Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Mapendekezo ya Mpango wa Tatu wa Maendeleo wa Taifa kwa Miaka Mitano (2021/2022 – 2025/2026) na Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Mwaka 2021/2022 pamoja na Mapendekezo ya Muongozo wa Maandalizi ya Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka 2021/2022

Hon. Selemani Moshi Kakoso

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mpanda Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

2

Ministries

nil

Mapendekezo ya Mpango wa Tatu wa Maendeleo wa Taifa kwa Miaka Mitano (2021/2022 – 2025/2026) na Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Mwaka 2021/2022 pamoja na Mapendekezo ya Muongozo wa Maandalizi ya Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka 2021/2022

MHE. MOSHI S. KAKOSO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nishukuru sana kunipa nafsi nami nichangie Mpango wa Taifa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nijikite katika eneo moja ambalo litatusaidia sana Waheshimiwa Wabunge tujue nini cha kufanya. Asilimia kubwa ya Wabunge wanalalamikia sana miundombinu na TARURA. Yalikuwepo mawazo kufikia hatua ya kutaka kufanya mgawanyo wa fedha za Mfuko wa Barabara.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nichukue nafasi hii kuwaelimisha ili wajue. La kwanza Mfuko wa Barabara umeundwa kwa sheria ambayo ilipitishwa na Bunge. Malengo yake yalikuwa kuhakikisha barabara zilizojengwa na TANROADS zinakuwa imara na zinapitika katika kipindi chote. Fedha za Mfuko wa Barabara si nyingi, ni karibia bilioni 900 kwa mwaka. Asimilia 70 ya fedha hizo zinaenda TANROADS kwa ajili ya maintenance barabara zetu, 30% ndizo ambazo zinaenda kuhudumia barabara za vijijini na mijini. Sasa hapa ndipo ambapo mnaweza mkaona kwamba tuna eneo ambalo Serikali inatakiwa ilifanyie kazi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mfuko wa Barabara ambao una 100%, 70% zinachukuliwa na TANROADS na ..

MWENYEKITI: Waheshimiwa Wabunge, anayechangia ndiye Mwenyekiti wa Kamati yetu ya Miundombinu. Kwa hiyo, tumsikilize vizuri mawazo yake kuhusu hii hoja ambayo Wabunge tumekuwa tukiisemea sana ya TANROADS na TARURA. Endelea Mheshimiwa. (Makofi)

