Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Mapendekezo ya Mpango wa Tatu wa Maendeleo wa Taifa kwa Miaka Mitano (2021/2022 – 2025/2026) na Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Mwaka 2021/2022 pamoja na Mapendekezo ya Muongozo wa Maandalizi ya Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka 2021/2022

Hon. Oran Manase Njeza

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mbeya Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Mapendekezo ya Mpango wa Tatu wa Maendeleo wa Taifa kwa Miaka Mitano (2021/2022 – 2025/2026) na Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Mwaka 2021/2022 pamoja na Mapendekezo ya Muongozo wa Maandalizi ya Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka 2021/2022

MHE. ORAN M. NJEZA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana kwa kunipa fursa hii ya kuchangia mapendekezo ya huu Mpango. Kwanza nianze kwa kumpongeza sana Mheshimiwa Waziri wa Fedha pamoja na timu yake. Kwa kweli, wamekuja na mpango ambao ni wa kibunifu sana hasa kwa dunia ya leo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukiangalia dhima nzima ya huu mpango ambao ni ushindani kwa kweli, unabeba kitu kikubwa zaidi ambacho duniani kote sasa hivi ushindani sio wa bidhaa peke yake, lakini mataifa yanashindana kuangalia resources zao walizonazo ni namna gani wazitumie vizuri na sisi kwa Tanzania Mwenyezi Mungu ametujalia resources nyingi sana ambazo kwa kweli ni za kishindani.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikianza kwa uchache tu kwa ajili ya muda, ukianza uzalishaji wa madini yetu. Kwanza nashukuru Serikali kwa kutunga Sheria ya Madini, lakini yale madini tutayatumia namna gani ili yatuletee kipato na kuongeza pesa za kigeni? Nina imani Waziri wa Fedha anahitaji FDIs nyingi. FDIs atazipata kutokana na mazao yetu ya madini. Kwetu Mbeya, Wilaya ya Mbeya ambayo na Mheshimiwa Mwenyekiti na wewe ndio unakotokea wilaya hiyo, sisi hatujaanza kuzalisha, lakini tuna madini yanaitwa niobium. Inawezekana likawa ni jina geni sana kwa Wabunge, lakini madini ya niobium ni madini adimu sana na huo mgodi ambao unaanzishwa utakuwa wa kwanza Afrika na wa nne duniani. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa ninachoiomba Serikali ni namna gani kufuatia mpango huu iweke hii mipango kwenye mpango wa muda mfupi, lakini iiweke vilevile kwenye mpango wa miaka mitano kwa sababu, haya madini yanategemewa yanaweza kuvunwa kwa miaka zaidi ya 30 mpaka 50. Sasa hayo madini yanatumika kwenye nini?

Mheshimiwa Mwenyekiti, hayo madini kwa kiasi kikubwa yanatumika kwenye kuimarisha vyuma, kwa hiyo, yataendana pamoja na madini ambayo tunayazalisha ya chuma cha Liganga. Hawa wawekezaji wanataka waanzishe hiki kiwanda cha kwanza Afrika, kwa hiyo, watachimba na kuchenjua, ili bidhaa hii ambayo inaitwa niobium ambayo ni ya kwanza kwa Afrika iweze kuzalishwa hapa kwetu na rasilimali kutoka mataifa mengine yaje hapa kwetu yalete hiyo rasilimali na sisi tuwe wazalishaji wakubwa. Haya ndio madini yanayotakiwa kwa leo ili tuweze kujenga madaraja ya baharini, madaraja ya ziwani, reli SGR na kadhalika. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, vile vile ukiangalia wataleta nini; hawa wanaleta FDI ya karibu zaidi ya bilioni 250 ambazo kila mwaka zitazalisha zaidi ya dola milioni 220, ukiangalia hiyo ni asilimia kubwa sana. Sasa ningeomba katika mikakati ya namna hii Wizara ziwe zinashirikiana isiwe kitu cha Wizara moja. Hizi ni opportunities, hizi ni fursa na haya madini kadri miaka inavyokwenda na teknolojia inavyobadilika si ajabu yakawa mawe ya kawaida tunayoyaona kama tunavyoyaona haya ya hapa mwanzo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini kuna suala zima la kilimo cha pareto. Nalo ni zao ambalo inawezekana watu wengi wakashangaa, lakini pareto tunayolima Tanzania kwenye Wilaya ya Mbeya ni ya kwanza Afrika na ya pili duniani. Inatumika kutengeneza dawa za kuua wadudu, lakini zaidi zaidi inatumika sasa hivi kwenye kutengeneza dawa za kuhifadhi nafaka na hii ni organic. Sasa viwanda vya namna hii inatakiwa viwekwe kwenye kipaumbele, ndio tunavyovihitaji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naiomba Wizara ya Kilimo iangalie kwa kipekee namna gani tuweze kuvutia viwanda vitakavyozalisha dawa zinazotokana na pareto. Kwa vile hatuna mshindani, wenzetu jirani zetu wanakuja kuchukua kwetu raw materials kutoka Tanzania, wanatengeneza hiyo raw materials, wanasafirisha kwenda nje. Sasa hivi Uganda na Kenya pamoja na Rwanda ndio wamekuwa wateja wazuri sana kwa wakulima wangu kule Mbeya kwenye mazao haya ambayo sisi yanakuwa ni semi processed.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naiomba sana Wizara iangalie namna gani tuchukue majukumu ambayo yataisaidia nchi yetu kupunguza pengo la pesa za kigeni. Pesa za kigeni zikipungua hatari yake ni nini? Hata ile kuingia kwenye uchumi wa chini wa kati ni rahisi tukaporomoka mara moja. Sasa hivi tuna dola 1,080 ambayo iko chini kabisa. Exchange rate kama sio tulivu ina maana tunaweza kuporomoka tukarudi tulikotoka. Sasa tuki-take advantage hii kwa fursa tulizonazo…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MWENYEKITI: Ahsante Mheshimiwa, kengele imegonga.

MHE. ORAN M. NJEZA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana na naunga mkono hoja. (Makofi)