Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Hotuba ya Mheshimiwa Rais, Dkt. John Pombe Joseph Magufuli aliyoitoa wakati wa Ufunguzi wa Bunge la Kumi na Mbili, Tarehe 13 Novemba, 2020

Hon. George Ranwell Mwenisongole

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mbozi

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Hotuba ya Mheshimiwa Rais, Dkt. John Pombe Joseph Magufuli aliyoitoa wakati wa Ufunguzi wa Bunge la Kumi na Mbili, Tarehe 13 Novemba, 2020

MHE. GEORGE R. MWENISONGOLE: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi hii. Kwa sababu leo ni mara yangu ya kwanza kusimama katika Bunge hili Tukufu la Kumi na Mbili, nianze kwa kumshukuru Mwenyezi Mungu mwingi wa rehema kwanza kwa kutuwezesha kufika hapa salama na kutuwezesha sisi kushinda uchaguzi mgumu uliopita.

Mheshimiwa Spika, vile vile napenda niwashukuru wananchi wa Jimbo langu la Mbozi Mkoa wa Songwe na Chama changu Cha Mapinduzi kwa kuniamini na kunichagua mimi kuwa Mbunge. Nianze kwa kusema naunga mkono hoja. Hotuba hii ya Mheshimiwa Rais sio tu ni dira kwetu sisi Wabunge, nafikiri ni mwelekeo kwa miaka mitano ijayo kwa Taifa letu. Kuna jambo moja ambalo ningependa nijikite ambalo nikuhusu kilimo. Chama chetu Cha Mapinduzi kwa nia njema kabisa kilileta hii sera ya ushirika kwa nia ya kumsaidia mkulima mmoja mmoja ili awe na uhakika wa masoko na bei yake.

Mheshimiwa Spika, katika maeneo mengi vyama hivi vya ushirika nahisi sijui vina mapepo au vimevamiwa na majambazi, sielewi! Sijaona mahali ambako vyama vya ushirika vimefanya vizuri. Ukienda Kagera, ukija Mbozi, ukienda Mbinga kote ni malalamiko hayo hayo yanayofanana. Kwangu mimi kwenye Jimbo langu la Mbozi vyama hivi vya ushirika sisi kule tunaita AMCOS, huwa wakulima wanapeleka kahawa. Kule kwetu Mbozi, sisi kahawa ndiyo kama dhahabu, sisi hatuna zao lingine tunalotegemea zaidi ya kahawa. Sasa wakulima wakishapima kahawa yao, hawa viongozi wa AMCOS wanachofanya, wanakwenda benki kuchukua mkopo bila wale wakulima wengine kwenye vyama vile vya msingi kujua kwamba wale viongozi wamechukua mkopo. Matokeo yake sasa benki inapokuja kufanya malipo inafyeka yale malipo na kuwafanya wakulima waishi katika hali ya umaskini. Hii hali imeendelea kwa kipindi kirefu sana.

Mheshimiwa Spika, napenda nishukuru juhudi ambazo zimeanza kuchukuliwa sasahivi naOfisi ya TAKUKURU ya Mkoa, ingawa zimekuja kwa kuchelewa lakini bado hatua zaidi, ningependa tunapozidi kufikiria hili suala liingie kisheria. Hawa watu sio tu wafilisiwe nyumba zao, wafikishwe mahakamani na kufungwa. Nafikiri tukiamua kuwa wakali katika hili suala la ushirika na hawa viongozi ambao wanataka kuua ushirika, nafikiri tutakuwa tumemsaidia sana mkulima, kwa sababu kwa muda mrefu sana hawa viongozi wamekuwa wanaishia TAKUKURU tu, wanapewa ratiba ya kurudisha fedha zao, wengine wanahama miji, lakini bado hatujapata solution ya kudumu ya kuokoa maisha ya hawa wakulima ambao bado wanaishi katika hali ya umaskini. Kwa hiyo, napenda kuunga hoja hii ya hotuba ya Rais, lakini hili suala la viongozi waAMCOS ni lazima tuje na solution ya kudumu ili kuhakikisha kwamba wakulima wa chini wanalindwa kutokana na mazao yake.

Mheshimiwa Spika, kingine napenda sana kumshukuru Mheshimiwa Rais, wakati wakampeni alikuja kwenye Jimbo langu la Mbozi na mimi binafsi pamoja na watu wengine tulimweleza shida ya wafanyabiashara pale Mlowo, Vwawa na Tunduma wanavyopata shida na TRA. Rais alikuja tarehe Mosi Oktoba, siku ya Alhamisi. Siku ya Jumatatu yake tarehe 4 alimtuma Kamishna waTRA aje pale Mbozi. Kinachotokea, TRA badala ya kuwa rafiki wanachofanya wakikutana na mfanyabiashara wanamkadiria makadirio ya juu kwa mapato yake, kodi ya juu sana kuliko uwezo wake ili tu akae nao mezani waweze kupata kitu chochote.

Mheshimiwa Spika, matokeo yake ni kwamba TRA imekuwa kama ni fimbo kwa wafanyabiashara na hili ni suala ambalo limekuwa kinyume na maono ya Mheshimiwa Rais. Rais wakati anazindua hili Bunge alisema kwamba angependa TRA na wafanyabiashara wawe marafiki, lakini mahali popote unapokutana na mfanyabiashara, adui yake mkubwa ni TRA. Kwa kweli hili ni suala ambalo kama kweli unataka kumsaidia mfanyabiashara na kuinua mapato ni lazima hawa maafisa wasio waaminifu wa TRA, washughulikiwe.

Mheshimiwa Spika,kwa hiyo kwa kusema hayo machache, naunga mkono hoja. Ahsanteni sana. (Makofi)