Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Hotuba ya Mheshimiwa Rais, Dkt. John Pombe Joseph Magufuli aliyoitoa wakati wa Ufunguzi wa Bunge la Kumi na Mbili, Tarehe 13 Novemba, 2020

Hon. Stella Simon Fiyao

Sex

Female

Party

CHADEMA

Constituent

Special Seats

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Hotuba ya Mheshimiwa Rais, Dkt. John Pombe Joseph Magufuli aliyoitoa wakati wa Ufunguzi wa Bunge la Kumi na Mbili, Tarehe 13 Novemba, 2020

MHE. STELLA S. FIYAO: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru sana kwa kunipa nafasi hii. Jambo la kwanza, nianze kwa kumshukuru Mwenyezi Mungu aliyeniba neema na kibali cha kuwepo katika Bunge hili la Kumi na Mbili. Namshukuru sana Mwenyezi Mungu.

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo la pili, naishukuru familia yangu ambayo imekuwa bega kwa bega na mimi mpaka hatua ya mwisho hata kuipata hii nafasi.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa niende moja kwa moja kwenye kuchangia suala la hotuba ya Mheshimiwa Rais kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, suala la kilimo kwenye Taifa hili limekuwa ni muhimu sana na linahitaji kuchukuliwa kwa uzito wa hali ya juu sana. Endapo suala hili litachukuliwa kwa uzito huo itapelekea kutokutoa shilingi trilioni 1.3 kila mwaka kwa ajili ya kwenda kuagiza chakula nje ya nchi na fedha hii tuielekeze moja kwa moja kwenye pembejeo za kilimo ili wakulima waweze kupata pembejeo kwa bei ndogo na waweze kulima na kupata mazao ya kutosha ikiwa ni sambamba na kuwatafutia soko la mazao. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ni wazi kwamba suala la kilimo limebeba ajira nyingi sana za vijana ndani ya Taifa letu na endapo tutalichukulia kipaumbele, tutapunguza changamoto kubwa ya vijana wetu kukosa ajira ndani ya Taifa letu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, suala la pili ni la wafanyabiashara ndani ya Taifa letu la Tanzania. Suala hili limekuwa changamoto kubwa kwa wafanyabiashara. Issue ya kodi imekuwa ni changamoto kubwa sana ambayo inapelekea wafanyabiashara wengi ndani ya Taifa kukimbia na kwenda kuwekeza katika mataifa mengine kwa sababu ya kukwepa kodi kubwa ambazo wameendelea kuzipata ndani ya Taifa letu.

Mheshimiwa Naibu Spika, nashauri kwamba kuna umuhimuwa kupitia upya Sheria za Kodi kwa wafanyabiashara, kwa sababu kodi hizi zimekuwa ni kandamizi. Huu utaratibu waTRA kuwakadiria kodi wafanyabiashara, unapaswa kupitiwa kwa upya. Wafanyabiashara wamekuwa wakikadiriwa kodi kubwa na wakati mwingine zinazozidi mitaji yao na hivyo kupelekeakukimbia kuwekeza ndani ya Taifa letu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa sababu Mheshimiwa Rais amesema wazi kabisa kwamba anahitaji kodi ziwe rafiki kwa wafanyabiashara, kuna umuhimu mkubwa wa kulichukulia jambo hili kwa uzito ili wafanyabiashara wengi na wa kutoka mataifa mengi waweze kuwekeza ndani ya Taifa letu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, suala la mwisho kabisa, pamoja na kwamba Mheshimiwa Rais ameipongeza Tume ya Uchaguzi kwa kusimamia uchaguzi, lakini ni suala lisilopingika kabisa na ni suala la wazi kabisa kwamba uchaguzi ulikuwa na dosari nyingi. Kutoka hatua ya kwanza kabisa ya zoezi la uchukuaji wa fomu, zoezi la urudishwaji liligubigwa na mambo mengi ya ovyo kabisa. Katika hatua ya kwanza ya uchukuaji wa fomu, wagombea wengi kutoka Vyama vya Upinzani walikamatwa na kupewa kesi mbalimbali. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sambamba na hilo, siku zilivyokaribia za urudishaji wa fomu, hata wale waliokuwa wamebahatika kuchukua fomu, walikamatwa na kupewa kesi, hawakupata kabisa ile nafasi ya kurudisha fomu. Pamoja na hilo, hata wale ambao walipata nafasi ya kurudisha fomu, siku chache baadaye walikamatwa na kupewa kesi.

Mheshimiwa Naibu Spika, ni ukweli usiopingika kabisa, hatuwezi kusema uchaguzi ulikuwa wa huru na haki. Pamoja na hilo, hata tu mara baada ya uchaguzi wananchi walijitokeza kwenda kupiga kura. Watu walipiga kura kwa kujitoa na wengine walikuwa ni wazee, wengine walikuwa ni wanawake wajawazito, lakini watu walivamiwa kwenye vituo vya kupigia kura. Wengine walipigwa, wengine waliumizwa na wengine wameachiwa majeraha mpaka sasa.

Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na hayo, hata mara tu baada ya wananchi kupiga kura, wagombea walitangazwa kabla ya majumuisho. Ni kitu ambacho kinaumiza sana.

MBUNGE FULANI: Taarifa.

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa, wakati natafuta amekaa wapi huyo mtoa taarifa, kengele imeshagonga.

MHE. STELLA S. FIYAO: Mheshimiwa Naibu Spika…

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa muda wako umekwisha. Ahsante.

MHE. STELLA S. FIYAO: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru sana. (Makofi)