Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Hotuba ya Mheshimiwa Rais, Dkt. John Pombe Joseph Magufuli aliyoitoa wakati wa Ufunguzi wa Bunge la Kumi na Mbili, Tarehe 13 Novemba, 2020

Hon. Jerry William Silaa

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Ukonga

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Hotuba ya Mheshimiwa Rais, Dkt. John Pombe Joseph Magufuli aliyoitoa wakati wa Ufunguzi wa Bunge la Kumi na Mbili, Tarehe 13 Novemba, 2020

MHE. JERRY W. SILAA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi hii kuchangia hotuba ya Rais aliyoitoa Bungeni akifungua Bunge letu hili la Kumi na Mbili.

Kwanza na mimi kwa sababu ni mara ya kwanza, nitumie fursa hii kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa kunipa fursa mimi kuwa mmoja wa Wabunge wa Bunge lako hili tukufu. (Makofi)

La pili, nikishukuru Chama changu cha Mapinduzi, chama ambacho nimekitumikia kwa zaidi ya nusu ya uhai wangu, kwa kunipa fursa, namshukuru sana Mwenyekiti, navishukuru vikao vya uteuzi na wanachama wenzangu.

Mheshimiwa Spika, naomba kuungana na wenzangu kuunga mkono hoja, lakini vilevile naomba sana kumpongeza Mheshimiwa Rais kwa hotuba hii iliyobeba dira na maelekeo ya nchi yetu kwa miaka mitano. Hotuba hii ukiisoma na ile ya Bunge la Kumi na Moja, ukisoma utekelezaji wa Ilani, ukisoma machapisho mbalimbali ya taarifa ya uchumi, utaona jinsi gani Rais wetu amefanya kazi kubwa kwa miaka mitano, tunampongeza sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, maeneo ya uchumi, uchumi wa nchi yetu umekua, Pato la Taifa limekuwa, mfumuko wa bei umekuwa uko katika hali nzuri, haujazidi asilimia 4.4, akiba ya fedha za kigeni kwa mara ya kwanza iko juu na inaendelea kuongezeka, thamani ya shilingi imeimarika sana, pongezi kubwa kwa Rais wetu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, katika huduma za jamii, kazi kubwa imefanyika, vituo vya afya, zahanati zimejengwa nchi nzima na tumeona kwenye hotuba hii tunayoijadili.

Mheshimiwa Spika, lakini labda kwa kifupi sana ni kuomba Bunge lako tukufu kwamba tuna kazi kubwa baada ya kumpongeza Rais kumsaidia ili malengo aliyoyaweka kwenye miaka hii mitano yatimie na katika kumsaidia wote tuna wajibu wa kumsaidia. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, wa kwanza ni wasaidizi wake, na bahati nzuri tunaye Waziri Mkuu mchapakazi, mpenda watu, anafikika na Waheshimiwa Wabunge mtakuwa ni mashahidi. Lakini wako wasaidizi wake wengine, watendaji wa Serikali nao wanafanya kazi nzuri, tumeanza vizuri. Sisi kule Dar es Salaam katika Jimbo langu la Ukonga, Mkurugenzi wetu Jumanne Shauri na watendaji wenzake wanatupa ushirikiano. Ingawa hatuwezi kuacaha kusema wako watendaji ambao inabidi wabadilike kuendana na kasi ya Rais wetu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, binafsi sina taabu na wewe na ninaamini Wabunge wenzangu hawana shida na wewe, tunafahamu kasi yako. Tumeona juzi hapa Mawaziri walivyokuwa wanajibu maswali ukisimamia Serikali kutoa majibu yanayoendana na shida za wananchi. Niwaombe Wabunge wenzangu, sisi tuna kazi kubwa ya kusaidia Mheshimiwa Rais kufikia malengo haya ya miaka mitano. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Wabunge hawa wamefanya kazi kubwa ya kampeni. Ukiingia hapa asubuhi Wabunge wengi wakiweka sura zao zile mashine zinakataa, siyo kwamba mashine ni mbovu ila sura walizokuja nazo hapa Novemba siyo sura walizonazo leo. (Makofi/Kicheko)

Tumefanya kazi kubwa, Waheshimiwa Wabunge wengine hapa wameosha vyombo, wengine wamepaka rangi kucha, tunayoyasema hapa ndiyo reflection ya matatizo ya wananchi wetu kule tunakotoka, tunaomba tusikilizwe na Waheshimiwa Wabunge, niwaombe tuseme, na wasiposikia tuwafokee. Tufoke kwa niaba ya wananchi tunaowawakilisha. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mimi niliwahi kuwa mmoja wa watu tuliokuwa tunaishauri Serikali kuanzisha TARURA. TARURA imekuja kuondoa matatizo ya urasimu ule wa kihalmashauri wa ujenzi wa barabara, ilikuja kuleta tija kwenye utendaji wa kihandisi, lakini matokeo yake, tulianza vizuri na mameneja wa TARURA wa wilaya, akawa kuna coordinator wa mkoa, leo kumetengenezwa Meneja wa Mkoa, Mhandisi wa TARURA yule Meneja wa Wilaya amegeuka kuwa karani. Hana fedha, hatafuti zabuni, hamlipi mkandarasi, nimshukuru Mheshimiwa Jafo ameanza kulifanyia kazi. (Makofi)

Tulileta jambo lileā€¦

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha muda wa Mzungumzaji)

SPIKA: Ahsante sana Mheshimiwa Jerry Silaa.

MHE. JERRY W. SILAA: Mheshimiwa Spika, naomba kuunga mkono hoja. (Makofi)