Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Hotuba ya Mheshimiwa Rais, Dkt. John Pombe Joseph Magufuli aliyoitoa wakati wa Ufunguzi wa Bunge la Kumi na Mbili, Tarehe 13 Novemba, 2020

Hon Ally Juma Makoa

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kondoa Mjini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

3

Ministries

nil

Hotuba ya Mheshimiwa Rais, Dkt. John Pombe Joseph Magufuli aliyoitoa wakati wa Ufunguzi wa Bunge la Kumi na Mbili, Tarehe 13 Novemba, 2020

MHE. ALI J. MAKOA: Mheshimiwa Spika, nikushukuru sana kwa kuniona. Awali ya yote nimshukuru Mwenyezi Mungu kwa neema zake mbalimbali anazotujaalia, lakini pia nimshukuru Mwenyezi Mungu kwa kumuumba mja wake Dkt. John Joseph Pombe Magufuli na akamjaalia kuwa Rais wa nchi hii na yeye akaitendea haki nchi hii kwa kufanya mambo mbalimbali.

Mheshimiwa Spika, kwa kuwa ndiyo mara yangu ya kwanza pia kusimama katika Bunge lako hili,nikishukuru chama changu Chama Cha Mapinduzi kwa kuniteua na kunifanya kuwa Mbunge. Pia niwashukuru wananchi wa Jimbo la Kondoa Mjini kwa kuniamini na kunipa kura nyingi za kishindo na mimi kuwa mwakilishi wao.Ahadi yangu kwao ni kwamba tutafanyakazi kwa bidii kubwa kuhakikisha tunaleta maendeleo kwa wananchi. Vile vile niishukuru familia yangu mama Hashim na watoto wangu wawili kwa kuendelea kunipa nguvu katika kufanyakazi za wananchi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nimepitia hotuba zote mbili za Mheshimiwa Rais ile ya 2015 na hii kwa kweli hotuba zote mbili hizi zimejaa kila aina ya miongozo kwa ajili ya kuliletea neema Taifa hili. Ukweli ni kwamba pamoja na michango yetu yote tutakayochangia bado haitoi maana ya kwamba Serikali hii ya Awamu ya Tano, imefanya mambo makubwa sana katika Taifa hili. Hivyo basi, katika kuchangia mimi nitakwenda ukurasa wa 10, Wizara ya Afya. Serikali ya Awamu ya Tano imepunguza kwa kiwango kikubwa sana vifo vya mama wajawazito na watoto wa umri wa chini ya miaka mitano. Kama tutamsaidia Mheshimiwa Rais kikamilifu basi tutaendelea kupunguza vifo hivi, lakini kama tutazembea, hatutaweza kumsaidia Mheshimiwa Rais, bado vifo hivi vitaendelea kupanda.

Mheshimiwa Spika, kwenye hiki kifungu cha akinamama wajawazito kumekuwa na malalamiko makubwa sana kwa wananchi kwamba sera za afya na Ilani ya CCM, utekelezaji wa sera unakinzana na Ilani ya CCM, Ilani ya CCM inaelezea kwamba tutaendelea kutoa huduma bure kwa akinamama wajawazito na watoto wa umri wa chini ya miaka mitano,lakini uhalisia haupo hivyo. Akinamama wamekuwa wakitozwa gharama katika kujifungua na akinamama wengi katika ziara zangu wamekuwa wakizungumza wengine wameamua kusimamisha kujifungua kwasababu ya gharama kubwa za afya.

Mheshimiwa Spika, juhudi za Serikali za kupunguza vifo zinaweza zikawa zinamikwamo kwasababu wapo akinamama ambao wameamua kujifungulia majumbani kwasababu wanaogopa kwenda kujifungua hospitali wakiogopa gharama. Sasa kama hili litaendelea na wakahamasishana akinamama basi juhudi za Serikali za kupunguza vifo hivi zitakuwa zimekwama.

Mheshimiwa Spika, Jimbo la Kondoa Mjini linaeneo ambalo limetengwa naMto Bubu. Miezi miwili iliyopita tumepata kesi za vifo, mama mjamzito akisubiria maji yapungue aende hospitali kujifungua maji hayakupungua akajifungulia upande wa pili wa barabara, mtoto akafariki,mama wakawa wanamkimbiza wampeleke Hanang, yule mama pia akafariki.

