Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Hotuba ya Mheshimiwa Rais, Dkt. John Pombe Joseph Magufuli aliyoitoa wakati wa Ufunguzi wa Bunge la Kumi na Mbili, Tarehe 13 Novemba, 2020

Hon. Zuena Athumani Bushiri

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Hotuba ya Mheshimiwa Rais, Dkt. John Pombe Joseph Magufuli aliyoitoa wakati wa Ufunguzi wa Bunge la Kumi na Mbili, Tarehe 13 Novemba, 2020

MHE. ZUENA A. BUSHIRI: Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kuwa ni mara yangu ya kwanza kusimama hapa Bungeni, nimshukuru Mwenyezi Mungu kwa kunipa kibali hiki kwa siku hii ya leo na niwashukuru wapiga kura wangu wanawake wa Mkoa wa Kilimanjaro kwa kunichagua kuingia katika Bunge hili la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, niko katika ukurasa wa 34 wa hotuba ya Mheshimiwa Rais aliyoitoa tarehe 13 Novemba, 2020. Kwanza niipongeze Serikali kwa kutekeleza miradi mikubwa ya maji, 1,423. Hii ni katika sera ya kumtua mwanamke ndoo ya maji. Katika Mkoa wa Kilimanjaro, tunazo wilaya ambazo zina matatizo ya maji na wilaya hizo ni Wilaya ya Mwanga, Same pamoja na Wilaya ya Rombo. Wilaya hizi mbili zimetolewa majibu na Waziri wa Maji asubuhi na bahati Mbunge wa Jimbo la Same aliongozana pamoja na Waziri wa Maji kwenda kuongea zaidi kuhusu mradi huo.

Mheshimiwa Naibu Spika, niongelee kuhusu Mradi wa Maji wa Ziwa Chala ambao ni mradi mkubwa ambao uko katika mipango ya kutekeleza katika Wilaya ya Rombo. Wilaya ya Rombo ina changamoto kubwa sana ya maji, mwanamke anaweza akatoka asubuhi nyumbani kwake, akatumia masaa sita kwenda kutafuta ndoo moja ya maji. Katika kutatua suala hili la maji, kuna mradi mkubwa ambao unatekelezwa katika Wilaya ya Rombo, Mradi wa Ziwa Chala, lakini mradi huu hauna fedha za kutosha. Hivyo, niiombe Serikali iwasaidie akinamama hawa, akinamama ambao wameifanya kazi kubwa sana katika uchaguzi huu kuhakikisha kwamba Chama Cha Mapinduzi kinaongoza Wilaya ile ya Rombo. Tuiombe Serikali ifanye haraka ili mradi huu ukamilike ili tuwatue akinamama ndoo ya maji katika Wilaya ya Rombo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pia nichangie katika ukurasa wa 19 kuhusu sekta ya viwanda, Manispaa ya Moshi Mjini ina viwanda vingi ambavyo vimefungwa amejaribu kuchangia Mbunge wa Jimbo, lakini kama mkazi wa manispaa ile na kama mwanamke ambaye naiangalia Serikali ya chama changu kwamba inao uwezo wa kufufua viwanda vile. Viwanda vile vimefungwa kwa muda mrefu na ni viwanda vingi ambavyo vimekosesha ajira kwa vijana, akinamama na wananchi wa Moshi kwa ujumla. Tuiombe Serikali sasa iwasaidie Manispaa ya Moshi, angalau ajira ziweze kupatikana, viwanda hivyo viweze kufunguliwa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nirudi katika Wizara ya Afya, kwanza niipongeze Serikali kwa kujenga vituo vya afya pamoja na hospitali za wilaya, lakini wilaya zetu hizo zinakuwa bado hazina dawa za kutosha. Tuiombe Serikali na Wizara ya Afya ijaribu kufuatilia na kupeleka dawa katika hospitali zetu za wilaya na vituo vya afya. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nyongeza ya hiyo, kuna changamoto katika Wizara ya Afya, kuna huduma ya mama na mtoto, huduma hii katika maeneo machache ya vijiji watumishi wetu wamekuwa sio waadilifu, kwa kuwa tunavyotambua kwamba huduma hii ya mama na mtoto chini ya miaka mitano inatolewa bure.

Hata hivyo, baadhi ya watumishi wetu wanakuwa wakiwatoza akinamama hata wanapopeleka watoto wao kliniki na hata wanapoenda katika masuala ya kupima uzito tunaiomba Wizara ya Afya, ifuatilie ili iweze kubaini watu hao, watendaji hao ambao wanaichonganisha Serikali yao na wananchi kwa kuwa Serikali inatambua kwamba huduma hii inatolewa bure, wananchi wanakuwa wanajenga chuki na Serikali yao. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba niunge mkono hoja ya hotuba ya Mheshimiwa Rais. Ahsante sana. (Makofi)