Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Hotuba ya Mheshimiwa Rais, Dkt. John Pombe Joseph Magufuli aliyoitoa wakati wa Ufunguzi wa Bunge la Kumi na Mbili, Tarehe 13 Novemba, 2020

Hon. Ng'wasi Damas Kamani

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Hotuba ya Mheshimiwa Rais, Dkt. John Pombe Joseph Magufuli aliyoitoa wakati wa Ufunguzi wa Bunge la Kumi na Mbili, Tarehe 13 Novemba, 2020

MHE. NG’WASI D. KAMANI: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru sana. Kwanza kabisa, nianze kwa kumrudishia shukrani Mwenyezi Mungu, Muumba wa Mbingu na Nchi kwa kutupa kibali wote kuwa hapa jioni hii ya leo.

Mheshimiwa Naibu Spika, pili, kwa nafasi ya kipekee kabisa niwashukuru vijana wote wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kupitia katika Baraza la Umoja wa Vijana wa Chama Cha Mapinduzi kwa imani kubwa waliyonipa ya kuwawakilisha katika Bunge hili la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pia nitumie fursa hii kumshukuru na kumpongeza sana Mheshimiwa Rais kwa kazi kubwa aliyokwishafanya katika nchi yetu kwa miaka mitano iliyopita. Hotuba aliyoitoa katika Bunge hili Novemba, 2020 inatia matumaini makubwa sana kwetu sisi Watanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, suala la ajira limekuwa changamoto kubwa sana kwetu sisi vijana. Mimi kama mwakilishi wa vijana naomba kuungana na Wabunge wenzangu kulichangia suala hili.

Mheshimiwa Naibu Spika, suala la ajira ni mtambuka na linahitaji juhudi za pamoja za Serikali, sekta binafsi, wadau wa maendeleo na sisi vijana wenyewe. Pamoja na hayo, jukumu la msingi bado linabaki kwa Serikali kuhakikisha inawezesha sekta binafsi ili kuzalisha ajira nyingi zaidi nchini. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, takwimu zinaonesha kwamba kuna sababu kuu nne zinazochangia pakubwa sana katika tatizo la ajira katika nchi hii. Naomba nizitaje na zitakuwa pointi zangu za msingi jioni ya leo. Kwanza, ni mifumo ya elimu ambayo ujuzi wake hauendani na mahitaji ya ajira; la pili ni vijana kutokuwa na taarifa na takwimu za fursa za biashara na ujasiriamali zinazowazunguka; ya tatu ni sera za vijana na uwezo mdogo wa kiteknolojia; ya nne ni Serikali kutowekeza vya kutosha kwenye sekta binafsi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, katika suala zima la mifumo ya elimu ambayo ujuzi wake hauendani na mahitaji ya ajira, kwanza kabisa, nianze kwa kuipongeza Wizara ya Elimu kwa kuendelea kuboresha vyuo vya ufundi katika sehemu mbalimbali. Pia nizidi kuwapongeza kwa kutupa ule mfumo wa competence-based system of education ambapo lengo lake kubwa ni kuwawezesha watoto na vijana wanaosoma kupata ujuzi wa msingi wa maisha.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini changamoto kubwa ya mfumo huu ni kwamba walimu ambao wanatakiwa kufundisha vijana wetu bado hata wao hawajauelewa mfumo huu. Utafiti uliofanywa na wanazuoni wa Chuo cha Sokoine unaonesha kwamba asilimia 86 ya walimu bado hawajaelewa dhima kuu ya mfumo huu na asilimia kama 78 ya lesson plans wanazotumia kufundisha haziendani na mfumo huu wa elimu.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuendelea na utaratibu huu kutatufanya tuwe na vijana ambao hawana stadi za kutosha na hawa wakiingia katika soko la ajira, itaongeza changamoto. Ushauri wangu kwa Wizara ya Elimu tuandae utaratibu ambao Walimu na Wakufunzi wataelekezwa upya ili waelewe namna mfumo huu unavyofanya kazi, kwa sababu mfumo huu una faida kubwa ili wao waweze kufundisha vijana wetu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pia niungane na Wabunge wengine walioweka msisitizo katika suala zima la elimu ya stadi ya ujuzi ambayo itaendana na mfumo wa sayansi na teknolojia. Katika hili niishauri Wizara ya Elimu ione utaratibu ambao elimu ya usimamizi wa fedha inaweza ikaanza kufundishwa katika shule zetu kuanzia ngazi ya chini kabisa.

