Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Mapendekezo ya Mpango wa Tatu wa Maendeleo wa Taifa kwa Miaka Mitano (2021/2022 – 2025/2026) na Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Mwaka 2021/2022 pamoja na Mapendekezo ya Muongozo wa Maandalizi ya Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka 2021/2022

Hon. Dr. Paulina Daniel Nahato

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Mapendekezo ya Mpango wa Tatu wa Maendeleo wa Taifa kwa Miaka Mitano (2021/2022 – 2025/2026) na Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Mwaka 2021/2022 pamoja na Mapendekezo ya Muongozo wa Maandalizi ya Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka 2021/2022

MHE. DKT. PAULINA D. NAHATO: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi hii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukitizama katika Dira ya Maendeleo ya 2025 pamoja na masuala mengi ambayo yameongelewa tunazungumzia juu ya elimu bora kwa wasomi wetu wa vyuo vikuu ili tuweze kupata Taifa bora lakini sasa katika elimu hiyo ya vyuo vikuu tunaona kwamba kuna maeneo ambayo tunatakiwa kuyazingatia. Eneo la kwanza ambalo tunatakiwa kuzingatia zaidi ni teknolojia ya ufundishaji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni ukweli kabisa kwamba kulingana na idadi ya wanafunzi ambao tunao katika vyuo vikuu vyetu mbalimbali, ili kuweza kuwafikia wanafunzi wote ni lazima teknolojia ya mawasiiliano iboreshwe kwa sababu sio rahisi wanafunzi wote kukaa darasani kwa wakati mmoja. Bado eneo hili la elimu ya masafa marefu halijatiliwa mkazo na mfumo huu kimsingi ungeweza kupunguza gharama hata za ada kwa wanafunzi kwa kuwa wanafunzi hao wanaweza wakasoma hata wanapokuwa sehemu mbalimbali katika mikoa yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini pia upo umuhimu wa kuboresha ufundishaji kwa vitendo. Ukiangalia sasa hivi tumeboresha zaidi kujenga majengo kama mabweni lakini katika ufundishaji wa vitendo, hususan katika fani ya sayansi na teknolojia, Serikali iweke kipaumbele katika kuhakikisha vifaa hivyo vinapatikana katika university zetu zote. Pia ipo haja ya kuhakikisha vyuo vinapanua uwezo wake wa kufundisha wanafunzi kwa kutumia teknolojia na uwezo ambao utaongeza wanafunzi kuwa wengi katika vyuo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini pia kuna tatizo la motisha kwa wafanyakazi. Wafanyakazi wengi ambao wapo pale hawana motisha. Walimu wengi au wahadhiri hupandishwa madaraja lakini hawalipwi stahiki zao kwa wakati. Unakuta kwamba mtu anajitahidi kufanya utafiti lakini akishapandishwa daraja hapati pesa kwa wakati na hiyo huwafanya kukata tamaa sana hasa katika eneo la utafiti.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, hili linaenda sambamba na kuhakikisha kuwa wale waliopandishwa madaraja wanapata motisha ili uweze kuwasaidia. Mtu anakuwa labda ni Assistant Lecturer amekuwa Lecturer au amepanda cheo amekuwa Profesa unakuta anaitwa Profesa lakini mshahara haujapanda. Kwa hiyo, mimi naishauri Serikali kwamba iweze kuangalia suala hili.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika masuala ya motisha kwa wafanyakazi, hasa Wahadhiri, ni pamoja na kuangalia masuala ya maeneo wanayoishi kwa mfano hata kupewa allowance za nyumba, allowance za kufanya kazi kwa muda ule wa ziada ili waweze kufanya kazi kwa motisha na madarasa pia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine ninaloweza kulishauri ni kwamba, sasa hivi Serikali imeongeza wanafunzi wengi sana katika vyuo vyetu na unakuta Mwalimu huyo anafundisha muda mrefu na anaweza akafundisha hata mara tatu kwa sababu wanafunzi wanaingia session tatu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine, nafikiri pia liangaliwe zaidi ni katika suala la hili GPA, unakuta kwamba mwanafunzi amemaliza degree yake ya kwanza ana GPA nzuri lakini sasa hapati yale masomo ya kuendelea, anapofika Masters (Shahada ya Uzamili) anatakiwa apate GPA ya 4. Kwa hiyo haya masuala yote yaweze kuangaliwa ili katika elimu ya juu tuweze kutoa wanafunzi ambao ni bora na Walimu nao waweze kuwa katika mazingira mazuri...

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MWENYEKITI: Ahsante Mheshimiwa kengele imeshagonga.

MHE. DKT. PAULINA D. NAHATO: Ahsante sana.