MHE. MOSHI S. KAKOSO: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo hizo 30% hazina uwezo wa kutengeneza kitu chochote. Kwa mwaka 2015/2016 Mfuko wa Barabara; TANROADS walipata shilingi bilioni 541 na TARURA zilienda shilingi bilioni 257. Mwaka 2016/2017 TANROADS zilienda shilingi bilioni 519 na TARURA zilienda shilingi billioni 247. Mwaka 2018 TANROADS zilienda shilingi bilioni 573 na TARURA zilienda shilingi bilioni 246. Mwaka 2020 TANROADS zimeenda shilingi bilioni 524 na TARURA zimeenda shilingi 224. Mwaka 2021 TANROADS zitaenda shilingi bilioni 572 na TARURA zitaenda shilingi bilioni 245. Barabara za TARURA zina zaidi ya kilometa 130,000 kitu ambacho haziwezi kutengenezwa kwa hizi fedha zinazotengwa. Ni miujiza ambayo itatokea kama tutaweza kutatua tatizo la TARURA. TANROADS wanaweza kwa sababu Serikali Kuu wanatoa bajeti ya kujenga barabara na hata hizi zinazotengwa kwa 70% hazitoshi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nina ushauri Waheshimiwa Wabunge, tunapokuwa tunajenga hoja ili barabara zetu ziweze kutengenezwa tuna maeneo ambayo tunaweza tukaishauri Serikali. La kwanza Serikali itenge fedha iwape TAMISEMI wawe na bajeti kwa ajili ya kujenga barabara zetu za vijijini. La pili linahitaji maamuzi sisi wenyewe kama Wabunge. Mimi naangalia chanzo kipya ambacho tunaweza tukakiangalia kikaja kutatua tatizo la ujenzi wa barabara za mijini na vijijini kupitia TARURA.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kipengele ambacho nataka niwashawishi Wabunge wenzangu kama tutafika mahali tukakubaliana, tukaishauri Serikali na Serikali ikachukua mawazo yetu, tuna eneo la mawasiliano. Kwenye sekta ya mawasiliano kwa siku tuna uwezo wa kutumia simu milioni 30, hizo zinafanya kazi ndani ya nchi yetu, tuna idadi ya simu karibia milioni 50. Kwa hiyo, milioni 30 zina uwezekano wa kupata chanzo kipya cha fedha na huko ni eneo ambalo ni luxury tu asilimia kubwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, napendekeza tutenge shilingi kumi kila mtumiaji wa simu ajue kwamba leo ninapopiga simu nachangia shilingi kumi kwa ajili ya mfuko wa barabara, zitakazokuja kujenga barabara za miji na vijijini. Milioni 30 mara kumi utapata milioni 300 mara saa moja, mara mwezi, mara mwaka, tuna uwezo wa kupata trilioni 1.296 ambazo zitakuja kutoa tatizo la barabara, hapo tunakuwa na chanzo ambacho ni kizuri na ambacho hakitakuwa na tatizo kwa wananchi wote na watu watakuwa wanajua kwamba mimi kama mtumiaji wa simu ninayetumia siku ya leo nimechangia barabara za miji na vijijini, tatizo hili litakuwa limeondoka kabisa. Naomba eneo tulifanyie kazi na wenzetu wa Kamati ya Bajeti waendee wakajaribu kuangalia haya. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo lingine ni kwenye eneo hilo hilo la mawasiliano, sisi tunafanya miamala ya simu kwa siku kwa mwezi tunafanya miamala yenye thamani ya shilingi milioni 300, kila mwezi ambayo iko kwenye mzunguko na Serikali wanapata fedha kupitia mzunguko huo huo karibu kwa mwezi mmoja kunakuwa mzunguko wa fedha wa trilioni 18 zinazozunguka kwenye sekta ya mawasiliano. Kwa hiyo, hata huko nako tukiangalia kwamba pana uwezekano naamini tunaweza tukafikia karibu trilioni moja na nusu tukapata fedha hizi zikaja kujenga mazingira ambayo yatawasaidia Watanzania, hata hiki kilimo tunachokisema kama hatuna barabara zinazounganisha huko vijijini ni sawa na hakuna. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hili ni eneo ambalo nililiona ni la muhimu sana, na ile dhana ambayo mnafikiri Waheshimiwa Wabunge kwamba tuzigawanye zile fedha tunakosea. Tusije tukarogwa kuja kupotosha kabisa kuuhamisha ule Mfuko wa TANROAD, tukihamisha matokeo yake barabara nyingi zilizojengwa na Serikali zitakufa, tukajifunze Zambia, Zambia walifanya kosa kama hili walijenga barabara hawakutenga fedha za maintenance matokeo yake barabara zote asilimia kubwa zilikuwa mashimo mashimo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hapa nchini ipo barabara ambayo ni ya mfano ilijengwa kwa mfumo huo, haikutengewa fedha za maintenance, barabara ya kutoka Arusha, Minjingu iliisha ndani ya kipindi kifupi sana. Naomba hili tulifanyie kazi na naomba Serikali ipokee mawazo ili yaweze kusaidia kutatua tatizo la barabara za miji na vijijini. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo hili ndilo nililochagua kuchangia kwenye mpango ili liweze kutusaidia na wananchi wote wajue na Waheshimiwa Wabunge waelewe kwamba mfuko tunaouchangia ni mfuko ambao fedha zake sio nyingi sana na tukiumega una athari kubwa sana ambazo zitaleta kwa Taifa letu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. (Makofi)