Mpango wa Tatu wa Maendeleo wa Taifa kwa Miaka Mitano (2021/2022 – 2025/2026) na Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Mwaka 2021/2022 pamoja na Mapendekezo ya Muongozo wa Maandalizi ya Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka 2021/2022

Hon. Khalifa Mohammed Issa

Sex

Male

Party

ACT

Constituent

Mtambwe

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

2

Ministries

nil

Mapendekezo ya Mpango wa Tatu wa Maendeleo wa Taifa kwa Miaka Mitano (2021/2022 – 2025/2026) na Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Mwaka 2021/2022 pamoja na Mapendekezo ya Muongozo wa Maandalizi ya Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka 2021/2022

MHE. KHALIFA MOHAMED ISSA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. Awali ya yote, nimshukuru Mwenyezi Mungu Mtukufu, Mwingi wa Rehema mwenye kurehemu, ambaye ametujalia kuwepo katika nyumba hii Tukufu. Pia nikushukuru wewe kunipa nafasi hii ya kuchangia huu Mpango ambao uko mbele yetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi nataka nijikite sana katika Mpango huu hususan niende katika Wizara yetu mama ambayo iko katika Ofisi ya Makamu wa Rais ambayo ni ya Muungano pamoja na Mazingira. Kama tunavyojua Tanzania ni pamoja na Zanzibar, bila Zanzibar hakuna Tanzania. Sote sisi ni waumini wa Muungano na mimi ni muumini wa Muungano wa haki na wa usawa. Kwa hivyo, napenda Muungano huu udumu katika mfumo huo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa basi jambo ambalo tuna shida kule katika visiwa ni kuhusu mabadiliko ya tabianchi. Mabadiliko ya tabianchi yametukumba sana katika Visiwa vyetu vya Unguja na Pemba na visiwa vidogovidogo ambavyo vimeizunguka Zanzibar. Wizara inayohusika nahisi kwa upande wangu haijafanya vya kutosha, leo ukiangalia visiwa vinavamiwa na maji ya bahari.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikitoa mfano kuna visiwa vidogovidogo kama Kisiwa Panza, Pemba kuna Kisiwa kinaitwa Kisiwa Panza. Kisiwa kile kimevamiwa mpaka sehemu ya kuzikia makaburi yamezolewa na maji, wakati mwingine unaweza ukaenda ukakutana na mafuvu ya vichwa ya maiti. Kadhalika kuna Kisiwa cha Mtambwe Mkuu, Mtambwe Mkuu ni katika jimbo langu ambacho ni kisiwa cha historia kilichokaliwa na Wareno katika karne ya 18 ambacho kinatishia amani, wananchi wake wanakaribia kuhama kwa sababu maji ya bahari yamevamia kisiwa kile.

Mheshimiwa Mwenyekiti, viko visiwa vingine vingi kwa mfano Misali ni kisiwa vilevile cha utalii, lakini nacho kimevamiwa na maji, lakini bado Serikali kupitia ofisi yetu hii haina jitihada yoyote ya makusudi ambayo inaifanya na mpango endelevu kuweza kushughulika na mambo haya ili kukinga maji yale yasiweze kuvamia makazi ya watu. Kwa hivyo, hofu yangu baada ya karne si nyingi zinazokuja tunaweza tukavipoteza visiwa hivi, kwa hivyo, yale matamanio na utashi tuliokuwanao wa kuwa na Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ikaondoka kwa sababu visiwa vile vimeondoka.

