Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Hotuba ya Mheshimiwa Rais, Dkt. John Pombe Joseph Magufuli aliyoitoa wakati wa Ufunguzi wa Bunge la Kumi na Mbili, Tarehe 13 Novemba, 2020

Hon. Joseph Zacharius Kamonga

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Ludewa

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Hotuba ya Mheshimiwa Rais, Dkt. John Pombe Joseph Magufuli aliyoitoa wakati wa Ufunguzi wa Bunge la Kumi na Mbili, Tarehe 13 Novemba, 2020

MHE. JOSEPH Z. KAMONGA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi, lakini pia nianze kwa kumshukuru Mwenyezi Mungu, mwingi wa rehema kwa neema na rehema zote, niwashukuru pia wananchi wa Jimbo la Ludewa na chama changu Chama Cha Mapinduzi (CCM). Nimshukuru pia Mheshimiwa Rais na Serikali yake yote kwa kazi nzuri ambazo zimekuwa zikifanyika na sisi kule Ludewa tumekuwa tukiziona. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nawashukuru sana wananchi wa Jimbo la Ludewa kwa kuniamini na kunituma nije niseme hapa Bungeni kwa niaba yao na vilevile sisi Wanaludewa tumezisoma vizuri hotuba zote za Mheshimiwa Rais na tukajitahidi kuzitafsiri ziendane na mazingira yetu ya Jimbo la Ludewa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nitaanza na eneo la uwekezaji kwenye miradi mikubwa ambayo inaweza ikaongeza mapato ya Taifa letu. Mwaka 1996 Baraza la Mawaziri kupitia Waraka wa Baraza la Mawaziri Na. 06/96 wa mwaka 1996 waliridhia miradi ya Mchuchuma na Liganga iweze kuanzishwa na viwanda vikubwa vijengwe kule. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mwaka 2011, NDC kwa maelekezo ya Serikali na Baraza la Mawaziri waliunda Kampuni ya ubia Tanzania-China International Mineral Resources Limited. Kampuni hii ilikwenda Ludewa na kufanya uthamini kwa nia ya kuwekeza kwenye huu mradi wa Mchuchuma na Liganga, baada ya kufanya upembuzi yakinifu na kujiridhisha eneo lile lina mali za kutosha.

Upande wa Liganga kuna chuma ambapo kampuni hii ingeweza kuzalisha zaidi ya tani milioni 2.9 kwa mwaka na kwa makaa ya mawe wangeweza kuzalisha tani milioni tatu kwa mwaka na ajira za moja kwa moja milioni sita na laki nne na ajira zisizo za moja kwa moja milioni 33. Lakini cha kushangaza ni kwamba mradi huu umekwama.

Mheshimiwa Spika, Wabunge watangulizi wangu wamejitahidi kupambana miradi ianze, lakini hatujaweza kufanikiwa. Wananchi wa Ludewa wana imani na Mheshimiwa Rais, Dkt. John Pombe Magufuli na wanamwalika sana aweze kwenda kutembelea miradi hii mapema iwezekanavyo kwani Wabunge wengi hapa wamekuwa wakilalamika fedha TARURA. Mimi nikuhakikishie Serikali ikiamua kuwekeza kwenye miradi ile tutapata fedha nyingi ambayo itatatua changamoto ya fedha na changamoto ya ajira. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, vilevile upo mradi wa Chuo cha VETA ambao ulianzishwa pale Shaurimoyo ambao nao umekwama kwa muda mrefu sana. Tulikwenda kufanya ziara Desemba na Mheshimiwa Mkuu wa Mkoa na ninamshukuru Rais kwa kutuletea Mkuu wa Mkoa mahiri, Engioneer Marwa Rubirya, tulikwenda naye, watu wa VETA waliahidi Januari wangeweza kuanza kujenga chuo kile, lakini cha kushangaza bado hakijafanikiwa. Kwa hiyo, tunaomba chuo kile kijengwe ili miradi hii inavyoanza na sisi wananchi wa Ludewa na Wananjombe tuweze kupata ajira kwenye miradi ile. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nikienda kwenye Sekta ya Maji; namshukuru Mheshimiwa Waziri wa Maji, nilipata nafasi nikateta naye, akanihakikishia kwamba mambo yatakwenda vizuri. Pale Ludewa kuna mradi ulitengewa shilingi bilioni saba, lakini kwa miaka mitatu zimeletwa milioni 180 tu, kwa hiyo pana mkwamo mkubwa. Tarafa ya Masasi ina changamoto kubwa ya maji, pale Lupingu walitengeneza mradi wa maji ila umesombwa na maji kwa hiyo kuna changamoto.

Na vilevile pale Kiogo kuna wanafunzi huwa wanakwenda kuchota maji kwenye Mto Ruhuhu kwa hiyo wanaliwa sana na mamba. Manda Sekondari kuna changamoto kubwa ya maji na wataalam wamejitahidi kufanya upembuzi yakinifu Kata ya Mawengi na maeneo mengineā€¦

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

SPIKA: Ahsante sana Mheshimiwa Kamonga.

MHE. JOSEPH Z. KAMONGA: Mheshimiwa Spika, nashukuru sana, ahsante. (Makofi)