Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Hotuba ya Mheshimiwa Rais, Dkt. John Pombe Joseph Magufuli aliyoitoa wakati wa Ufunguzi wa Bunge la Kumi na Mbili, Tarehe 13 Novemba, 2020

Hon. Samweli Xaday Hhayuma

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Hanang'

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Hotuba ya Mheshimiwa Rais, Dkt. John Pombe Joseph Magufuli aliyoitoa wakati wa Ufunguzi wa Bunge la Kumi na Mbili, Tarehe 13 Novemba, 2020

MHE. SAMWELI X. HHAYUMA: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru kwa kupata nafasi hii. Awali ya yote, kwa sababu ni mara yangu ya kwanza kusimama ndani ya Bunge hili Tukufu, nitumie nafasi hii kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa kutupa uzima. Pia nikishukuru chama changu, Chama cha Mapinduzi na Wanahanang kuniwezesha kuwa Mbunge wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, aidha, nitumie nafasi hii kuishukuru familia yangu kwa jinsi wanavyoniunga mkono katika kufanikisha majukumu yangu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nitumie nafasi hii pia kukupongeza wewe na Mheshimiwa Spika kwa jinsi mnavyotuongoza vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa nijielekeze kwenye kuchangia hotuba ya Mheshimiwa Rais. Awali ya yote, nitumie nafasi hii kuipongeza sana Serikali yangu, Serikali ya Chama cha Mapinduzi, ikiongozwa na Jemedari, Dkt. John Joseph Pombe Magufuli, kwa kazi kubwa ambayo imefanyika kwa muda wa miaka mitano iliyopita.

Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Rais kwenye hotuba yake ameeleza mambo mengi ya msingi kwa ajili ya maendeleo ya nchi yetu. Nitajikita kwenye maeneo matatu kwa sababu ya muda.

Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Rais ameeleza mafanikio yaliyopatikana kwenye sekta ya maji, kwamba kwenye eneo la vijijini kumekuwa na ongezeko la upatikanaji wa maji kwa asilimia 47 mpaka asilimia 70.1 na mjini asilimia 74 mpaka asilimia 84; hayo ni mafanikio makubwa sana. Mheshimiwa Rais pia alibainisha kwamba wakati wa kampeni kulikuwa na malalamiko mengi kwenye eneo la maji.

Niombe Wizara ya Maji wawasimamie kwa karibu wataalam wetu ili miradi mingi ya maji ikamilike. Wenzangu waliotangulia waliiongelea, wengine walifikia hatua ya kusema miradi mingine isianzishwe lakini mimi nasema kwamba usimamizi uimarishwe ili miradi hii iweze kutekelezwa kwa wakati.

Mheshimiwa Naibu Spika, ninao mfano wa Mradi mmoja wa maji Katesh, mradi huu ni wa muda mrefu lakini mpaka sasa bado haujakamilika. Ukienda Mji wa Katesh watu wanatembea na mikokoteni mjini haipendezi sana. Tunaomba ule mradi ukakamilike. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tunao Mradi wa Maji wa Lambo ambao ulitakiwa ukamilike mwezi Mei, 2020, lakini mpaka sasa umefanyika asilimia 45 tu. Wananchi wanasubiri maji na ndiyo malalamiko mengi ambayo tunayapata kwa wananchi wetu. Naomba huo mradi uweze kukamilishwa kwa wakati.

Mheshimiwa Naibu Spika, nikiri kwamba Wizara inafanya kazi nzuri na kubwa. Mheshimiwa Waziri Aweso na Mheshimiwa Naibu Waziri Mheshimiwa Engineer MaryPrisca, wanafanya kazi kubwa sana. Kuthibitisha hilo, toka Uhuru, Kata ya Gehandu imekuwa ikilia maji, kwa sasa kisima kimechimbwa, maji yamepatikana mengi. Wameshafanya pump testing. Ninachoomba, usanifu ukamilike haraka ili mradi uweze kutekelezwa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, niongelee kidogo eneo la kilimo. Mheshimiwa Rais alibainisha wazi kabisa kwamba nchi yetu ina upungufu mkubwa wa ngano ya chakula na akamwelekeza Mheshimiwa Waziri wa Kilimo atakayemteua kwamba hiyo ndiyo iwe kazi yake ya kwanza. Nampongeza sana Waziri wa Kilimo, Mheshimiwa Profesa Mkenda na Naibu Waziri Mheshimiwa Bashe kwa kazi waliyoanza nayo. Wamekuja Hanang, tumetembea nao kwenye mashamba ya NAFCO, mashamba ya ngano ambapo Hanang ndiyo ilikuwa inaongoza kuzalisha ngano.

Mheshimiwa Naibu Spika, tuliwaahidi wananchi wale wakusanye ngano, kwa sasa zimeshakusanywa zaidi ya tani 480, zile ngazo zikanunuliwe ili wananchi wapate fedha za kurudi mashambani ili tuweze kuzalisha ngano zaidi. Pia tuliwaahidi wananchi wale mbegu; na sasa ni wakati wa msimu wa kupanda, tunaomba zile mbegu zipatikane. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, eneo la NAFCO yale mashamba yalikuwa ya mwekezaji kabla. Maeneo yale mengi yamebinafsishwa kwa wawekezaji wengine ambao uwezo wao ni mdogo. Naomba sana Wizara ya kilimo ifanye tathmini ya kina ya wale wawekezaji ambao wako kwenye lile eneo ili hatua stahiki ziweze kuchukuliwa tupate wawekezaji au Wanahanang wenye uwezo tuweze kutumia yale mashamba na wazalishe kwa tija.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa sababu ya muda, naomba niishie hapo, naunga mkono hoja. Ahsante sana. (Makofi)