Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Hotuba ya Mheshimiwa Rais, Dkt. John Pombe Joseph Magufuli aliyoitoa wakati wa Ufunguzi wa Bunge la Kumi na Mbili, Tarehe 13 Novemba, 2020

Hon. Margaret Simwanza Sitta

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Urambo

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Hotuba ya Mheshimiwa Rais, Dkt. John Pombe Joseph Magufuli aliyoitoa wakati wa Ufunguzi wa Bunge la Kumi na Mbili, Tarehe 13 Novemba, 2020

MHE. MARGARET S. SITTA: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa nafasi hii na mimi nichangie hotuba ya Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. (Makofi)

La kwanza kabisa ni shukrani kwa Mungu ambaye amenipa uhai, lakini la pili shukrani ziende kwa Chama changu cha Mapinduzi ambacho kimenipa nafasi ya kuchaguliwa kuwa Mbunge. Wakati huo huo nawashukuru sana wananchi wa Urambo wamenipa kura nyingi sana najivunia kura zao nawaahidi nitajitahidi kadri ya uwezo wangu nisiwaangushe. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini pia naikumbuka familia yangu imenisaidia sana, nawaombea kwa Mungu nao waendelee vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, umenipa nafasi hii wakati muafaka, nashukuru sana kwa sababu leo umetangaza kwamba kutakuwa na uchaguzi wa TWPG na nimeona ni vizuri nichukue nafasi hii kwa niaba ya wenzangu wote tuliofanya kazi ndani ya TWPG kumshukuru sana Mungu alitupa nafasi tukafanya kazi nyingi sana, ahsanteni sana Wabunge Wanawake mliokuwepo, ahsante sana Wabunge wanaume mliokuwepo wote tulifanya kazi kwa pamoja. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kipekee tukushukuru wewe, akinamama wenzangu Wabunge naomba na kinababa wote waliotuunga mkono tumpigie sana makofi mengi sana Mheshimiwa Spika kwa jinsi alivyotusaidia. Ahsante sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nasema mbele ya Mwenyezi Mungu ametusaidia sana ndugu zangu tulikuwa na shughuli kubwa wa mradi ule unaoendelea wa Bunge Girls High School, bila wewe tusingefanikiwa jamani, ahsante sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nichukue nafasi hii pia kwa niaba ya wenzangu kushukuru ofisi yako bila kumsahau Naibu Spika, Katibu wa Bunge, ofisi yake yote wafanyakazi wa Bunge walisimama mstari wa mbele chini ya uongozi wako tukafanikiwa sasa Waheshimiwa Wabunge tuna Bunge Girls High School, ahsante sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nilifika ofisi kwako kukushukuru na pia nakuaga kwamba tumefanya kazi kwa karibu sana na wewe na ofisi yako na wote nakushukuru sana. Tuwatakie wenzetu mema ambao watakuwa kwenye uongozi unaokuja, lakini muwe na uhakika Spika tunaye. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, baada ya kushukuru kwa upande wa TWPG, nirudi sasa kwa hotuba ya Mheshimiwa Rais. Hotuba ya Mheshimiwa Rais inahitaji sana kupongezwa kwa hali ya juu, mambo mengi yamefanywa, wenzangu Wabunge mliotangulia mmeongelea mambo ya afya ambayo pia imetugusa Urambo, mambo ya maji, umeme, mengi kwa kweli yaliyofanyika pia na sisi yametugusa Wilaya ya Urambo, cha maana tumuombee Rais wetu maisha mema na kuitakia la heri Serikali kwa kuwa kweli Mawaziri, Naibu Waziri na Makatibu Wakuu wanafanya kazi kubwa tuwaombee na kuwatakia kila la heri. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ningeomba kama ifuatavyo, kwa kweli kwa sasa hivi wenzangu wameshaongea sehemu za vijijini barabara ni mbaya, tuombe Serikali yetu iongezee fedha TARURA kwa sababu barabara zetu zinahitaji kutengenezwa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini pia kwa upande wa kilimo, nafahamu kabisa Mawaziri walioko na Serikali kwa ujumla wanajitahidi, lakini bado tuwaombe pembejeo zifike kwa wakati lakini pia mazao yetu yapate bei ya kutosha kwa kupata wanunuzi wengi zaidi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini nishukuru Serikali yetu, tuna VETA zipo na Urambo ninayo lakini kama walivyotangulia kuongea wenzetu ziongezewe aina mbalimbali za ufundi. Nishukuru sana kuona kwenye kipindi kimoja VETA moja tayari inatengeneza simu hayo ndiyo mambo tunayotaka. Kwa hiyo, tunaomba kwamba VETA iongezewe aina mbalimbali za ujuzi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini kwa upande wa wafanyakazi nitakuwa sikutenda haki bila kutajia suala la wafanyakazi, kuna ukurasa hapa ambao unasema Serikali itaendelea kuwajali wafanyakazi. Naomba kwa siku ya leo wafanyakazi kwa kweli wanapopandishwa madaraja warekebishiwe mishahara kwa haraka ili isilete matatizo wanapostaafu. Nina orodha ya walimu wengi ambao wanaendelea kuomba wamestaafu, lakini mishahara yao haikurekebishiwa kwa hiyo, kutengenezewa mafao yao inakuwa shida. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lingine ambalo limejitokeza nashukuru kwamba Serikali yetu imeanzisha mtindo wa e-Government yaani mambo ya kutumia mtandao, wasaidiwe kwa upande wa uhamisho, inawapa tabu sana wafanyakazi.
Baada ya kusema hayo nampongeza Mheshimiwa Rais…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha muda wa Mzungumzaji)

SPIKA: Ahsante sana.

MHE. MARGARET S. SITTA: Lakini bado nakupongeza Mheshimiwa Spika kwa kutusaidia TWPG, Mwenyezi Mungu isaidie TWPG. (Makofi)