Kwa hiyo kutokana na hali hii iko haja ya Serikali kuona namna gani wanaweza wakasaidia ng’ambo ile ya Kata ya Serya ambayo haina kituo cha afya wala zahanati na wakati huo huo hawana uwezo wa kipindi cha masika kuja mjini kwaajili ya kutafuta huduma za afya.

Mheshimiwa Spika, imekuwa ni kero kubwa sana katika maeneo hayo ambayo yanazungukwa na huo Mto Bubu. Kwahiyo ombi letu watu wa Kondoa tunaomba aidha yafanyike mambo mawili katika moja; kulijenga lile daraja ili watu waweze kufanya shughuli zao za kiuchumi pamoja na kupata huduma za afya au kujenga kituo cha afya katika maeneo yale ya Serya.

Mheshimiwa Spika, eneo la kilimo wako wananchi ambao mashamba yao yaliharibiwa na tembo na wakaahidiwa muda mrefu sana watalipwa kifuta jasho. Mpaka leo watu wale wanadai, hawakulipwa fedha zao, lakini wananchi wa Kondoa wanalalamikia suala la kulipwa kifuta jasho.

SPIKA: Mheshimiwa Makoa, tembo walifika Kondoa Mjini?

MHE. ALI J. MAKOA: Mheshimiwa Spika, jimbo langu lina maeneo ya mjini na vijijini. Ipo Kata ya Kingale na Kata ya Serya ipo pembezoni mwa Hifadhi ya Swagaswaga. Kwa hiyo, tembo wale waliharibu mashamba ya watu lakini vifuta jasho wanavyopewa haviendani na thamani ya mashamba yao. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kama tunataka kupata mabilionea kupitia wakulima basi Wizara ione haja sasa ya kuangalia uwezekano wa kudhibiti tembo wale na kuwalipa wananchi fidia ya maeneo yao na siyo vifuta jasho. Kwa sababu kifuta jasho analipwa pesa ndogo sana ni bora alipwe fidia ili ile dhana ya kuwa na mabilionea kutokana na kilimo basi ipatikane.

Mheshimiwa Spika, eneo lingine ni ajira kwa vijana. Serikali yetu imefanya vizuri sana kutenga asilimia 10 kwa ajili ya vijana. Hata hivyo, katika sera ya mfuko ule nashauri kwamba akaunti ya mikopo ya vijana ingetofautishwa na akaunti zingine za halmashauri ili wakati wa kupanga bajeti ya kuviwezesha vikundi asilimia 10 ya bajeti ya mwaka huu iwe inaendana na zile asilimia 10 zilizopita ambazo zimerejeshwa. Tofauti na ilivyo sasa asilimia 10 inayofanyiwa hesabu ya current year lakini yale marejesho yanaingia kwenye akaunti ya maendeleo. Kwa hiyo, tunashindwa kujua uhalisia hasa marejesho yamekuwa ni kiasi gani na asilimia kumi ya safari hii ni kiasi gani ili kuwawezesha wale vijana, kinamama na walemavu kuweza kupata fedha ambazo zitawasaidia. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, utaona vikundi vingi ambavyo vinapewa mikopo utakuta watu kumi wanapewa shilingi milioni 10, ukipiga hesabu ni shilingi milioni moja moja unashindwa hata kuwashauri wale vijana wafanye biashara gani. Mikopo hii maeneo mengi imekuwa siyo neema kwa vijana, wengi wamekimbia nyumba zao, wameshindwa kulipa madeni kwa sababu wanapewa mikopo kabla ya kupewa elimu ya kuifanyia kazi mikopo hiyo.

Mheshimiwa Spika, niipongeze sana Serikali kwa namna ambavyo imefanya juhudi kubwa ya kujenga miundombinu ya barabara. Hata hivyo, kilio kilekile cha wananchi ni kwamba kipindi hasa hiki cha masika barabara nyingi hazipitiki. Kwa jimbo langu eneo ambalo linashughulikiwa na TANROADS mpaka sasa ni kilomita kama 0.8. Kwa hiyo, unaweza ukaona kwa miaka yote mitano TANROADS wanaweza wasitie mkono au mguu katika jimbo langu. Eneo kubwa linachukuliwa na TARURA, uwezo wa TARURA ni mdogo kwa maana hiyo, tunaomba TARURA waongezewe nguvu kwa sababu barabara nyingi sasa hivi zinashikwa na TARURA.

Mheshimiwa Spika, nashukuru sana kwa kunipa nafasi hii. (Makofi)