Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Hotuba ya Mheshimiwa Rais, Dkt. John Pombe Joseph Magufuli aliyoitoa wakati wa Ufunguzi wa Bunge la Kumi na Mbili, Tarehe 13 Novemba, 2020

Hon. Asia Abdulkarim Halamga

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Hotuba ya Mheshimiwa Rais, Dkt. John Pombe Joseph Magufuli aliyoitoa wakati wa Ufunguzi wa Bunge la Kumi na Mbili, Tarehe 13 Novemba, 2020

MHE. ASIA A. HALAMGA: Mheshimiwa Spika, kwanza nichukue nafasi hii kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa kuniwezesha kufika katika Bunge lako hili tukufu. Nichukue nafasi hii kumpongeza sana Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzaia Dkt. John Pombe Joseph Magufuli kwa kupata kura za kutosha na za kihistoria ambazo toka tumeingia katika chaguzi za vyama vingi uchaguzi wa Dkt. John Pombe Joseph Magufuli ameshinda kwa kishindi, ninampongeza sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nichukue nafasi hii pia kukishukuru Chama chetu Cha Mapinduzi pamoja na jumuiya zake zote kwa kazi kubwa na nzuri wanayoifanya wakati wote na hatimaye tumekwenda kwenye uchaguzi na Chama Cha Mapinduzi tukashinda kwa kishindo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini bila kusahau Jumuiya ya Umoja wa Vijana kwa kuhakikisha kuwa inalinda na kutetea itikadi ya Chama Cha Mapinduzi wakati wote.

Mheshimiwa Spika, nina mengi ya kuchangia lakini kulingana na dakika tano ninaomba niende kwa haraka. Niende kuwasemea vijana ambao wametoka juzi JKT. Vijana takribani 10,000 ambao wamepata mafunzo mbalimbali ya kijeshi na ya kuweza kuzalisha na kutengeneza uchumi katika Taifa letu. Vijana hawa wamekwenda kukaa kwa miaka mitatu Jeshini pamoja na kupata mafunzo, vijana hawa wamerudi mtaani hawana ajira na wote tunafahamu JKT haiwezi kuajiri vijana hawa wote.

Mheshimiwa Spika, niishauri Serikali kuona sasa ni namna gani tunaweza kuwasaidia vijana hawa wakawezeshwa. Mfano, tuna Kambi ya Makutupora ambayo inazalisha zabibu, tuone vijana hawa wanaotoka katika kambi hii na tayari wana mafunzo ya kutosha wanawezeshwa ili na wao waweze kulima zabibu kwa sababu wana ujuzi huo na ikiwezekana Makutupora ipokee zao hilo kutoka kwa vijana hawa na kuwezesha nchi yetu kufikia sasa kile kilimo ambacho ni nia na dhahiri ya Mheshimiwa Rais kupitia hotuba yake. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pamoja na hayo tunao mfano wa Kambi zingine, tuna kambi ya Kigoma kule ambayo inalima mchikichi, tuna kambi ya Ruvu. Wote hawa vijana wana mafunzo ya kutosha, tuone sasa Serikali kwa namna gani inawawezesha kiuchumi ili vijana hawa kwa miaka hiyo mitatu na sasa hivi wako mtaani, hawana mitaji hawajui pa kwenda, hawana chochote. Tunazalisha bomu lingine katika nchi yetu bila kujua utatuzi wa vijana hawa wanapotoka makambini wanakuja kufanya nini huku uraiani. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tunaishukuru Serikali kwa nia njema ya kuwasaidia vijana kwa kutoa mikopo kwa vijana, akina mama na watu wenye uhitaji maalum mikopo ya asilimia 10. Tuombe sasa Serikali ifike ichukue hatua ya kuona mbali zaidi kwa kuwakopesha vijana mmoja mmoja na ikiwezekana Serikali kupitia Halmashauri ijifunze namna gani Bodi ya Mikopo inavyoweza kuwakopesha vijana na kila mwaka kurudisha fedha hizo na basi vijana hawa mmoja mmoja waweze kuaminika na kukopeshwa na Serikali kwa kijana mmoja mmoja badala ya vijana kwa makundi. Ni kweli, njia ya vikundi ni njia sahihi lakini sio vijana wote wanaoweza kupitia makundi kwa sababu hawalingani mawazo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, baada ya kusemea suala la mkopo Serikali yetu ya Chama Cha Mapinduzi kupitia Ilani yake, lakini pia hotuba ya Mheshimiwa Rais lengo ni jema, yote yaliyoandikwa kama dhamira hii tutaichukua, viongozi wa Serikali tukaenda kutekeleza na kusimamia…

(Hapa kengele ililia kuasiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MHE. ASIA A. HALAMGA: Mheshimiwa Spika, ninaunga mkono hoja kwa asilimia zaidi ya 1,000. Ahsante sana kwa kunipa nafasi. (Makofi)