Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Hotuba ya Mheshimiwa Rais, Dkt. John Pombe Joseph Magufuli aliyoitoa wakati wa Ufunguzi wa Bunge la Kumi na Mbili, Tarehe 13 Novemba, 2020

Hon. Sylivia Francis Sigula

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Hotuba ya Mheshimiwa Rais, Dkt. John Pombe Joseph Magufuli aliyoitoa wakati wa Ufunguzi wa Bunge la Kumi na Mbili, Tarehe 13 Novemba, 2020

MHE. SYLIVIA F. SIGULA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru. Nami ikiwa ni mara yangu ya kwanza kuongea katika Bunge hili tukufu, nianze kwa kumshukuru Mungu Mwingi wa Rehema kwa kuendelea kutupa kibali kuiona siku ya leo.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa nafasi ya pekee sana, nakishukuru Chama changu cha Mapinduzi kinachoongozwa na Mheshimiwa Dkt. John Joseph Pombe Magufuli kwa kutuamini vijana na kutupa uwakilishi katika Bunge hili tukufu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, binafsi nimepata bahati ya kuipitia hii Hotuba ya Mheshimiwa Rais zaidi ya mara tatu. Naomba nikiri katika Bunge hili Tukufu, kama kuna hotuba nilizowahi kuzisoma ambazo ni bora, hii ni hotuba nambari moja. Hotuba hii imebeba dira, maono, matarajio na matamanio makubwa sana ya vijana na Watanzania kwa ujumla. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ukianzia ukurasa namba moja mpaka ukurasa wa 41, utaona kabisa Mheshimiwa Rais amegusia sekta zote na zote hizo anamlenga kijana. Unapozungumzia viwanda, unazungumzia wanufaika ambao ni vijana; unapozungumzia nishati, wanufaika wa kwanza ni vijana; unapozungumzia mikopo, wanufaika wa kwanza ni vijana. Kwa hiyo, wakati Mheshimiwa Rais kwenye hotuba yake anazungumzia utengenezaji wa ajira zaidi ya milioni nane, naona ni jambo ambalo linawezekana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, napenda nijielekeze katika ukurasa wa 37 ambapo Mheshimiwa Rais ameelezea kukuza sekta ya sanaa, michezo na utamaduni. Ni wazi kabisa tunafahamu michezo ni ajira na ni kipato; katika kuelezea sekta hii Mheshimiwa Rais amesema kabisa kwamba ataanzisha mfuko ambao utawawezesha wasanii kimafunzo na mikopo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nichangie hapa; kwanza naipongeza Serikali kwa kuanzisha Taasisi ya Sanaa ambapo zamani kilikuwa ni Chuo cha Sanaa Bagamoyo. Taasisi hii inatoa kozi, lakini kozi zinazotolewa pale ni chache. Tukisema tuwezekeze katika sekta ya sanaa tutatengeneza ajira nyingi sana kwa vijana. Tunajua sanaa ipo kwa upana wake mkubwa lakini tunaona sanaa hizi zinawatoa vijana wengi na kuwatengenezea kipato. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nitoe mfano mdogo tu. Juzi tulitembelewa na vijana hapa, tunaweza tukawatengeneza vijana wa aina ile zaidi. Tunaweza tukawatengeneza akina Manula na Boko wengi kutoka kwa vijana wengine. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwenye ukurasa huu wa 37 naomba kunukuu. Rais anasema: “Tutahuisha Mfuko wa Utamaduni na Sanaa ili kuwasaidia wasanii wetu ikiwemo kupata mafunzo na mikopo.” Napenda nijikite hapa, kipengele hiki ni kikubwa sana na kama tutakifanyia kazi vizuri, basi tutatengeneza ajira nyingi kwa vijana. Kwa sababu sekta ya sanaa tukisema tuwekeze kwa nguvu kubwa, itaweza kuwainua vijana wengi.

Mheshimiwa Naibu Spika, nitoe mfano mdogo tu wa mkoani kwetu Kigoma. Tunaelewa kabisa Mkoa wa Kigoma ndiyo kitovu cha sanaa za hapa Tanzania. Ndiyo maana ukifanya tathmini ya wasanii wengi wa Tanzania utaona wengi wanatokea Mkoa wa Kigoma. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ushauri wangu kwa Serikali, naiomba sana Wizara husika ione ni namna gani ya kuboresha na kuwekeza katika sekta hii ya sanaa. Sawa tumeanzisha Taasisi hiyo ya Sanaa lakini bado tuna vijana wengi wa Kitanzania wenye vipaji ambao wakipewa fursa wanaweza wakafanya vizuri. Changamoto katika sekta hii ya sanaa, vijana wengi hawana mitaji. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa sasa tuna chuo hicho kimoja lakini naiomba Serikali kama itawezekana tuweze kuongeza vyuo hivi hata kwa level ya kanda. Itakuwa rahisi kuwahudumia vijana wengi kwani watapata mafunzo pale, lakini hii mikopo ambayo ameisema Mheshimiwa Rais ikawasaidie hawa vijana wajiendeleze. (Makofi)

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa muda umeisha.

MHE. SYLIVIA F. SIGULA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana lakini mada yangu nitaiwasilisha vizuri kwa sababu iko katika mapana yake. Nakushukuru sana. (Makofi)