Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Hotuba ya Mheshimiwa Rais, Dkt. John Pombe Joseph Magufuli aliyoitoa wakati wa Ufunguzi wa Bunge la Kumi na Mbili, Tarehe 13 Novemba, 2020

Hon. Zuberi Mohamedi Kuchauka

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Liwale

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Hotuba ya Mheshimiwa Rais, Dkt. John Pombe Joseph Magufuli aliyoitoa wakati wa Ufunguzi wa Bunge la Kumi na Mbili, Tarehe 13 Novemba, 2020

MHE. ZUBERI M. KUCHAUKA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa nafasi ili niweze kuchangia hotuba ya Rais. Kama ilivyo ada na kwa kuwa ni mara yangu ya kwanza naongea kwenye Bunge hili la Kumi na Mbili, naomba nitoe shukurani zangu za dhati kwa Mwenyezi Mungu, nitoe shukrani kwa wapiga kura wangu wa Liwale, nitoe shukrani kwa Chama changu Cha Mapinduzi kwa kuniwezesha kuwepo hapa sasa hivi na kulitumikia Taifa na nawaahidi utumishi uliotukuka. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwenye hotuba ya Rais naomba nijikite katika sehemu moja au mbili; sehemu ya kwanza kabisa nizungumzie suala la kilimo. Ni kweli kabisa Mheshimiwa Rais amedhamiria kufufua kilimo, kwa maana ya kwamba kwenda na kilimo cha kisasa na kufanya mapinduzi ya kilimo. Hata hivyo, hatuwezi kwenda na mapinduzi ya kilimo kama hatujawekeza kwenye utafiti. Ni lazima tuhakikishe tunafufua au tunaimarisha vyuo vyetu vya utafiti, vile vile kujikita kwenye bajeti kwa kuongeza zaidi katika sehemu hiyo ya utafiti.

Mheshimiwa Naibu Spika, mfano mzuri kwenye zao letu la korosho mwaka juzi kwenye Halmashauri yetu ya Wilaya ya Liwale, kulikuwa na ugonjwa wa mikorosho, ilikuwa inanyauka mizima mizima, ilikuwa inanyauka mpaka inafikia kukauka. Kwenye msimu wa mwaka huu, korosho zile zimezaa vizuri, lakini ukibangua ile korosho yenyewe tayari ndani unakuta imeharibika, kwa maana korosho zimeharibika, kitendo ambacho kimeilazimu Wilaya ya Liwale kuuza korosho zake kwa kiwango kikubwa kwenye grade ya pili. Jjambo hili naiomba Serikali kupitia Waziri wa Kilimo ihakikishe tunapeleka wataalam kwenye mashamba haya ya kilimo ili tuweze kugundua tatizo ni nini. Hii ni kwenye upande huo wa utafiti.

Mheshimiwa Naibu Spika, vilevile Mheshimiwa Rais kwenye hotuba yake alizungumzia suala la miundombinu. Ni kweli kabisa jambo la miundombinu huwezi kutenganisha na maendeleo ya watu kama hatujawahi kuunganisha miundombinu. Hapa naunganisha na Sera ya Taifa letu ya kuunganisha mikoa yetu kwa barabara za lami.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba niiambie Serikali Mkoa wa Lindi bado haujaunganishwa na Mkoa wa Morogoro kwa barabara za lami. Mkoa wa Lindi tunayo barabara moja tu inaitwa Kibiti – Lindi ambayo ni kama trunk road. Hata hivyo, barabara hii isiposaidiwa na regional roads hatutapata tija yake.

Mheshimiwa Naibu Spika, hapa naizungumzia barabara inayotoka Nachingwea kwenda Liwale, Nachingwea kwenda Masasi, Ruangwa kwenda Nachingwea, Ruangwa kwenda Kilwa, barabara hizi zisipofunguliwa bado manufaa ya hii trunk road ya Kibiti – Lindi hayataonekana. Naiomba Serikali, pamoja na kwamba tumejikita kwenye kuunganisha mikoa, hizi regional roads tunaweza kuziita feeder roads, ndizo barabara zinazowezesha mazao ya wakulima kufika kwenye masoko kwa urahisi zaidi.

Mheshimiwa Naibu Spika, Kwa hiyo, naiomba Serikali, pamoja na sera ya kuunganisha mikoa Mkoa wa Lindi wauangalie kwa jicho la huruma kwa sababu ni mkoa pekee ambao una barabara moja tu yenye lami ambayo hiyo ni trunk road, regional roads zote ni za vumbi. Naomba sana Mheshimiwa Waziri au Serikali kwa ujumla tuifikirie barabara ya Nangurukuru – Liwale. Barabara hii ni ya kiuchumi na siyo ya kisiasa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa upande huohuo wa miundombinu, tunalo tatizo kubwa sana upande wa wakandarasi. Tunatekeleza miradi mikubwa sana lakini wakandarasi wanachelewa kulipwa. Jambo hili linafanya miradi yetu mingi itumie hela nyingi.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa mfano, barabara inaweza kujengwa labda kwa shilingi bilioni 200, lakini kwa sababu tu mkandarasi amechelewa kulipwa, barabara imeisha ina miaka mitatu, minne mkandarasi hajalipwa, utakuta ile barabara badala ya kujengwa kilometa moja kwa bilioni 1.2 tunajenga mpaka bilioni 1.8 au bilioni 2. Hii yote ni kwa sababu tunachelewa kuwalipa wakandarasi. Kwa hiyo, naiomba Serikali kuhakikisha kwamba wale wakandarasi ambao wanamaliza miradi kwa wakati basi miradi hiyo iishe kwa wakati na wakandarasi waweze kulipwa kwa wakati.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa sababu ya muda, hayo tu mawili yananitosha kwa mchango wangu kwenye hotuba hii. Ahsante sana. (Makofi)