Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Hotuba ya Mheshimiwa Rais, Dkt. John Pombe Joseph Magufuli aliyoitoa wakati wa Ufunguzi wa Bunge la Kumi na Mbili, Tarehe 13 Novemba, 2020

Hon. Kunti Yusuph Majala

Sex

Female

Party

CHADEMA

Constituent

Special Seats

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Hotuba ya Mheshimiwa Rais, Dkt. John Pombe Joseph Magufuli aliyoitoa wakati wa Ufunguzi wa Bunge la Kumi na Mbili, Tarehe 13 Novemba, 2020

MHE. KUNTI Y. MAJALA: Mheshimiwa Spika, nikushukuru na mimi kwa kunipatia fursa ya kuweza ushauri wangu katika hotuba ya Mheshimiwa Rais. Nimshukuru Mwenyezi Mungu aliyeweza kutujaalia uhai na afya njema imetusababisha tunaendelea kukutana katika ukumbi huu.

Mheshimiwa Spika, mimi naomba nisemee suala zima la huduma ya afya kwa Watanzania. Mheshimiwa Rais amesema kwenye hotuba yake kwamba tumeongeza vituo vya afya, zahanati pamoja na hospitali za wilaya na mikoa na ukarabati wa hospitali zetu za kanda. Kwenye hili, kujenga vituo vya afya kwa maana ya majengo, kujenga zahanati kwa maana ya majengo, kujenga hospitali za wilaya kwa maana ya majengo bila kuwa na dawa pamoja na vifaatiba na wahudumu kwenye hospitali zetu ni sawasawa na kutwanga maji kwenye kinu, mshahara wake ni kuloa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, niiombe Serikali kama jinsi mlivyojenga haya majengo tunwaomba muende mkawaajiri watumishi wa Wizara ya Afya ili waende kwenye hospitali zetu hizo kuanzia zahanati mpaka hospitali zetu za rufaa waweze kupata huduma.

Pili, muende mkanunue vifaatiba. Asubuhi dada yangu Mheshimiwa Ritta aliuza swali kuhusiana na CT-Scan kwenye hospitali ya Mkoa wa Iringa. Lakini hata sisi Dodoma hapa, CT–Scan tunayo Ntyuka pale ni shilingi 200,000; ni Mtanzania gani anayeweza kumudu kipimo hicho? Kwa hiyo niombe Wizara na Serikali iweze kuona kwenda kununua vifaatiba hivi ili Watanzania wenzetu waendelee kupata huduma iliyo bora ya afya na waimarishe afya zao ili waweze kujenga uchumi wa Taifa letu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwenye suala zima la maji; mwaka 2015 mlituahidi wakati wa kampeni mkatuambia mnakwenda kumtua mwanamke ndoo ya maji kichwani. Watanzania tukaenda tukapiga kura, ndoo ya mwanamke kichwani bado haijatulika kichwani. Bado mwanamke wa Kitanzania hususan anayeishi vijijini anateseka kutembea umbali mrefu akiwa na ndoo yake na mtoto mgongoni anatafuta maji.

Niiombe Serikali safari hii mkija kwenye suala zima la Wizara ya Maji, twendeni tukatenge bajeti ambayo haitakuwa bajeti ya maandishi na maneno na ya kusifiana humu ndani, twendeni tukatenge bajeti itakayokwenda kutekeleza miradi ya maendeleo kama jinsi Mheshimiwa Spika tulivyokwenda kuwekeza kwenye miradi mikubwa Stiegler’s, tumenunua ndege. Basi vivyo hivyo hebu twende tukaone suala zima la upatikanaji wa maji ndani ya Taifa letu ili tuweze kuepuka maradhi, lakini pili tupate fursa ya kupoteza na kuokoa muda ambao tunautumia kwenda kutafuta maji. Muda ule utusaidie kujenga uchumi wa Taifa letu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, waswahili wanasema kitanda usichokilalia huwezi kuwajua kunguni wake. Tunapoomba suala zima la Katiba Mpya, sio kwamba tunaomba ili tuweze kujifurahisha. Tumekuwa hatuna imani na suala zima la Tume yetu ya Uchaguzi na unaweza ukasema Kunti unasema huna imani na Tume ya Uchaguzi mbona wewe uko humu ndani, mimi nilishiriki uchaguzi wa Jimbo yaliyotokea ni mengi. Kwa maoni yetu tunatamani hiyo Katiba Mpya ambayo yale maoni ya wananchi waliyoyatoa kwenye mapendekezo ya hiyo Katiba Mpya ambayo yatakwenda kutupatia Tume Huru ya Uchaguzi yanaweza kutujengea faraja sisi wa vyama vya upinzani pamoja na Watanzania kwenda kuamini tena kwamba tutakuwa kwenye Taifa letu uchaguzi wa huru na wa haki na wa kidemokrasia katika Taifa letu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika,…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha muda wa Mzungumzaji)