Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Mapendekezo ya Mpango wa Tatu wa Maendeleo wa Taifa kwa Miaka Mitano (2021/2022 – 2025/2026) na Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Mwaka 2021/2022 pamoja na Mapendekezo ya Muongozo wa Maandalizi ya Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka 2021/2022

Hon. Jonas William Mbunda

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mbinga Mjini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Mapendekezo ya Mpango wa Tatu wa Maendeleo wa Taifa kwa Miaka Mitano (2021/2022 – 2025/2026) na Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Mwaka 2021/2022 pamoja na Mapendekezo ya Muongozo wa Maandalizi ya Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka 2021/2022

MHE. JONAS W. MBUNDA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa kupata nafasi. Awali ya yote, naomba nimshukuru Mwenyezi Mungu kwa kupata nafasi ya uhai. Vilevile naomba nikishukuru Chama changu cha Mapinduzi kwa kuniteua kuwa mgombea na pia niwashukuru wapigakura wangu wa Jimbo la Mbinga Mjini kwa kunichagua kwa kishindo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba niende moja kwa moja kwenye Mpango wa Awamu ya Tatu wa Maendeleo. Dhima ya Mpango wa Awamu ya Tatu wa Maendeleo ya Taifa ni kujenga uchumi shindani na viwanda kwa maendeleo ya watu. Hata hivyo tutajengaje uchumi huu? Ni lazima tuhakikishe kwamba nyanja zote zinazotakiwa zilete maendeleo zimesimamiwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mchango wangu utakuwa kwenye suala la kilimo. Ukiangalia Mpango uliopita tulikuwa na malengo ya kukua kwa uchumi kupitia kwenye upande wa kilimo kwa asilimia 7.6 lakini uchumi huo ulikua kwa asilimia 4.4. Ukija kwenye uchangiaji wa pato la Taifa napo tumeshuka. Kwa hiyo, utaona kabisa kwamba kwenye suala la kilimo tumerudi nyuma lakini ukiangalia sehemu kubwa ya wananchi wa Tanzania wanashughulika na kilimo na wako vijijini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, siku ya mwisho tunategemea kwamba tutakuja kupata maendeleo ya watu na kuondoa umaskini kwa kupitia kilimo. Tutakapokuja kugawa na kuona kila mwananchi anapata kiasi gani ili aweze kuonekana kwamba ameendelea kimaisha tutaangalia pamoja na idadi hiyo kubwa ya wakulima ambao wako vijijini na bado wanaishi katika maisha ya shida.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nachoishauri Serikali kwanza kabisa, kama walivyochangia wenzangu kwenye suala la mbegu tuhakikishe kwamba wakulima wanasaidiwa namna ya kupata mbegu bora. Pia Wizara ya Kilimo isimamie kuhakikisha kwamba wananchi wanapata pembejeo zenye ruzuku. Zaidi ya hapo wananchi hao wasaidiwe kupata masoko ya uhakika hasa wale ndugu zangu wakulima wa kahawa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ili sasa tuweze kufika kwenye maendeleo, hasa kwenye suala la viwanda, kwenye suala la elimu naipongeza Serikali imefanya vizuri lakini hatujawekeza sana kwenye suala la elimu ya ufundi. Kwa hiyo, naishauri Serikali kwenye suala la elimu ya ufundi ijitahidi kujenga vyuo vya VETA kwenye wilaya zetu ili suala la ufundi lifike kwa wananchi wetu na waweze kuanzisha viwanda vidogo vidogo ili viweze kusaidia kwenye suala la maendeleo ili tuweze kufikia uchumi wa viwanda na wananchi hawa waweze kupata unafuu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ili tuweze kupata maendeleo lazima pawe na umeme wa uhakika. Naomba niipongeze Serikali kwa kujenga miundombinu mingi ya umeme na kugawa kwenye maeneo mbalimbali lakini tatizo kubwa lipo katika upatikanaji wa umeme wa uhakika. Katika Jimbo langu la Mbinga Mjini, kila mara natumiwa meseji za kunijulisha kwamba umeme umekatika. Kwa hiyo, tutashindwa kabisa kufanya kazi za maendeleo kama tutakuwa hatuna umeme wa uhakika katika maeneo yetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba niunge mkono hoja. (Makofi)