Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Hotuba ya Mheshimiwa Rais, Dkt. John Pombe Joseph Magufuli aliyoitoa wakati wa Ufunguzi wa Bunge la Kumi na Mbili, Tarehe 13 Novemba, 2020

Hon. Zainab Athuman Katimba

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Hotuba ya Mheshimiwa Rais, Dkt. John Pombe Joseph Magufuli aliyoitoa wakati wa Ufunguzi wa Bunge la Kumi na Mbili, Tarehe 13 Novemba, 2020

MHE. ZAINAB A. KATIMBA: Mheshimiwa Naibu Spika, awali ya yote nianze kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa ajili ya baraka zake nyingi sana. Pia nikishukuru Chama changu cha Mapinduzi kwa kuendelea kuniamini. Kipekee kabisa niwashukuru wanawake wa Mkoa wa Kigoma, wapiga kura wangu ambao wameniamini mimi kijana wao niweze kuwa mwakilishi katika Bunge hili Tukufu. Nachowaahidi sitowaangusha. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sisi sote ni mashahidi ya namna gani Serikali ya Awamu ya Tano imefanya jitahada kubwa sana ya kuwawezesha wanawake lakini pia kusimamia masuala ya kijinsia. Hata ukisoma kwenye hotuba hii ya Mheshimiwa Rais, ukurasa namba 4, utaona Mheshimiwa Rais ametoa ahadi na amesema naomba kunukuu: Kwa msingi huo, napenda nitumie fursa hii kuwaahidi kuwa Serikali ninayoiongoza itaendelea kuwaamini wanawake katika kushika nafasi mbalimbali za uongozi. Wanawake na kinamama hoyeeā€¯. (Makofi)

WABUNGE FULANI: Hoyeee.

MHE. ZAINAB A. KATIMBA: Mheshimiwa Naibu Spika, ni katika Serikali ya Awamu ya Tano katika historia ya nchi hii Tanzania tumepata Makamu wa Rais wa Kwanza mwanamke, Mheshimiwa mama yetu Samia Suluhu Hassan ambaye pia amefanya kazi vuziri sana na sisi sote ni mashahidi ni namna gani yeye amedhihirisha uongozi wa mwanamke jasiri. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini sio hivyo tu, kuna mifano mingi ya wanawake wengi ambao wamepewa fursa katika Serikali hii ya Awamu ya Tano ikiwemo wewe mwenyewe Naibu Spika, Mbunge wa Jiji la Mbeya. Tuna Mheshimiwa Jenista Mhagama, aliyekuwa Waziri wa Afya, Mheshimiwa Ummy Mwalimu, tuna viongozi wengi pia kwenye Serikali, Makatibu Wakuu, Naibu Makatibu Wakuu, Wakurugenzi, Wakuu wa Mikoa, Wakuu wa Wilaya, Mabalozi na wote wanafanya kazi nzuri sana. Kwa hiyo, naomba nichukue nafasi hii kusisitiza na kuwaambia wanawake wenzangu tunavyopewa nafasi sisi wanawake tufanye kazi kwa weledi ili tuhakikishe tunajenga taswira nzuri ya uongozi wa mwanamke katika jamii. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ukisoma kwenye ukurasa wa 17 - 19 wa hotuba ya Mheshimiwa Rais, utaona ameelezea mafanikio makubwa ya kiuchumi yaliyofanyika katika kipindi cha miaka mitano. Ameelezea ni namna gani sisi kama nchi tumeingia katika uchumi wa kati, tena tumeingia katika uchumi wa kati miaka mitano kabla ya ule muda tuliotarajia, haya ni mafanikio makubwa sana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwenye ukurasa wa 20 amesisitiza kwamba mipango hii ya kuendeleza na kukuza uchumi wetu itaendelea. Amezungumzia mipango ya kuwawezesha wanawake kiuchumi, masuala ya kuhakikisha kwamba anatoa kipaumbele kikubwa sana katika sekta binafsi lakini pia kutengeneza ajira milioni 8. Kusema kweli mipango mingi ya Serikali ni mizuri, naomba kusisitiza katika maeneo mawili. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kitu cha kwanza, naomba sana Serikali ihakikishe na isimamie katika hiki kipindi kunakuwa na sera, sheria, miongozo na taratibu ambayo inagusa masuala ya uwekezaji, biashara na uchumi isiwe inabadilika sana ili kutoa fursa ya wawekezaji na wafanyabiashara kuzitambua lakini kufanya biashara kwa utulivu. Pia Serikali isimamie utekelezaji wa blue print, kazi kubwa imefanyika lakini sasa tusimamie utekelezaji wa haraka ili kuhakikisha mazingira ya uwekezaji na kufanya biashara yameboreshwa na yamekaa vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, aidha, napenda kuishauri Serikali katika sekta ya elimu. Katika sekta ya elimu sisi tunajenga uchumi wa viwanda, kwa hiyo lazima tuhakikishe tunaandaa rasilimali watu ambao wataenda kuhudumia uchumi wa viwanda. Kwa hiyo, lazima tuwekeze katika kada ya kati kwa sababu ndiyo inayohitajika kwa ajili ya kuhudumia uchumi wa viwanda. Kwa hiyo, nguvu yetu kubwa tuangalie katika zile kada za kati kwa maana yaani tuangalie wale wanafunzi wanaosoma cheti, mafunzo ya ufundi na stashahada, hawa ndiyo wengi watakaohitajika katika uchumi wa viwanda. Hata Bodi ya Mikopo iwawezeshe hawa wanafunzi wa hii kada ya kati ili kuzalisha rasilimali kubwa ambayo itahijika kwa ajili ya uchumi wa viwanda. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mwisho, naomba sana tuangalie katika mtaala ya elimu. Katika mitaala yetu ya elimu tuhakikishe katika masomo yote angalau kuwe na mafunzo ya msingi ya namna gani ya kuanzisha na kuendeleza biashara ili mhitimu anapomaliza chuo hata kama amesoma shahada tuseme ya sociology au political science na anashindwa kuajiriwa katika ajira rasmi basi aweze yeye mwenyewe kuwa mawazo ya namna gani yeye mwenyewe anaweza akaanzisha biashara na kuiendeleza. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naunga mkono hoja na nawaomba sana Watanzania wote kila mmoja wetu ana jukumu la kuhakikisha anatimiza wajibu wake ili ile dhamira ya dhati ya Mheshimiwa Rais ya kulijenga Taifa hili iweze kutimia. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema hayo, nakushukuru. (Makofi)