Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Hotuba ya Mheshimiwa Rais, Dkt. John Pombe Joseph Magufuli aliyoitoa wakati wa Ufunguzi wa Bunge la Kumi na Mbili, Tarehe 13 Novemba, 2020

Hon. Deus Clement Sangu

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kwela

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

2

Ministries

nil

Hotuba ya Mheshimiwa Rais, Dkt. John Pombe Joseph Magufuli aliyoitoa wakati wa Ufunguzi wa Bunge la Kumi na Mbili, Tarehe 13 Novemba, 2020

MHE. DEUS C. SANGU: Mheshimiwa Spika, kwa kunipa nafasi hii ili na mimi niweze kuchangia hotuba zote za Mheshimiwa Rais, kwanza kabisa ikiwa mara yangu ya kwanza kusimama katika Bunge lako tukufu, nichukue nafasi hii kumshukuru Mwenyezi Mungu aliyenijaalia kuweza kufika mahali hapa. Lakini kwa namna ya pekee wananchi wa Jimbo la Kwela kwa kuniamini kuwa Mbunge wao, naomba niwahakikishie nitawatumikia kwa nguvu zangu zote na uwezo wangu kadri Mwenyezi Mungu atakavyonijaalia. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, katika mchango wangu nimpongeze sana Mheshimiwa Rais kwa namna alivyowasilisha hotuba nzuri sana alipolihutubia Bunge hili la Kumi na Mbili. Kuna mambo mengi mazuri yameelezwa katika hotuba hiyo, lakini mimi kwanza nianze na sekta ya madini. Kweli tupongeze hasa alivyoitendea haki kwa miaka mitano iliyopita ambayo sasa sekta ya madini imeweza kuchangia Pato la Taifa. Kutoka mwaka 2015 ilikuwa ni 3.4% na sasa sekta ya madini inachangia Pato la Taifa kwa 5.2% ni mafanikio makubwa yanastahili pongezi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini katika hotuba yake Mheshimiwa Rais aliongelea jambo kubwa sana na kuutangazia ulimwengu juu ya kuvumbua kwa gesi ya helium ndani ya Bonde la Ziwa Rukwa. Gesi hii inaenda kuleta mapinduzi makubwa katika uchumi wa Tanzania, lakini naomba nitoe rai na juzi nilikuwa nateta na Naibu Waziri wa Madini akanihakikishia kwamba mwezi nne zoezi la kufanya inflation na drilling inaweza ikaanza, changamoto ninayoiona ni maandalizi. Mara nyingi tunakuwa na miradi mikubwa kama hii kwa mfano hii gesi ya helium wasiojuwa ni gesi yenye thamani kubwa na Tanzania tuna ujazo unaokaribia futi za ujazo bilioni 1.38 ambao tunawazidi hadi nchi ya Marekani mara mbili na ambao uchimbaji wa gesi hiyo wao mwaka huu inaelekea kufikia ukomo. Kwa hiyo sisi kama Tanzania tutakuwa tunaweza kuongoza soko hilo la dunia na kuweza kuilisha dunia kwa miaka 20 ijayo na jambo hili liko kwenye Bonde la Ziwa Rukwa ndani ya Jimbo langu la Kwela kuna hekta 3,500. Maandalizi ninayosema ni kuandaa wananchi maana yake huu mradi unaweza kwenda kwao wakaupokea kama tu muujiza kwa kuwa hawakuandaliwa yakatokea mambo kama yale yaliyotokea Mtwara.

Pili, miundombinu naona bado si rafiki sana, nadhani Mheshimiwa Naibu Waziri wa Ujenzi na Uchukuzi wewe ni shahidi siku ya mwaka mpya tulikuwa ndani ya eneo hilo ninalolisema ulijionea hali ya miundombinu ya barabara kuwa ni mibovu, sasa tuna mradi mkubwa kama huu, miundombinu ya barabara ni mibovu kiasi kile na hata Mheshimiwa Waziri Mkuu ni shahidi mwaka juzi ulikuja kule Bonde la Ziwa Rukwa ulijionea mpaka ukaanza kuuliza kuna njia nyingine tutarudi tena tulikotoka, lakini njia ndiyo hizo hizo Mheshimiwa Waziri Mkuu.

Kwa hiyo, niombe tunapokuwa na mradi mkubwa tufanye maandalizi mazuri ili huu mradi uweze kuleta manufaa makubwa kwa taifa lakini kwa watu wale ambao wanaishi maeneo yanayozunguka mradi mkubwa kama huu.

Mheshimiwa Spika, pili nichukue nafasi hii kuongelea sekta ya kilimo na naomba hapa Mheshimiwa Waziri wa Kilimo na Naibu mnisikilize kwa makini. Katika hotuba yake Mheshimiwa Rais ameeleza wazi kwamba tunaagiza ngano kutoka nje karibu tani 800,000 kila mwaka, lakini nitangaze neema ndani ya Bunge lako tukufu, ndani ya Mkoa wa Rukwa tuna ekta zipatazo zaidi ya 60,000 ambazo zimefanyiwa tafiti na zinafaa kwa kilimo cha ngano. Tukiwekeza huko hakika hata hizi shortage ya tani 800,000 itakuwa historia. Tayari Mkoa wa Rukwa hasa katika Jimbo langu la Kwela eneo hilo lipo, nakuomba Mheshimiwa Waziri wa kilimo na Naibu Waziri kama mtaweza yeyote atakayeweza afike huko twendeni mkajionee jambo hili na pia tuitumie Benki ya Maendeleo ya Kilimo kwa maana ya Benki ya Kilimo waje waweze kuwawezesha wananchi ili hii shortage ambayo inatokea, sisi tumeumizwa sana, tumelima kwa nguvu kubwa, mahindi tumezalisha tani nyingi, tumebaki nayo majumbani yanaoza na mwaka huu tumelima sana hatujui tutapeleka wapi walau hii ujio wa ngano hii na sisi tutapata ahueni kama mkoa na kuachana sasa tuanze kugawa tulime nusu mahindi na nusu ngano kwa sababu mahindi yametutesa, hatujui wapi kwa kupeleka na hali ni nguvu pamoja na hayo uzalishaji huu tunaofanya unategemea tu mvua, umwagiliaji miradi mingi tuliyonayo hasa kwenye Jimbo langu ime-prove failure.

Mheshimiwa Spika, ahsante sana na naomba kuunga mkono hoja. (Makofi)