Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Hotuba ya Mheshimiwa Rais, Dkt. John Pombe Joseph Magufuli aliyoitoa wakati wa Ufunguzi wa Bunge la Kumi na Mbili, Tarehe 13 Novemba, 2020

Hon. Kilumbe Shabani Ng'enda

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kigoma Mjini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Hotuba ya Mheshimiwa Rais, Dkt. John Pombe Joseph Magufuli aliyoitoa wakati wa Ufunguzi wa Bunge la Kumi na Mbili, Tarehe 13 Novemba, 2020

MHE. KILUMBE S. NG’ENDA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi hii na naunga na wenzangu wote….

SPIKA: Kwa wale wengine wasiomfahamu huyu ndio Mbunge wa Kigoma Mjini eeeh! Si mnaelewa.

MHE. KILUMBE S. NG’ENDA: Mheshimiwa Spika, naungana na wenzangu waliotangulia kuutambua utukufu wa Mungu katika kutuweka hapa, naungana pia na wenzangu kukishukuru Chama cha Mapinduzi na wapiga kura wetu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mjadala unaohusu hotuba ya Rais wetu ni mjadala wenye kusudio kubwa moja la kutafsiri dira hii aliyoitoa Rais wetu katika utekelezaji wa kazi za Serikali na Taifa kwa ujumla. Kama ulivyosikia wazungumzaji waliotangulia na wengine hakuna anayekosoa wala kupinga, maana yake wote tunaikubali kwamba hii ni dira ya Taifa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nimepata bahati kuanza kazi za uongozi wa siasa toka kipindi cha mwisho cha Mwalimu alipokuwa anamalizia nafasi yake ya uongozi.

Kwa hiyo, nimepata nafasi ya kujifunza kutoka kwa Mwalimu, kwa Mzee Mwinyi, Hayati Mzee Mkapa na Mzee wetu Jakaya Mrisho Kikwete. Kwa hiyo, wazee wote hawa kwa kweli walikuwa na vipawa mbalimbali ambavyo vimelifikisha Taifa letu mahali hapa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, niseme juu ya Mheshimiwa Dkt. Magufuli, huyu mtu amepewa uthubutu wa aina yake haogopi, hakuna mtu alifikiri kwamba unaweza ukawa Rais usiende nje kupiga magoti kwa wakubwa hawa halafu ukaongoza nchi vizuri, lakini ametufikisha hapo na sasa tunaamini unaweza ukaongoza Taifa la Tanzania bila kwenda kupiga magoti huko nje na shughuli zikaenda. Ni Rais ambaye amekuwa na uwezo mkubwa wa kutafsiri nadharia katika vitendo katika muda mfupi, anaamua jambo hili lifanyike na muda mfupi wananchi wanaona jambo limefanyika. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, hatuna jambo kubwa katika haya tunayozungumza zaidi ya kuonesha kwamba hotuba yake ni dira kwa Taifa letu. Katika kipindi cha miaka ya 1990, Chama chetu cha Mapinduzi kilijikita katika sera ya kutaka kulitoa Taifa letu kuwa Taifa lenye uchumi tegemezi na kulileta kwenye uchumi wa kisasa wa Taifa linalojitegemea. Tumekwenda hivyo katika kipindi chote, lakini sasa tunauona mwanga, mwanga huu tunauona hapa tulipofikia kwenye hatua ya kuwa kwenye uchumi wa kati kwenye kipindi kifupi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ninachokusudia kusema hapa ni kwamba sekta ya viwanda ambayo sasa imetupiga tafu (imesaidia) kubwa ni lazima tuiongezee kasi na katika kuiongezea kasi ni kuiongezea kasi katika kuongeza thamani ya mazao ya kilimo, uvuvi na ufugaji, wenzangu wengi wameshalieleza. Lakini niseme kwa upande wa Mkoa wetu wa Kigoma, sisi tunaweza tukasaidia sana Taifa letu kuondokana na fedha nyingi za kigeni zinazotumika kuagiza mafuta ya kula kutoka nje na Serikali imeanza na Waziri Mkuu huyu Mheshimiwa Kassim Majaliwa amekuwa ndio askari wa mstari wa mbele wa kuhakikisha zao la michikichi linalimwa, linakuzwa na ikiwezekana linavunwa na kusaidia kuondokana na tatizo hilo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, changamoto tuliyonayo, kulima ni mchakato mrefu, na mabenki yetu mengi si rafiki kwa mkulima, miaka mitatu ya kutunza mchikichi mpaka uanze kuzaa ni changamoto kwa wakulima wetu. Kwa hiyo, Serikali iangalie uwezekano wa kutumia fedha, mfuko sijui wa kilimo kwanza kuwapa kama ruzuku wale wakulima ili waweze kusaidia kulima na tuweze kuondokana na tatizo la kuagiza mafuta kutoka nje. Mafuta ambayo siyo tu ni gharama, lakini ni hatari kwa maisha ya Watanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, jambo lingine ambalo nataka niliseme ni lile ambalo Mheshimiwa Rais amelisema katika ukurasa wa 27 wa hotuba yake nalo linahusu…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha muda wa Mzungumzaji)

MHE. KILUMBE S. NG’ENDA: Mheshimiwa Spika, nimesikia kengele naunga mkono hoja mengine tutachangia katika mpango ahsante sana. (Makofi)