Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Mapendekezo ya Mpango wa Tatu wa Maendeleo wa Taifa kwa Miaka Mitano (2021/2022 – 2025/2026) na Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Mwaka 2021/2022 pamoja na Mapendekezo ya Muongozo wa Maandalizi ya Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka 2021/2022

Hon. Michael Mwita Kembaki

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Tarime Mjini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Mapendekezo ya Mpango wa Tatu wa Maendeleo wa Taifa kwa Miaka Mitano (2021/2022 – 2025/2026) na Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Mwaka 2021/2022 pamoja na Mapendekezo ya Muongozo wa Maandalizi ya Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka 2021/2022

MHE. MICHAEL M. KEMBAKI: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa sababu ni mara yangu ya kwanza kusimama katika Bunge hili, napenda kuchukua nafasi hii adhimu kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa kunipa nafasi hii ili leo niweze kusimama hapa na niweze kuchangia katika Mpango huu ambao umeletwa katika Bunge letu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia napenda kuchukua nafasi hii kuwashukuru wanananchi wa Tarime, wapiga kura wangu kwa kura nyingi walizonipa ili niweze kuwakilisha katika Bunge hili la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Najua wana imani kubwa na Chama cha Mapinduzi lakini pia wana imani kubwa na mimi, niwahakikishie kwamba nitawatendea haki kuwawakilisha vyema kuhakikisha kwamba mji wetu unaendelea vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini pia nichukue nafasi hii kushukuru chama change, Chama cha Mapinduzi kwa kuniamini na kuniteua kupeperusha bendera ya Chama cha Mapinduzi na hatimaye tukapata ushindi mnono katika jimbo ambalo lilikuwa limekaa upande wa pili kwa muda mrefu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kuchukua nafasi hii kumshukuru Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kazi kubwa ambayo ameifanya kwa kipindi cha miaka mitano iliyopita. Nikianza upande wa elimu, Serikali imefanya kazi kubwa ikiwemo ujenzi wa miundombinu muhimu katika shule zetu zaidi ya 3,904 kwa mwaka 2019/2020. Vilevile imetoa elimu bure kwa shule za msingi na sekondari na imetoa pesa nyingi kugharamia masomo hayo ambayo imewezesha watoto wetu kupata elimu kwa wingi katika nchi yetu ya Tanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ndugu zangu mchango wangu nitauelekeza sana upande wa ukusanyaji wa mapato. Ili nchi iweze kusimama na iweze kutekeleza miradi ambayo imepangwa katika kipindi cha mwaka huu au miaka inayokuja lazima iwe vizuri katika ukusanyaji wa mapato ili uweze kupata fedha ya kutosha kujiendesha.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nina mashaka kidogo kuhusiana na ukusanyaji wa mapato katika nchi yetu na hii nipeleke kwa TRA. Mfano katika Jimbo letu la Tarime Mjini hakuna mahusiano mazuri kati ya TRA na wafanyabiashara. Mfano cement katika Mji wetu wa Tarime inauzwa Sh.24,000 ambapo cement inayotoka katika nchi jirani ya Kenya inauzwa Sh.16,000. Kipato cha watu wa Tarime bado kipo chini na wanahitaji kujenga na ukiangalia cement inayotoka katika nchi jirani inauzwa bei ya chini tofauti ya Sh.8,000. Hivyo basi, naomba Mamlaka ya Mapato na Bunge hili Tukufu tuangalie namna gani tunaweza kufanya ili hizi kodi ambazo ni kubwa zinazopelekea wafanyabiashara kukwepa kodi ziangaliwe upya. Waziri Mpango aweze kuleta hoja hapa ili hizi kodi ziweze kuangaliwa upya ziweze kusababisha wafanyabiashara walipe kodi bila kukwepa kodi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kinachonisikitisha ni kwamba badala ya TRA kutoa elimu kwa wafanyabiashara na kwa wananchi inatumia nguvu kukusanya kodi. Mfano kama mfanyabiashara au wale wanaoendesha bodaboda amekwenda kuchukua cement moja Kenya anaileta huku, wanatumia gharama kubwa kufukuza vijana hawa na mwishoni vijana hawa wamekuwa wakiumia na wengine hata kufariki wakitumbukia kwenye mitaro na kujigonga pembezoni mwa barabara. Naamini njia pekee ambayo tungeweza kufanya ni TRA kukaa chini na wafanyabiashara waone umuhimu wa kulipa kodi kwa hiari bila kufukuzana nao. Pia kutoa elimu kwa wananchi, mfano, ukienda kununua spear dukani unaambiwa bei mbili; ya kwanza unaambiwa…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MWENYEKITI: Kengele imegonga Mheshimiwa.

MHE. MICHAEL M. KEMBAKI: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba niunge hoja mkono lakini pia nina mambo mengi ya kusema. (Makofi)