Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Mapendekezo ya Mpango wa Tatu wa Maendeleo wa Taifa kwa Miaka Mitano (2021/2022 – 2025/2026) na Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Mwaka 2021/2022 pamoja na Mapendekezo ya Muongozo wa Maandalizi ya Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka 2021/2022

Hon. Nape Moses Nnauye

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mtama

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Mapendekezo ya Mpango wa Tatu wa Maendeleo wa Taifa kwa Miaka Mitano (2021/2022 – 2025/2026) na Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Mwaka 2021/2022 pamoja na Mapendekezo ya Muongozo wa Maandalizi ya Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka 2021/2022

MHE. NAPE M. NNAUYE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi. Pamoja na kuwashukuru wananchi wangu wa Jimbo la Mtama kwa kuniamini na kunipitisha bila kupingwa kuwa mwakilishi wao ndani ya Bunge hili, nakishukuru pia chama changu, Chama cha Mapinduzi, kwa kunipa dhamana hii. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja. Kwa kuwa muda hautoshi, naomba nizungumze mambo mawili. Mpango huu ni mzuri sana lakini utafanikiwa tu ikiwa kutakuwa na fedha za kuutekeleza. Fedha zinapatikana kutoka kwenye makusanyo ya kodi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna changamoto kubwa sana inaendelea katika nchi yetu. Ukusanyaji wa kodi ni taaluma na katika historia ni taaluma ya muda mrefu sana. Changamoto tuliyonayo ni kwamba tumeamua kuacha kuwatumia wataaluma ambao ndiyo wakusanya kodi badala yake tunatumia Task Forces kukusanya kodi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Task Forces kwa sababu siyo taaluma yao, wanachofanya wanakwenda kuua biashara. Kelele hizi zote unazozisikia ni kwa sababu tumeamua kuacha kutumia taaluma ya ukusanyaji wa kodi, tumeamua kutumia Task Forces kukusanya kodi na kwa sababu siyo taaluma yao wanachoangalia ni kufikia lengo walilowekewa. Kinachotokea ni kwamba wanakwenda kwa mfanyabiashara, hawajali maisha yake ya kesho, hawajali kwamba wanatakiwa wakusanye kodi leo wamuachie uwezo wa kuzalisha ili wakusanye na kesho. Tunafurahia matokeo ya muda mfupi; ni kweli tumefanya kazi nzuri ya kukusanya kodi, lakini haya matokeo tunayoyafurahia ni ya muda mfupi sana kwa sababu idadi ya biashara zinazofungwa ni nyingi mno, kesho hatuna ng’ombe wa kumkamua maziwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ushauri wangu kwa Serikali, hebu punguzeni habari ya Task Forces kukusanya kodi, siyo kazi yao, hawa wanakwenda kuua biashara. TRA ilianzishwa kwa kazi hiyo na watu wamesomea. Tukijiwekeza kwenye Task Forces kesho hatutakuwa na cha kukusanya kwa sababu siyo kazi yao. Nimeambiwa baadhi ya maeneo wanakwenda na draft ya kesi za uhujumu uchumi, wanawatisha watu, watu inabidi watoe fedha, wakitoa fedha wanafunga biashara zao. Sasa mwendelezo wa hiki tunachokifanya mwisho wake utakuwa nini? Ushauri wangu Serikali ondokeni kwenye Task Forces, rudini kwenye taaluma ya ukusanyaji wa kodi itatupa uhalali wa kuendelea kukusanya hiyo kodi kesho na kesho kutwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hoja ya pili, tumefanya vizuri sana kwenye kuungamanisha ukuaji wa uchumi na maendeleo ya watu kwenye Sekta ya Elimu. Tumetoa elimu ya msingi bila malipo kwa kipindi cha miaka mitano; siyo kazi ndogo. Hata tulipofanya uamuzi huu tulijua ni kazi kubwa. Nampongeza Mheshimiwa Rais na Serikali yake kwa kazi nzuri waliyofanya ya kutekeleza jambo hili. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa ushauri wangu; tumetekeleza kwa kipindi cha miaka mitano, tumefanya vizuri lakini bila shaka umefika wakati tupitie changamoto tulizokutana nazo katika kipindi cha miaka mitano halafu tufanye marekebisho kwa baadhi ya maeneo. Hapa ntatoa mfano, tunatumia kigezo cha idadi ya wanafunzi kupeleka fedha, kigezo hiki nadhani kimepitwa na wakati, twende tutanue. Kwa sababu mtu mwenye watoto kumi na mwenye watoto 200 baadhi ya mahitaji yanafanana, ukimpelekea fedha ileile unamuua huyu mwenye watoto wachache.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, nadhani ni vema Serikali tupitie upya, tuangalie hivi vigezo tunavyovitumia vya kupeleka fedha kusaidia elimu bure. Jambo hili ni jema lakini tupitie upya tuliboreshe, tulifanye vizuri ili tuongeze vigezo vya kupeleka fedha. Fedha za utawala zizingatie mahitaji ya kiutawala. Fedha za kuangalia mwenendo wa watoto, performance yao zifuate hivyo vigezo vingine lakini tuongeze idadi ya vigezo; nadhani hili jambo litatusaidia twende mahali pazuri zaidi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja, nakushukuru kwa nafasi uliyonipa. (Makofi)