Mheshimiwa Naibu Spika, ni changamoto sana kama vijana hawa ambao wanatoka mashuleni wanakuja, tunawakabidhi fedha na mikopo mbalimbali kutoka kwenye Halmashauri zetu na Serikali lakini hawana elimu ya usimamizi wa fedha. Kwa hiyo, kama tulivyolifanya somo la historia ili kukuza uzalendo, vivyo hivyo somo la usimamizi wa fedha lianze kufundishwa katika shule zetu kuanzia ngazi ya chini kabisa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, katika suala zima la vijana kutokuwa na taarifa na takwimu ya fursa za biashara na ujasiriamali zinazowazunguka, ningependa katika suala hili niongelee mikopo ya Halmashauri, almaarufu 4,4,2 na mifuko mbalimbali ya uwezeshaji wa vijana katika Wizara zetu. Tunaishukuru sana Serikali kwa kuanzisha utaratibu huu na kweli unasaidia vijana, lakini bado kuna changamoto katika utoaji na ufanisi wa mikopo hii.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza kabisa, kuna baadhi ya halmashauri ambazo zinakuwa na mapato makubwa kuliko nyingine. Hivyo vijana ambao wako katika halmashauri zisizo na mapato, wanakuwa na shida kidogo. Tungeangalia utaratibu wa kuweza ku-centralize mfumo huu au Mfuko huu ili vijana wote tuweze kunufaika sawasawa.

Mheshimiwa Naibu Spika, pili, naomba tuangalie utaratibu wa kuweza kupunguza idadi ya watu katika kundi la watu ambao wanaweza kuwa eligible kwa ajili ya kupata mikopo hii. Kundi la watu 10 ni changamoto kidogo. Tuangalie kupunguza list, wawe watano mpaka watatu ili tuweze kupata ufanisi zaidi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, katika suala zima la Mifuko ya Uwezeshaji katika Wizara mbalimbali; kwanza nianze kwa kumshukuru Mheshimiwa Rais, katika hotuba yake ya ufunguzi wa Bunge hili alisisitiza kwamba Mifuko hii iongezewe ufanisi. Mifuko hii ina changamoto kuu tatu; kwanza, mara nyingi haina fedha; na ile yenye fedha huwa mara nyingi ina urasimu mkubwa katika upatikanaji wa fedha zake; na tatu, vijana wengi hawana taarifa ya namna gani fedha hizi wanazipata. Hivyo, nadhani ni jukumu la moja kwa moja la Serikali kuhakikisha kwamba vijana wanapata taarifa zilizo sahihi za fedha hizi na namna gani wanaweza kuzipata fedha hizi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kuanza, nimeamua kuanzisha Kongamano la Vijana na Maendeleo kwa vijana wote nchi nzima, litakalofanyika mwaka huu mwezi wa Saba na litakuwa endelevu kwa kila mwaka, ambapo nitaalika Wizara zote na Taasisi zote za uwezeshaji wa vijana ndani na nje ya nchi, ili tukutane na vijana hao na kuwapa elimu juu ya Mifuko hii na fursa zilizopo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa nawaomba Waheshimiwa Wabunge, pale nitakapokuja kuwaomba ku- support mfumo huu, naomba muwe wepesi ku-support kwa sababu vijana hawa ambao ni asilimia 61.9 wa nchi hii ndio waliokuwa wapiga kura wenu na tuna jukumu la moja kwa moja kuhakikisha tunawasaidia kuwanyanyua kiuchumi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, katika suala la Sera ya Vijana na uwezo mdogo wa kiteknolojia; namshukuru sana Mheshimiwa Rais na sera yake ya Serikali ya Viwanda. Hii imetusaidia sana katika kuzalisha ajira nyingi. Katika Hotuba yake Mheshimiwa Rais ameweka wazi, viwanda vidogo vidogo kama 8,477 vimeanzishwa kati ya mwaka 2015 mpaka 2020; na jumla ya ajira kama 480,000 zimezalishwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, idadi hii bado ni ndogo. Naomba kushukuru sana Wizara ya Kazi na Vijana chini ya Mheshimiwa Jenista, imeanzisha Mfumo wa Green House ambapo itaweka green house hizi katika Halmashauri mbalimbali…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MHE NG’WASI D. KAMANI: Mheshimiwa Naibu Spika, nilikuwa na mengi ya kusema, lakini naamini mengine nitayawasilisha kwa njia ya maandishi.

Mheshimiwa Naibu Spika, mwisho wa yote, naunga mkono hoja. Ahsante sana. (Makofi)