Mheshimiwa Mwenyekiti, huo ni mfano ambao uko hai kabisa. Sisi wazee wetu ambao wameishi katika miaka sitini, sabini siku za nyuma wanatueleza tunapita katika bahari ya kina sasa hivi lakini miaka sitini iliyopita ilikuwa watu ni mashamba wakilima mipunga katika maeneo yale, lakini kwa sababu hakuna jitihada maalum kwa hivyo, bahari inapanda juu kila uchao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, naiomba Ofisi, Wizara kattika Ofisi ya Makamu wa Rais kwa makusudi kabisa ifanye bidii tuje tuvitembelee visiwa. Awamu iliyopita ya Bunge tulifanya jitihada kubwa kuonana na Mawaziri lakini haikuwezekana, hawakupata nafasi ya kuja kuvikagua na kuweza kupata ufumbuzi. Kwa hivyo, huo ni msisitizo wangu mkubwa ambao napenda kuutoa kwenye Mpango huu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, athari hii kwa kweli inaanza kuonekana. Hata hizi mvua ambazo hazina misimu, unakuta mvua zinanyesha wakati mwingine, mafuriko yanatokea wakati wa kiangazi, lakini wakati wa msimu wa mvua yenyewe mvua haipatikani. Ndio maana wakati mwingine tunapata hii collusion katika nchi yetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la pili ambalo nilitaka niliseme kwa ufupi ni kuhusu huu Mfuko wa Kunusuru Kaya Masikini ambao unajulikana kwa TASAF. Mfuko huo kwa kiasi kikubwa nikiri umeleta manufaa makubwa katika kaya zile ambazo ni masikini. Familia zile za kaya masikini zimemudu kuwapeleka watoto wao shule, kupata uniform, kupata chakula, kupata ada za shule na wakati mwingine kupata pesa za matibabu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hivyo, ni jambo zuri, lakini tatizo linakuja, uteuzi wa hawa wanufaika unakuwaje? Wakati mwingine unaweza kuona watu ambao wanastahiki hasa kuingizwa katika mpango huu wameachwa, lakini wale ambao wana uwezo kidogo ndiyo ambao wamechukuliwa. Hii inatokea wakati mwingine utashi wa viongozi wa Shehia, kama mnaendana pamoja na kiongozi wa Shehia, Sheha, basi anaweza kukuingiza katika listi.

T A A R I F A

MHE. OMAR ISSA KOMBO: Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa.

MHE. KHALIFA MOHAMED ISSA: Mheshimiwa Mwenyekiti, niendelee kusema kwamba…

MWENYEKITI: Mheshimiwa Khalifa kuna Taarifa.

MHE. OMAR ISSA KOMBO: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nimpe Taarifa mzungumzaji…

MWENYEKITI: Jitambulishe tafadhali.

MHE. OMAR ISSA KOMBO: Mheshimiwa Mwenyekiti, jina naitwa Omar Issa Kombo, Mbunge wa Jimbo la Wingwi, Pemba.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nimpe Taarifa mzungumzaji kuhusu utaratibu unaotumika kuwapata wanufaika wa kaya maskini kule Pemba. Kunafanyika kikao cha jamii ambapo wanajamii hawa wanachagua watu wa kuratibu na kuorodhesha wanufaika wa kaya masikini ambao wanaitwa CMC si Sheha.

WABUNGE FULANI: Aaaaa.

MHE. OMAR ISSA KOMBO: Sheha hashiki daftari kuandika wanufaika wa kaya masikini, ni wananchi wenyewe ndiyo wanaoandika kupitia wajumbe wanaowachagua wao wenyewe ambao wanaitwa CMC, asipotoshe umma. Ahsante. (Makofi)

MWENYEKITI: Mheshimiwa Khalifa, unaipokea Taarifa hiyo?

MHE. KHALIFA MOHAMED ISSA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nafikiri tuendelee, asiyejua maana haambiwi maana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niendelee kusema kuwa upande wa pili miradi hii, hasa ule mradi wa kutoa ajira ya muda, tatizo lililopo pia ni ule uteuzi wa ile miradi. Wakati mwingine miradi inateuliwa au inawekwa lakini haiangaliwi sustainability yake, nini uendelevu wake na nini tija yake mwisho? Kwa hivyo, unaweza kuanzisha mradi lakini baadaye ukawa haukufika mwisho, tija yake inakosekana. Pia wakati mwingi mradi ule unakosa ile value for money. Utakuta mradi umefanywa lakini value for money haipo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mfano, mimi kuna mradi wa tuta la kuzuia maji ya bahari ambao umefanywa katika kipindi fulani, ukiangalia umechukua muda mrefu, lakini tija yake haikuonekana kwa sababu leo tuta lile limevurugika, maji yanaendelea kuingia katika mashamba ya watu kwa hivyo, ile sustainability inakosekana. Hata ukiangalia tuta lile labda lingejengwa na watu kwa kulipwa shilingi milioni mbili, milioni tatu, lakini limegharimu zaidi ya shilingi milioni 10, lakini tija yake haikupatikana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini kubwa zaidi tunasikitika Wabunge katika maeneo ya miradi hatushirikishwi. Mimi kipindi kile nilikuwepo, mradi huo uko karibu tu, umo katika kata au shehia yangu, lakini mimi sikushirikishwa vyovyote ili kuweza kutoa ushauri wangu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwisho kabisa, yangu ni hayo niliyosema kwa ufupi, ahsante sana. (Makofi)