Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Mapendekezo ya Mpango wa Tatu wa Maendeleo wa Taifa kwa Miaka Mitano (2021/2022 – 2025/2026) na Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Mwaka 2021/2022 pamoja na Mapendekezo ya Muongozo wa Maandalizi ya Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka 2021/2022

Hon. Abdallah Dadi Chikota

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Nanyamba

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Mapendekezo ya Mpango wa Tatu wa Maendeleo wa Taifa kwa Miaka Mitano (2021/2022 – 2025/2026) na Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Mwaka 2021/2022 pamoja na Mapendekezo ya Muongozo wa Maandalizi ya Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka 2021/2022

MHE. ABDALLAH D. CHIKOTA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi na mimi nitoe mchango wangu kuhusu hoja ambazo zipo Mezani. Kabla sijaanza kuchangia, nitumie nafasi hii, kwa moyo wa dhati, kuipongeza Serikali yangu ya Awamu ya Tano kwa kazi nzuri ambayo imeifanya katika utekelezaji wa Mpango wa Pili wa Maendeleo wa nchi yetu. Kwa kweli kazi kubwa imefanyika, miradi mingi imetengenezwa, mingi tumeiona katika maeneo yetu. Changamoto iliyopo kwa pale ambapo haikutekelezwa ndiyo taratibu za mipango. Imeingizwa kwenye Mpango huu wa Tatu ili itafutiwe fedha iendelee kutekelezwa. Kwa hiyo naipongeza sana Serikali ya Awamu ya Tano.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mchango wangu unajikita katika maeneo mawili. Sehemu ya kwanza ni sehemu ya kilimo na hapa nitashauri namna gani ya kupata fedha ili tuendelee kutengeneza miradi mingine na itahusu kuongeza thamani kwenye mazao ya biashara na hususan zao la korosho.

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la ubanguaji ndiyo njia pekee ya kuhakikisha kwamba korosho yetu inapata bei nzuri kwenye soko la dunia. Kubangua korosho ni mkakati ambao tulishauanza hapo nyuma. Lengo la kuweka export levy ilikuwa ni kuwazuia wanunuzi wasisafirishe korosho ghafi, lakini mpango huo naona kama una dosari.

Mheshimiwa Mwenyekiti, uwezo wetu wa kubangua korosho kwa viwanda tulivyonavyo ni kama tani 70,000 na sasa hivi tunazalisha mpaka tani 220,000. Kwa hiyo korosho nyingi tunaziuza zikiwa ghafi. Nashauri kwamba tukose fedha kidogo leo ili tupate fedha nyingi baadaye na hii itawezekana kwa kufanya nini?

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza tuondoe tozo na kodi zilizopo wakati wa uingizaji wa mashine za kubangua korosho. Wawekezaji wanalalamika kwamba kodi ni kubwa kwa hiyo tuondoe hizo kodi ili mashine nyingi ziweze kuingizwa. Pili, nashauri, tuweke vivutio maalum kwa wawekezaji wapya wa viwanda vya korosho. Ushauri wangu wa tatu, tuondoe kodi na tozo kwenye vifungashio. Wale ambao wana viwanda sasa hivi wanalalamika kwamba vifungashio vina kodi kubwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tukifanya hivyo faida yake hapa ni nini? Faida ya kwanza ni kwamba tutapunguza gharama za uwekezaji, kwa hiyo tutapata wawekezaji wengi; Pili, tutawapata wawekezaji wa ndani badala ya kuwategemea wawekezaji wa nje tu; na tatu, tutapata wawekezaji au wabanguaji wadogo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kiwanda kidogo cha korosho unaweza ukatumia mtaji wa milioni 60. Kwa hiyo kwa sababu sasa hivi korosho inalimwa na zaidi ya mikoa 12, tunaweza tukatumia halmashauri zetu badala ya kutoa zile fedha za Mfuko wa Vijana kwa vijana mmoja mmoja, tunaweza tukaamua waanzishe viwanda vidogo vidogo vya kubangua korosho. Hapo tutaongeza ajira kwa vijana wetu, tutaongeza ajira kwa wanawake na utakuta thamani ya fedha ile tutakuwa tunaiona. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, wenzetu wa Vietnam na India wanatumia sana korosho yetu kuongeza ajira kwao. Mipango hii wakiisikia wenzetu watakuwa na hofu sana kwa sababu korosho ghafi hazitakwenda kwao. Kwa hiyo muda ni sasa tuwekeze katika ubanguaji ili tuongeze ajira. Naona kabisa tukiwekeza kwenye korosho hizi ajira milioni nane ambazo tumeahidi kwenye Ilani ya chama chetu karibu robo yake zitatoka kwenye viwanda vya kubangua korosho. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hoja yangu ya pili, niungane na Mheshimiwa Hokororo kuhusu Mradi wa Makaa ya Mawe Mchuchuma na ule wa Chuma Liganga. Ukiangalia Mipango yetu yote mitatu ile inaendelea kutajwa. Wakati umefika sasa tuweke fedha za kutosha ili miradi hii iende kutekelezwa. Mradi huu unakwenda sambamba na ujenzi wa reli kutoka Mtwara – Mbambabay na ile pacha ya Mchuchuma na Liganga. Tuwekeze katika miradi hii sasa ili tuweze kupata fedha za kutosha. Tukiwekeza kwenye reli hii ya Kusini basi Bandari ya Mtwara itatumika ipasavyo na siyo kama malalamiko yaliyopo sasa hivi kwamba inategemea zao la korosho, tutasafirisha tumbaku kutoka kwa wenzetu Songea lakini Malawi, Zambia na DRC Kongo wanatumia bandari yetu na hivyo tutapata kodi nyingi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana na naunga mkono hoja. (Makofi)