Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Hotuba ya Mheshimiwa Rais, Dkt. John Pombe Joseph Magufuli aliyoitoa wakati wa Ufunguzi wa Bunge la Kumi na Mbili, Tarehe 13 Novemba, 2020

Hon. Prof. Patrick Alois Ndakidemi

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Moshi Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

2

Ministries

nil

Hotuba ya Mheshimiwa Rais, Dkt. John Pombe Joseph Magufuli aliyoitoa wakati wa Ufunguzi wa Bunge la Kumi na Mbili, Tarehe 13 Novemba, 2020

MHE. PROF. PATRICK A. NDAKIDEMI: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru sana kwa fursa hii. Kwa kuwa ni mara yangu kwanza kuchangia katika Bunge lako Tukufu, naomba nimshukuru Mwenyezi Mungu kwa kunijalia uzima na kunipa nafasi ya kuongea hapa nikiwa mwakilishi wa watu wa Jimbo la Moshi Vijijini. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza kabisa napenda nimshukuru Mwenyezi Mungu kwa kutujalia afya. Nataka niwashukuru watu wengi ambao wamenisaidia nikawa Mbunge, nianze kuishukuru familia yangu, namshukuru sana mama pamoja na watoto, nakishukuru sana Chama changu cha Mapinduzi kwa kuniteua nigombee ubunge, nawashukuru wapiga kura wa Moshi Vijijini kata zote 16 walinipa kura za kutosha kuhakikisha nimeshinda kwa kishindo na Mheshimiwa Rais na Madiwani wote 16. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza kabisa nianze kwa kumpongeza Mheshimiwa Rais Dkt. John Pombe Magufuli kwa kazi nzuri ambayo ameifanya toka mwaka 2015 tangu achaguliwe kuwa Rais na kwa hutoba nzuri sana ya kulizindua Bunge hili. Katika hotuba yake Mheshimiwa Rais aliongea mambo mengi makubwa ambayo sisi kama Wabunge endapo tutayazingatia na kama tutaisimamia Serikali vizuri nina hakika tutaacha alama kama moja ya Mabunge bora katika nchi hii. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, niende moja kwa moja kwenye mchango, nitachangia eneo la kilimo mifugo na uvuvi na nafasi ikipatikana nitaongelea miundombinu na sekta ya afya. Tukubaliane Wabunge wenzangu wote waliopo huku ni matunda ya watoto wa wakulima, kama siyo mtoto wa mkulima ni mtoto wa mfugaji, kama siyo mtoto wa mfugaji ni mtoto wa mvuvi. Tukubaliane tu Rais ana nia nzuri ya kuhakikisha kwamba katika miaka mitano ijayo anaboresha sekta hii ambayo nimeitaja ambapo sote sisi ndiyo tumetoka huko. Niombe tu kwamba ni wakati wetu sisi kama Wabunge tumuunge mkono Rais, tuhakikishe kwamba tunarudi kule nyumbani tulikotoka kwa kuziunga mkono hizi sekta ili nao waweze kuongeza kipato na kuchangia katika pato la Taifa na katika uchumi wa nchi yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, niseme tu sekta hii ina changomoto nyingi sana, changamoto mojawapo ni kwamba wakulima wengi wafugaji na wavuvi ni wazee, vijana wetu ambao ndiyo wanategemewa warithi hii kazi hawana interest na hizi kazi za kilimo ama ufugaji ama uvuvi. Niishauri Serikali ikiwezekana tuchukue hatua muhimu kabisa ya kuhakikisha tunawashawishi vijana wetu ili waweze kuwa wakulima, wafugaji na wavuvi.

Mheshimiwa Naibu Spika, ushauri wangu wa kwanza wa Serikali ni kwa Wizara ya Elimu ikiwezekana wabadilishe zile shule zote za kata ambazo ziko karibu na vijijini zifundishe somo la kilimo na Vyuo vya MATI, LITA, VETA, Chuo Kikuu cha Sokoine na Chuo Kikuu cha Mandela ambacho vinafundisha kilimo kwenye mitaala yao waweke component ya ubunifu na ujasiriamali. Kwa kufanya hivyo tutakuwa tunawaandaa hawa vijana ili waje wawe waajiriwa kwenye hii sekta ya mifugo kilimo na uvuvi.

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema hayo, niseme tu kwa kuwa Rais amedhamiria kusaidia hii sekta ya uzalishaji ambayo ni kilimo, mifugo na uvuvi, nishauri Serikali iweke pesa za kutosha kwenye utafiti wa kilimo, mifugo na uvuvi ili waweze kuzalisha mbegu za kutosha na teknolojia ambazo zitatumika kuongeza tija katika kilimo. Tukishazalisha mbegu bora na tukiziwezesha zile taasisi zinazozalisha mbegu kama vile ASA kama vile NIKE pale Arusha watazalisha mbegu bora za kilimo za mifugo na zamaki ambazo zitatumika kuongeza tija na kuwaongezea wakulima wetu kipato.

Mheshimiwa Naibu Spika, eneo jingine muhimu ni eneo la umwagiliaji; Serikali ina nia nzuri ya kuboresha sekta ya umwagiliaji na tukitaka tuzalishe vizuri naishauri Serikali pia iiongezee Wizara ya Kilimo pesa za kutosha ili sekta ya umwagiliaji iweze kupata mshiko. Tukishapata maji ya kutosha nina uhakika tunaweza tukalima mbogamboga. Mbogamboga ni eneo ambalo linaweza likasaidia sana nchi yetu nitatoa mifano na figure kidogo. Ukilima nyanya inayoitwa tanya kwa space ya 60 kwa 60 unapata miche 11,111 kwa hekari moja na mche mmoja wa nyanya unauzwa Sh.1,000, kilo mbili unaweza ukauza kwa Sh.1,000 na ukiuza kwa hekari moja utapata Sh.22,000,000. Ukiuza kwa Sh.500 unaweza ukapata Sh.11,000,000; ukiuza kwa Sh.250 kwa kilo hiyz nyanya unaweza kupata zaidi ya milioni tano. Sasa…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

NAIBU SPIKA: Muda wako umekwisha Mheshimiwa.

MHE. PROF. PATRICK A. NDAKIDEMI: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba tuwa-support wakulima wenzetu. Naunga mkono hoja kwa asilimia mia moja ili tuwaajiri vijana wakulima na watu wengine. Nashukuru sana. (Makofi)