Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Hotuba ya Mheshimiwa Rais, Dkt. John Pombe Joseph Magufuli aliyoitoa wakati wa Ufunguzi wa Bunge la Kumi na Mbili, Tarehe 13 Novemba, 2020

Hon. Abdallah Dadi Chikota

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Nanyamba

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Hotuba ya Mheshimiwa Rais, Dkt. John Pombe Joseph Magufuli aliyoitoa wakati wa Ufunguzi wa Bunge la Kumi na Mbili, Tarehe 13 Novemba, 2020

MHE. ABDALLAH D. CHIKOTA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi na mimi nianze kwa kumshukuru Mwenyezi Mungu mwingi wa rehema ambaye ametuwezesha kukutana katika Bunge hili la Kumi na Mbili, lakini kipekee nikishukuru Chama changu cha Mapinduzi na wananchi wa Jimbo la Nanyamba kwa imani yao kwa kunirejesha tena kwa mara ya pili, nawashukuruni sana. Na niwaahidi Wana Nanyamba kwamba nina nguvu na nitaendelea kuwatumikia kwa nguvu zangu zote ili kuhakikisha changamoto za Nanyamba tunapata ufumbuzi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, hotuba ya Mheshimiwa Rais ina mambo mengi na imetoa maelekezo mengi katika sekta mbalimbali na mimi nitajikita katika sekta mbili, ya kilimo na miundombinu na nianze na sekta ya kilimo. Hotuba imeelezea vizuri kwamba kilimo chetu sasa kinataka kuwa cha kibiashara, lakini Mheshimiwa Rais ametoa ahadi ya upatikanaji wa pembejeo na viuatilifu kwa wakulima tena kwa wakati sahihi na kwa bei nafuu.

Mheshimiwa Spika, sisi Wana-Mtwara zao kuu la uchumi ni zao la korosho. Niiombe Serikali sasa kuwe na mkakati maalum wa kuhakikisha pembejeo ambazo zinatumika kwenye zao la korosho zinapatikana kwa wakati na kwa bei nafuu, lakini sio hivyo tu tuhakikishe kwamba zao la korosho tunapanua soko lake. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kuna minada ambayo inaendelea, lakini tuna TMX, TMX sasa hivi wanashiriki wanunuzi wale wale ambao wanaingia minadani. Hebu TMX iwezeshwe ili tuwapate wanunuzi wakubwa kutoka Vietnam, China na maeneo mengine wasi-bid wale wanunuzi ambao tunawaona kwenye minada. Tuwe na tofauti kwenye TMX tuwaone wale wanunuzi wakubwa na huku kwenye minada tuone wale wa kawaida ambao tunakuwanao. (Makofi)

Vilevile niombe Serikali sasa ielekeze kwenye kuwawezesha wabanguaji wadogo tuongeze thamani korosho badala ya kuuza korosho ghafi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kuhusu miundombinu, naomba niipongeze TARURA kwa kazi nzuri ambayo imeifanya na ambayo inaendelea kuifanya, lakini kama walivyosema Wabunge wenzangu kuna changamoto ya kibajeti. Naomba Serikali itafute chanzo kingine cha fedha ili kuiongezea fedha TARURA ili iendelee kufanya kazi nzuri ambayo inaendelea kuzifanya. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini si hivyo tu, miundombinu kwa upande wetu wa Kusini tuna barabara yetu ya Ulinzi inatoka Mtwara mpaka Newala, Tunduru hadi Songea. Nivipongeze vyombo vya ulinzi na usalama kwa kazi nzuri ambayo vinaifanya katika mpaka huu wetu wa Kusini, mpaka wa Mto Ruvuma, lakini kwa changamoto ya usalama kwa nchi za jirani sasa barabara hii naomba ijengwe kwa kiwango cha lami kutoka Mtwara kwenda Newala, Tunduru mpaka Mbinga na maeneo ya Songea. Barabara hii ni muhimu na ni muhimu kwa ulinzi na usalama wa nchi yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kuhusu miundombinu vilevile kuna changamoto ya Bandari yetu ya Mtwara. Naibu Waziri hapa asubuhi amejibu kwamba kuna uwekezaji wa bilioni 157 zimepelekwa pale na kuna changamoto ya meli kwenda Mtwara, lakini sababu kubwa ni kwa sababu ya zao moja tu la korosho. Mimi naomba Serikali itoe kiwango maalum cha tozo kwa meli zinazoingia Mtwara ili kuvutia wamiliki wa meli wapeleke meli nyingi kwa wakati huu kwa sababu ukiifanya Bandari ya Dar es Salaam na Mtwara kuwa na rate sawa watu hawawezi kupeleka meli Bandari yetu ya Mtwara. Kwa hiyo, naomba sana kuwe na kiwango maalum ili kuwavutia wasafirishaji walete meli Mtwara.

Mheshimiwa Spika, nimalizie na changamoto ya maji. Niiombe Serikali sasa kwamba kwa changamoto ya maji kwa maeneo ya Mtwara tutumie maji ya Mto Ruvuma kujenga miradi mikubwa ya maji.

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha muda wa Mzungumzaji)

SPIKA: Ahsante sana Mheshimiwa Abdallah Chikota.

MHE. ABDALLAH D. CHIKOTA: Mheshimiwa Spika, naunga mkono hoja kwa asilimia mia moja. Ahsante. (Makofi)