Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Hotuba ya Mheshimiwa Rais, Dkt. John Pombe Joseph Magufuli aliyoitoa wakati wa Ufunguzi wa Bunge la Kumi na Mbili, Tarehe 13 Novemba, 2020

Hon. Mashimba Mashauri Ndaki

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Maswa Magharibi

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Hotuba ya Mheshimiwa Rais, Dkt. John Pombe Joseph Magufuli aliyoitoa wakati wa Ufunguzi wa Bunge la Kumi na Mbili, Tarehe 13 Novemba, 2020

WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Naibu Spika, nikushukuru sana kwa kunipa nafasi ili niweze kuchangia sehemu ya hotuba ya Mheshimiwa Rais ambayo aliitoa tarehe 13 Novemba, 2020. Kabla ya hapo nichukue nafasi hii kumshukuru sana Mungu kwa kuniwezesha kurudi tena kwenye nyumba hii ambayo kwa kweli, sio rahisi kurudi, lakini kwa nguvu za Mungu basi anatuwezesha kurudi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nichukue nafasi hii pia kukishukuru Chama Cha Mapinduzi pamoja na wapiga kura wangu wa Jimbo la Maswa Magharibi kwa kunipa imani tena kurudi ndani ya nyumba hii, lakini nichukue nafasi hii kwa kipekee sana kumshukuru sana Mheshimiwa Rais John Pombe Magufuli kwa kuniamini kwamba, naweza kumsaidia kazi kwenye Wizara ya Mifugo na Uvuvi. Namshukuru sana Mheshimiwa Rais na niahidi tu kwamba, sitamwangusha, nitafanya kazi kwa bidii, maarifa, nguvu zangu zote na akili zangu zote ili kusudi tu kusudi ambalo analiona linatakiwa kutimizwa na Wizara hii basi liweze kukamilika. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Wizara ya Mifugo na Uvuvi ilipewa malengo makubwa mawili kwenye hotuba ya Mheshimiwa Rais. La kwanza, ni kuhakikisha kwamba, sekta hizi mbili zinachangia kwa sehemu kubwa kuondoa umaskini wa Watanzania wanaoshughulika na mifugo na uvuvi, lakini la pili kuhakikisha sekta hizi zinachangia kwa sehemu kubwa kwenye pato la Taifa na la mwisho kuhakikisha sekta hizi zinachangia kwenye ajira kwa Watanzania, kitu ambacho kimekuwa adimu sana.

Mheshimiwa Naibu Spika, tulipewa pia kwenye hotuba hiyo lengo dogo mahususi hasa kuhusiana na uvuvi wa bahari kuu kwamba, sasa uvuvi wa bahari kuu uchangie kwa mwaka bilioni 352 badala ya kuchangia kwa wastani wa bilioni 3.3 kwa mwaka. Sasa hayo ndio malengo makubwa yaliyoko kwenye hotuba ya Mheshimiwa Rais. Sasa pamoja na kwamba, tungependa sana kufikia malengo hayo, lakini kuna changamoto ambazo Waheshimiwa Wabunge katika michango yao hapa wamekuwa wakiziainisha, lakini pia ziko changamoto nyingine ambazo hazijaweza kuainishwa na Waheshimiwa Wabunge, lakini tumeziona katika Wizara ya Mifugo na Uvuvi tulipoingia hapo.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa upande wa uvuvi lipo suala la uvuvi haramu. Uvuvi haramu unapunguza rasilimali ya uvuvi katika nchi yetu bila mpangilio wowote. Kwa hivyo, uvuvi haramu unapaswa kupigwa vita kwa namna yoyote ile na kila Mtanzania ili tuweze kulinda rasilimali hii na tuweze kuirithisha hata kwa wenzetu watakaokuja baadaye. Sasa ili kuondoa uvuvi haramu sisi tumekuja na mbinu shirikishi tukitaka kuwashirikisha wadau wote wanaohusika na uvuvi, ili kuhakikisha kwamba, tunakubaliana ni kwa namna gani kwa pamoja tuweze kuondoa uvuvi haramu ambao ni hatari kwa rasilimali hii ya uvuvi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, liko suala la tozo mbalimbali ambazo Waheshimiwa Wabunge pia wamezitaja. Tumeliona na tumeliangalia, kwa sehemu kubwa limefanyiwa kazi suala la tozo, lakini tutaendelea kuliangalia suala la tozo zinazotozwa kwa leseni za biashara na tozo nyingine zinazotozwa zinakwaza wavuvi wetu. Tutaliangalia kwa upande wa juu, lakini niombe pia Wizara ya TAMISEMI, Mamlaka za Serikali za Mitaa, waangalie pia na wao kwa upande wao tozo wanazotoza kwa upande wa uvuvi ili tuwaondolee mzigo mzito wavuvi wetu kwenye maeneo yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, suala lingine katika uvuvi ni suala la uvuvi kwa bahari kuu. Tumejipanga vizuri na suala hili, Mheshimiwa Rais alishasema kwenye hotuba yake, kuna mpango wa meli zile nane; nne Bara na nne Zanzibar, lakini kwa Bara pia tumepata msaada mwingine wa meli moja kutoka Japan kwa hiyo zitakuwa tano. Kwa hiyo, tutakuwa na meli tano zitakazoanza kuvua kwenye uvuvi wa bahari kuu, lakini pia shirika letu au Mamlaka yetu ya Uvuvi wa Bahari Kuu imeimarishwa sasahivi ina staff wanaofanya kazi. Mwaka jana Sheria ya Uvuvi wa Bahari Kuu ilipitishwa, sasa hivi tunamalizia Habari ya kanuni zake tuipitishe ili tuweze kuanza kushughulika na uvuvi wa bahari kuu ambao kusudi lake ni kuleta bilioni 352 kwa mwaka. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa sababu ya muda, katika upande wa mifugo. Tumejipanga kwa habari ya miundombinu ili kuweza kuhakikisha kwamba, miundombinu ya uvuvi inakamilika katika maeneo ya wavuvi. Hii ni pamoja na malambo au mabwawa, minada, majosho na mambo mengine yanayotakiwa na wafugaji, ili kusudi tu waweze kuboresha mifugo yao ili iweze kuwa na afya bora na afya njema ili iweze kuleta tija kwa wananchi.

Mheshimiwa Naibu Spika, suala la malisho; katika suala hili pia tumejipanga vizuri kama Wizara, tumepanga kwamba tuwe na hekta milioni moja na nusu kufikia mwisho wa mwaka huu, lakini ndani ya miaka mitano tunataka kufikia malisho ya hekta milioni sita. Kwa hiyo, tumepanga ili kufikia lengo hilo, kwanza kwa kushirikiana na zileā€¦

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa muda wako umeisha.

WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana na naunga mkono hoja. (Makofi)