Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Mapendekezo ya Mpango wa Tatu wa Maendeleo wa Taifa kwa Miaka Mitano (2021/2022 – 2025/2026) na Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Mwaka 2021/2022 pamoja na Mapendekezo ya Muongozo wa Maandalizi ya Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka 2021/2022

Hon. Sylivia Francis Sigula

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Mapendekezo ya Mpango wa Tatu wa Maendeleo wa Taifa kwa Miaka Mitano (2021/2022 – 2025/2026) na Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Mwaka 2021/2022 pamoja na Mapendekezo ya Muongozo wa Maandalizi ya Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka 2021/2022

MHE. SYLIVIA F. SIGULA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipatia nafasi hii. Nianze moja kwa moja kwa kuchangia mapendekezo ya Mpango uliopo mbele yetu. Nianze kwa kumpongeza Waziri wa Fedha. Kwa kweli ukiusoma mpango utaona kabisa dhamira ya dhati ya kutupeleka katika uchumi imara tunaoutarajia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda sana kwa ajili ya muda nijielekeze katika Sekta ya Uvuvi. Tunapoteza sana mapato katika Sekta ya Uvuvi. Nasema hivi kwa sababu Tanzania tumebarikiwa. Tuna maziwa ambayo tungeweza kuyatumia yakatusaidia kutengeneza ajira nyingi lakini pia kukuza uchumi. Kwa sababu tukiangalia vipaumbele vyetu tunasema kipaumbele ni kukuza uchumi na pato la Taifa, lakini kwenye Sekta hii ya Uvuvi tunapoteza mapato mengi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimesoma hapa naona kwamba tutapanua Bandari za Kigoma na Tanga lakini pia kuboresha miundombinu. Nitoe mfano mdogo tu; tumekuwa na tatizo, japo limeahidiwa kwenye ilani, Meli yetu ya Liemba, kuanzia mwaka 2017 haifanyi kazi. Kwa kweli tumepata hasara na uchumi umezorota. Kwa hiyo maboresho haya yatakwenda sambamba na kuipatia Serikali mapato lakini pia tutatengeneza ajira nyingi kwa vijana wetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukiangalia Meli yetu hii ya Liemba na Ziwa Tanganyika, linawanufaisha watu wa Kigoma, Katavi pamoja na Rukwa. Kwa hiyo kuwepo kwa fursa hii ya meli kutaweza kuchochea maendeleo kwa haraka, lakini pia kukuza kipato na uchumi. Pia tukiangalia Ziwa letu Tanganyika hili tunashirikiana na wenzetu wa Burundi na Kongo. Kwa hiyo kuwepo kwa meli hii kutachochea sana kipato na uchumi, lakini pia Serikali itaweza kukuza uchumi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimeangalia pia naona kabisa kutokuwepo kwa meli hii kumezorotesha uchumi. Vijana wengi wamekosa ajira lakini pia hata usafirishaji wa mazao ambayo yanapatikana Kigoma, Katavi na Rukwa umekuwa shida.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba niishauri Serikali katika mpango wetu huu ni Mpango mzuri sana na ukiupitia Mpango mzima unaona kabisa tutatoka hapa kwenda level nyingine. Niombe marekebisho haya ya bandari hizi, upanuzi huu ufanyike kwa haraka ili Serikali isiendelee kupoteza mapato yanayotokana na Sekta hii ya Uvuvi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, wakati nachangia hotuba ya Mheshimiwa Rais nilijielekeza katika Sekta ya Sanaa na kwa sababu muda ulikuwa mchache nilishindwa kusema; siyo vibaya sana kujifunza kwa wenzetu wanaofanikiwa. Nimepata kusoma Makala moja, tunaambiwa wenzetu wa Nigeria mwaka 2013 suala la Sanaa lilichochea maendeleo sana na liliweza kuchangia zaidi ya robo ya bajeti yao katika Serikali yao. Kwa hiyo na sisi tunaweza tukatengeneza fursa nyingi kupitia huko, lakini tukubali kujifunza kwa waliofanikiwa, siyo dhambi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimeona kwenye hotuba hii Mheshimiwa Dkt. Mpango amekiri kwamba pamoja na mengine tuliyoyafanya kumekuwa na changamoto. Nimeona kuna baadhi ya Wabunge wamefanya kama kebehi, lakini niseme tunapokubali changamoto au unapokiri changamoto siyo udhaifu ila ni uimara, kwa sababu changamoto ndizo zinazokujenga. Kwa hiyo wanaobeza naomba tu niseme wanakosea kwa sababu kukiri changamoto pia kunakuimarisha.

Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda niendelee hapo, kwa sisi watu tunaopakana na maziwa haya, nikiizungumzia Ziwa Tanganyika na Ziwa Victoria, tunaona kabisa kupitia maziwa haya tunaweza tukatengeneza viwanda vikatusaidia kuwaajiri vijana wengi. Hata hivyo, lazima tukubali, lazima niishauri Serikali na Wizara husika; lazima tuwekeze katika Sekta hii ya Uvuvi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, bado tuna changamoto, hatuna vifaa imara vya kuvulia. Bado tuna changamoto vifaa tulivyonavyo haviwezi kutusaidia kuendesha viwanda hivi vya uvuvi. Kwa hiyo niombe sana, bado tuna kazi ya kufanya, lazima tuwekeze ili tuweze kupata matunda bora sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja. Ahsante sana. (Makofi)